Tuesday, June 17, 2014

Niliokolewa Toka Kwenye Nguvu za Giza - Sehemu ya 8




Sura ya 6: Majaribu na Ushindi

Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu.” (Yohana 10:27-28) 

Baada ya kumpokea Kristo, jambo la kwanza lililotokea lilikuwa ni kutoweka kwa zawadi zote ambazo nilipewa kule baharini, yaani teleskopu, TV, mashati, picha nilizopiga kwenye maabara za ndani ya bahari na picha za malkia wa pwani ambazo zilikuwa nyumbani kwangu.


Niliporudi Port Harcourt, nilikuwa na shauku ya kushuhudia yale ambayo Bwana alinifanyia lakini Kanisani hawakuniruhusu. Mke wa marehemu mjomba wangu, ambaye naye ni Mkristo, alinipeleka kwa mchungaji mmoja, lakini swali alilouliza lilikuwa ni, “Amekuja na makaratasi?” Baadaye ndipo nilipokuja kujua kuwa makaratasi yalimaanisha barua ya kuwa mshirika. Barua yangu ya kuwa mshirika ina uhusiano gani na kushuhudia kwangu juu ya nguvu za Kristo na kile alichonitendea Mungu kunihamisha toka kwenye nguvu za giza hadi kwenye ufalme wa Mwanawe mpendwa, ambaye kwa huyo nina ukombozi kwa njia ya damu yake, na hata msamaha wa dhambi?

Nilihuzunika sana, nikiwa ninajua ya kuwa shetani haruhusu waamini wapya kushuhudia, hasa wale ambao mwanzoni walikuwa wamezama ndani kabisa ya mambo yake. Atafanya kila awezalo ili kuzuia shuhuda kama hizo. Tena nakumbuka Bwana aliniagiza wazi kabisa kuwa “nenda ukashuhudie kile nilichokutendea” na hapa nikawa nimekumbana na kukataliwa. Labda muda ulikuwa haujafika. Kwa hiyo niliamua kuweka pembeni habari ya kumshudia mtu yeyote mambo yale. Nilisafiri na wafanyabiashara watatu kutoka Aba hadi Togo kibiashara. Hapo nilinunua bidhaa za thamani ya Naira 160,000. Katiya fedha hizi, za kwangu zilikuwa N70,000 na zilizobakia, yaani N90,000 nilikopa toka kwa wafanyabiashara wa Aba. Miongoni mwa vitu nilivyonunua ni vitambaa vya lesi, dawa mbalimbali (hasa antibiotics), sindano, vipima joto, n.k. Kwenye mpaka wa Naijeria, tulishikiliwa na watu wa forodha na baadaye wakataka tutoe rushwa. Tulikataa na vitu vyetu vikachukuliwa ikiwa ni pamoja na vile vya wenzangu. Miezi michache baadaye, vile vya wenzangu viliachiliwa isipokuwa vyangu. Nilirudi tena baadaye na kukuta vitu vyote vya thamani vilishaibiwa. Nilikagua vitu vilivyobaki na kugundua kuwa kulipa N40,000 kwa watu wa ushuru kungeongeza tu hasara kwangu. Kwa hiyo niliamua kuviacha vitu vile.

Wafanyabiashara ambao niliwakopa fedha walianza kunifuatilia. Baadhi waliita polisi, wengine walijichukulia sheria mkononi na kuamua kuniua. Suluhisho pekee lilikuwa ni kufunga akaunti yangu ya benki na kutumia fedha yote niliyokuwa nayo ili kulipa madeni. Kwa neema ya Mungu, nililipa madeni yote isipokuwa N1,000 ambazo zilikuwa ni kwa ajili ya mwenye nyumba wangu kule Lagos. Nilifilisika kabisa na nilikuwa ninakopa hata N20 kwa ajili ya nauli ya teksi.

