Sunday, April 21, 2013

Mwanamke wa Kiislamu Aokoka Baada ya Yesu Kumjia Ndotoni





Katika kukua kwangu, mara zote nilimwona Mungu kama yuko mbali sana. Nilikuwa nikimuogopa sana. Na nilikuwa nikijaribu kumpendeza kwa matendo yangu yote, huku nikijitahidi kubakia safi kulingana na mafundisho niliyopokea, nikiwa kama mwislamu wa kishia.

Nilikuwa nikijitahidi kufanya zile swala 5 kwa siku, huku nikigeukia kwenye Ka’aba, Makka. Pamoja na matendo yangu haya mazuri, nilikuwa sina uhakika ni wapi nitakwenda baada ya maisha haya.

Na tena, kwa sababu ya vita na hali ilivyokuwa nchini, nikiwa nimezaliwa wakati wa mapinduzi na kuona vijana hawa wote waliouawa, nilianza kumhoji Mungu. “Hivi wewe kweli upo ilhali haya yote yanatokea?” Na mara zote mama yangu alikuwa akiniambia, “Nyamaza. Utakwenda motoni. Hutakiwi kumhoji Mungu!”

Kwa hiyo, nilikuwa nikisoma Quran. Kilichokuwa kinanishangaza ni kuwa, nilijifunza kuwa Allah ana majina 99 – kwamba yeye ni Muweza, ni hivi, ni vile; lakini hakuna hata jina moja linalomaanisha upendo!

Kulikuwa na mikanganyiko mingi; maswali mengi na nikawa natafuta kweli halisi. Na hofu kubwa niliyokuwa nayo ni kuwa, kama nikimkataa huyu Allah, ataniadhibu na nitaishia kwenye moto. Nilikuwa nikisema tu, “Inshallah, nitakwenda peponi.”
Maana yake kwamba, “Mungu akipenda, nitaenda mbinguni.” Inakatisha sana tamaa kujua kuwa unaishi kwenye maisha haya bila hasa kuyaishi.

Baadaye nilienda chuo kikuu. Niliona tangazo kwenye ubao kwamba wataonyesha sinema ya Yesu. Kutokana tu na shauku na udadisi, nikasema, “Alikuwa ni nabii mzuri, alitenda miujiza mingi. Nabii niliyekuwa nikimwamini wakati ule hakuwahi kufanya miujiza yoyote, hivyo acha tu nikaangalie sinema hii. Kwani nitapoteza kitu gani?”

Nilienda na kwa mara ya kwanza nilikutana na Waislamu waliobadili dini na kuwa Wakristo. Walikuwa ni madaktari, wengine walikuwa mahaji (waliwahi kwenda kuhiji). Kwa hiyo nilikuwa nasema, ni kitu gani kiliwafanya wamwamini Yesu, si kama nabii mkuu tu, bali kama Mwana wa Mungu; kama Mwokozi wa ulimwengu?

Baada ya kutazama sinema hii, nilianza tena kuhoji mafundisho ya Quran. Maana niliona kwenye sinema ile kwamba Yesu alisulubiwa; alienda msalabani kwa ajili yetu wenye dhambi, kisha akafufuka kutoka kwa wafu siku tatu baadaye na kaburi lake ni tupu!

Hii haikuwa ni namna ambayo nilijifunza kuhusu Yesu; na jinsi alivyozaliwa; alizaliwa Bethlehemu. Quran ilinifundisha kuwa alizaliwa kwenye sehemu tu ya jangwa jangwa. Kulikuwa na mambo mengi yaliyokuwa yanakanganya.

Baada ya kutazama sinema hii walikuja kwangu wakaanza kuongea, na kidogo kidogo nilianza kubishana nao. Kwa namna fulani nilijua kuwa walichokuwa wakisema ni kweli, lakini kutokana na ile roho ya hofu iliyokuwa imenikamata, sikuweza kukubaliana nao. Hasa pale waliposema kuwa sisi sote ni wenye dhambi. Nilisema, “Hapana. Mimi sijatenda dhambi yoyote, uzinzi, ulevi au chochote.”

Nilikuwa naogopa sana kutokana na mafundisho ya Quran niliyofundishwa kwamba tukiukataa Uislamu, tutakwenda motoni. Kwa hiyo niliwaambia, “Mtakwenda motoni.” Nilijaribu kuwashawishi warudi tena kwenye Uislamu, lakini bado walinionyesha upendo. Hilo kwa kweli lilikuwa ni jambo kubwa sana lililogusa moyo wangu. Na kwa mara ya kwanza maishani mwangu niliona Biblia – Agano Jipya.

Na kulingana na tena na mafundisho niliyokuwa nayo, Biblia ni kitabu kilichobadilishwa. Na kutokana na ile shauku ya kutaka kujua ni sehemu gani hizo ambazo zimebadilishwa, nilianza kusoma na kujifunza Biblia.

Na kwa mshangao mkubwa, si tu kwamba sikuona kujikanganya kwa aina yoyote, au kubadilishwa kokote, lakini nikuwa naona tu uthibitisho wa pendo la Mungu kuanzia mwanzo hadi sura ya mwisho!