Niliwaendea Wakristo wachache niliokuwa nawafahamu, ili kuwaomba msaada niweze kuanza upya. Hakuna aliyesema ndio au hapana. Badala yake nilikuwa naambiwa tu njoo kesho hadi ninachoka au hadi napata msaada kwingineko. Sikujua Neno la Mungu na kutokana na mkanganyiko wote uliokuwa moyoni mwangu, nilikuwa nikisoma Biblia bila kuelewa. Nikiwa bado natafakari cha kufanya, nilipokea ujumbe wa dharura toka kijijini kwangu. Nilikimbia mbio nyumbani na kukuta kile kibanda changu kidogo kilishabomolewa na mjomba wangu ambaye alikuwapo na alitishia kuniua. Tabia yangu ya zamani iliguswa. Nikakumbuka nilipokuwa kwenye kundi la siri jinsi ambavyo aliniogopa na alikuwa akipiga magoti mbele yangu. Lakini sasa alifahamu nilikuwa mtu tofauti (jinsi alivyofahamu, sijui maana tangu niokoke sikuwa nimewahi kufika kijijini kwetu); na sasa alikuwa akitishia maisha yangu. Nilimwita Bwana na kusema, “Kwa hiyo uliniokoa ili uniache nikiwa nimechanganyikiwa na kuruhusu maadui zangu kusherehekea!” Nililia na nikafanya uamuzi wa kurudi tena kwenye lile kundi la siri. Niliwaza kuwa angalau nitaepukana na mkangayiko huu na nitamkomesha huyu mjomba wangu kwa namna ambayo hatasahau maishani mwake.

Japo niliamua hivyo, lakini nilikuwa na hofu kuu mbili ndani yangu:
1. Wakati wa wokovu wangu, Bwana aliniambia waziwazi: “Hii ni nafasi yako ya mwisho.” Nikajua nikirudi kule inaweza kumaanisha kifo, si tu cha kimwili, bali pia cha kiroho.
2. Kama nikibakia kwa Bwana, mjomba wangu atakuwa akinitishia maisha yangu.


Nilichanganyikiwa na nikawa nahitaji msaada. Nilikuwa sijui Neno la Mungu na sikujua linasema nini kuhusiana na mambo hayo. Mpendwa msomaji, utagundua hapa kuwa nilikuwa na mkanganyiko huo wote kwa sababu sikuwa na mtu wa kunifuatilia ningali mwamini mchanga. Kuwafuatilia waamini wapya ni jambo la muhimu sana na Wakristo ni lazima walichukulie jambo hili kwa uzito sana. Kama unajua kuwa hutawafuatilia wale unaowaleta kwa Kristo, tafadhali usitoke kwenda kushuhudia! Yesu Kristo alisisitiza hili mara tatu pale alipomwambia Petro, “Simoni wa Yohana, wanipenda? Akamwambia, Ndiyo, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Chunga kondoo zangu. Waamini wengi wapya hurudi nyuma kutokana na kutokuwa na watu wa kuwafuatilia. Kama unampenda Yesu, basi lisha wanakondoo wake!

Vita na maajenti wa shetani

Wakati huu, maajenti wa malkia wa pwani walianza kunifutilia. Nilipata mateso sana mikononi mwao. Nilikuwa nasumbuliwa na majinamizi. Tarehe 1 Mei 1985, mwezi mmoja baada ya kuokoka, kwenye saa 8:00 usiku, wakati watu wengine kwenye nyumba wakiwa wamelala, niliamshwa na hawa maajenti. Waliniamuru nitoke nje ya nyumba. Nilitii, nikatoka nje na wao wakanifuata nyuma. Yote hayo yalikuwa yanatokea kama kwenye ndoto lakini ilikuwa ni kweli kabisa. Tulienda makaburini karibu na Kanisa la Anglikana la Mt. Paulo, nje ya barabara ya Aba, kule Port Harcourt.