Siku moja, nilikuwa nimepiga magoti; na nikasema, “Mungu, kwa kweli sitaki kwenda motoni. Kama wewe ni huyu ambaye hawa marafiki wananieleza, tafadhali jidhihirishe! Tafadhali jionyeshe kwangu!”

Na kwa neema kuu ya Mungu, alinitokea kwenye ndoto. Usiku ule, katika ndoto hiyo niliyoota, wanaume watatu waliovaa mavazi meupe, na kandambili za Kirumi; zenye umbo la pembetatu, walisimama mbele yangu. Sikuweza kuona nyuso za wawili kati yao. Lakini yule aliyesimama mbele yangu, alijibu maswali yangu. Maswali ambayo nilienda kulala nayo.

Alisema, “Kwa nini una mashaka sana na mimi, wewe niamini tu.”

Niliamka. Sikuwahi kukutana na Mungu kwa karibu namna ile! Sikuwahi kuzungumza na Mungu kibinafsi namna ile! Maana kwangu mimi, Allah alikuwa mbali sana, juu sana nisikoweza kufika. Ndiyo maana ilikuwa inabidi upitie kwa maimamu au watu wa kati ili kuomba hata sala rahisi tu.

Na nilipoamka, kwa mara ya kwanza amani ilikuja ndani yangu; maana nilijua kuwa ndani yetu kuna utupu au uwazi fulani ambao ni Muumba wetu tu ndiye anayeweza kuuziba.

Kwa hiyo, nilipoamka (asubuhi) naelekea chuoni, ndoto hii ilikuwa kama sinema mbele ya macho yangu. Nilimwita yule dada aliyewahi kwenda kuhiji, nikamwambia, “Nimeota hivi na hivi.” Akasema, “Hatuwezi kuona uso wa Baba au wa Roho Mtakatifu. Lakini kwa imani tu kama Yesu anavyosema, “Kama ukikiri kwamba wewe ni mwenye dhambi na ukanipa maisha yako; na ukaamini kuwa nilikuja kwa ajili yako; kwamba mimi ni Mungu; nilikufa msalabani kwa ajili yako na kwa ajili ya dhambi zako; nilifanyika dhambi kwa ajili yako; nilimwaga damu yangu ili kukusafisha na uchafu huu wote; na nikafufuka tena siku tatu baadaye; umeokoka.”

Kwa hiyo, ni kwa imani tu. Japokuwa nilikuwa bado nahoji kama Yesu ni Mungu; ni Mwana wa Mungu; maana nilikuwa bado nina mawazo ya kimwili juu ya Yesu kuwa Mwana wa Mungu akilini mwangu.

Niliomba sala hii kwa imani tu na baada ya kumaliza, nilijihisi kama unyoya kwenye hewa. Nilijisikia mwepesi mno! Ilikuwa ni kama mizigo mizito inaondolewa kutoka kwangu!

Na wakati fulani nilisoma Biblia tena kwenye sura ya kwanza ya kitabu cha Yohana kabla ya kunjua Bwana na kumkiri kama Bwana na Mwokozi wangu. Nilisoma Biblia na sikuwa na Roho wa Bwana. Kama Roho wa Mungu asipokufunulia kuwa Yesu ni Bwana, hakuna jinsi.

Nilisoma aya ya kwanza: Hapo mwanzo kulikuwako na Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Na sauti ya wazi kabisa kama ninavyoongea na kusikia sauti yangu sasa hivi ndani yangu ilisema, “Angalia aya ya kumi na nne.”
Nilitazama aya ya 14 na inasema: Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu.

Mara moja lile giza liliondoka machoni mwangu! Na kwa mara ya kwanza maishani mwangu nilikiri kwa moyo wangu wote kwamba Yesu ni Bwana. Na hakuna jina jingine humu duniani; chini ya mbingu hizi tunaloweza kuokolewa kwalo, bali ni jina la Yesu!

Yesu Kristo ni Mwokozi wangu; wako; na wa ulimwengu! Niwaambie kaka na dada zangu kwamba, mikono ya Mungu aliyetuumba; aliyejibadili na kuvaa mwli, na kusema, Niko hapa; ninakukubali hivyo hivyo ulivyo. Huna haja ya kuniridhisha mimi kwa matendo yako mema ili upate uzima wa milele. Nakukubali hivyo hivyo ulivyo, na mikono yangu ni mikuu sana na imenyooshwa kukuelekea ili kukupokea kwa upendo; na kukujaza kwa amani, na furaha, na upendo; kiasi kwamba, hakuna jambo maishani litakaloweza kupokonya hiyo amani, furaha na upendo; maana mimi ni mtoa uzima. Mimi siondoi uzima bali natoa uzima. Alisema, Nilikujua wewe kwa jina tangu ulipokuwa tumboni mwa mama yako.

Tunamwongelea Mungu mkuu anayeweza kujaza mioyo yetu; anayejua kinachoendelea ndani kabisa ya mioyo yetu. Yeye ni njia pekee! Hasemi, Mimi ni njia mojawapo, au mimi ni nabii tu. Alisema, Mimi ni njia, na kweli, na uzima. Yeye ni kila kitu. Ndiyo maana alisema tutaijua kweli; kuijua kweli; kumjua Yesu, kutakuweka huru!

No comments:

Post a Comment