Tulipofika pale wakasema, “Ni lazima urudi. Ukikataa tutakuua au tutakufanya uwe fukara kabisa.” Baada ya maagizo haya, waliondoka. Fahamu ziliponirudia nikaanza kushangaa nimefikaje makaburini! Nilirudi kitandani na kulala. Wakaamua kunishambulia mchana. Wakati mwingine, nikiwa natembea barabarani, walikuwa wakipigana na mimi. Watu wengine wanakuwa wanaona napigana na hewa au kuona nakimbia kama nafukuzwa. Mimi tu ndio nakuwa nawaona. Walifanya hivi mara nne kisha wakaacha. Kisha kiongozi wao, yaani malkia wa pwani, alichukua jukumu hilo. Siku ya kwanza alikuja na gari na kuegesha pembeni mwa nyumba yetu. Alivaa vizuri sana na kama kawaida alikuwa anavutia sana. Watu wengine walichukulia kuwa ni hawara yangu. Mara tu alipofika, nilimtambua ni nani. Alikuja kwenye saa 6:00 mchana wakati eneo lote halina hekaheka nyingi. Alikaa chini, na pamoja na mambo mengine, alisema, “Unaweza kwenda Kanisani, amini unachotaka kuamini, lakini kama hautaeleza habari zangu, nitakupa chochote ukitakacho kwenye maisha haya.” Sikuwa najua Maandiko, kwa hiyo nilimtazama tu akitembea na kuondoka. Alinisihisi na kujaribu kunishawishi nirudi kwake. Sikumjibu ndiyo au hapana. Aliinuka, akaenda kupanda gari lake na kuondoka.  

Kama mara mbili hivi, mke wa mjomba wangu alimkirimu bila kujua ni nani na wala mimi sikumwambia. Mara ya mwisho alibadili mbinu. Safari hiyo alinipa onyo kali akisema kuwa alijaribu safari hizi kadhaa alizonitembelea kunishawishi nirudi kwake lakini nimekuwa mkaidi sana; na kwamba hii ingekuwa ni mara yale ya mwisho kuja. Kama ningekataa kurudi, angekuja kwangu mwezi Agosti na ama ataniua, au ataniharibu sura au atanifanya niwe fukara sana. Baada ya hapo akaondoka.

Niliogopa, kwa hiyo siku moja nilienda Kanisani na kumwita ndugu mmoja. Nilimweleza matatizo yangu na uchunguzi wangu juu ya baadhi ya washirika wa Kanisani, n.k. Ndugu huyu alinipa anwani ya ofisi ya Maandiko [SCRIPTURE UNION (SU)] na kuniambia, “Pale utapata msaada.” Na ikatokea kwamba hiyo ndiyo ilikuwa mara yangu ya mwisho kumwona yule “ndugu”. Sijawahi kumwona tena kokote Port Harcourt hadi leo. Nilichukua anwani ile na siku iliyofuata nilipanda taksi hadi Bonny Street, Na. 108 ziliko ofisi na nikakutana na mpiga chapa ambaye alinipatia programu ya robo mwaka ya shughuli za Kundi la SU la Mahujaji wa Rumuomasi, ambalo ndilo lililokuwa karibu na mimi. Alisema, “Uje Jumapili!” Nilikuwa pale kwenye Fellowship Centre - St. Michael's State School, Rumuomasi – saa 8:00 mchana bila kujua kuwa feloshipu inaanza saa 9:00 mchana; lakini nilikutana na kikundi cha maombi na nikaungana nao.

Baada ya feloshipu siku ile, nilijua kuwa hapo ni mahali pangu sahihi. Mungu alinikutanisha na mwanamke mmoja ambaye nilimchukulia kama mama yangu. Huyu alichukua jukumu la kunifafanulia Neno la Mungu na kunishauri katika mambo mengi. Ndugu walianza kuvutiwa nami na kunijali. Nilikutana na upendo halisi. Roho Mtakatifu alianza kunipa ufahamu wa Neno na imani yangu ikakua. Lakini malkia wa pwani hakuja kama alivyokuwa ametishia. Zaburi 91 kuhusu ulinzi wa Mungu ilitimia kwenye maisha yangu. Isaya 54:17 inasema:  “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa Bwana, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema Bwana.” Haya nayo yalitimia kwangu.

Septemba 1985, nilipokea ujumbe kwamba jina langu lilitokea kama msambazaji wa Simenti Chapa Silver, Lagos; na kwamba nilitakiwa kuripoti kwenye ofisi zao tarehe 27/9/85. Niliondoka Port Harcourt tarehe 26/9/85 na kufika Lagos usiku. Asubuhi iliyofuata tarehe 27/9/85, nilienda kwenye ofisi hizo. Nilijikuta nikiambiwa na Ofisa Utumishi kuwa nafasi yangu alishapewa mtu mwingine. Aliniambia nijaribu tena siku inayofuata tarehe 28/9/85 kumwona Mkurugenzi Mkuu. Nikiwa narudi kwangu, huku nikiwa napita kwenye njia, mtu mmoja alikuja kwa nyuma na kunikamata na akajaribu kuniziba mdomo na pua. Nilishindana naye huku watu wakiwa wanapita tu. Hakuna aliyekuja kunisadia, lakini Bwana aliingilia kati. Huku nikiwa naendelea kuhangaika kwa mikono yangu, alinisukuma huku akisema kwa sauti, “Huyo aliye nyuma yako ni nani?” Alirudia tena kusema hivyo, kisha akatoweka. Kutokana na sauti, nilijua kuwa alikuwa ni mwanamke lakini sikumwona alikuwa nani. Nilipigwa butwaa kisha nikaelekea kwangu.  

Nilipofika kwangu, hapa nako mwenye nyumba yangu akawa amejawa ghadhabu na kusema, “Kwa nini ulikimbia na fedha zangu za kodi?” Nilimsihi sana huku nikijaribu kuelezea kuwa wakati huo sikuwa na fedha na kwamba nikipata tu nitamlipa. Kwa jinsi alivyoniitikia, nilidhani mambo yameisha. Siku iliyofuata tarehe 28/9/85, nilirudi kwenye ofisi ile na kukutana na Mkurugenzi Mkuu ambaye aliomba msamaha kwa kutoa nafasi yangu kwa mtu mwingine. Wakati akiendelea kuongea, kijana mmoja aliingia na kuniuliza, “Wewe sio Emmanuel?” Nikasema, “Ndiyo. Ni mimi.” Akasema, “Ndiyo, tumekupata hatimaye! Umeshamaliza kukimbia? Tumetembelea Port Harcourt mara kadhaa na kukuta mara kwa mara uko na mama yako wa kiroho. Amekuwa ni kikwazo kwetu na sasa kwa kuwa umekuja Lagos, basi tumeshakupata! Hautarudi tena kamwe Port Harcourt! Mimi ndio niliyechukua nafasi yako.”  Nilimpinga na kumwambia, “Huwezi kunifanya chochote!” Mkurugenzi Mkuu alibaki anashangaa kile kinachoendelea. Niliaga na kuondoka kurudi nyumbani.

Dakika chache baadaye, nilisikia mlango ukigongwa na NINA akaingia. Aliniuliza kama nilikuwa na mpango wa kurudi Port Harcourt. Nikasema, “Ndiyo.” Alinisihi sana niende kwao na kwamba kazi ambazo ndizo hasa nilikuwa na ujuzi nazo zilikuwa bado hazijakamilika: KOTIPARI (kwa Kiyoruba). Ujuzi wangu ulikuwa ni:

- kuwa msimamizi wa maajenti wa nguvu za kipepo.
- kuwa msimamizi wa “chumba cha kuongozea cha baharini,” ili kufuatilia yanayoendelea duniani, kutuma na kupokea mawimbi (signals), na kuandaa majeshi, n.k.
- kuwa msaidizi wa malkia wa pwani. Hii ilijumuisha si tu sherehe, kafara, utekelezaji wa majukumu maalum anayotoa yeye, bali pia na mambo mengine ambayo ni vugumu kuyaelezea.
- kwa msaada wa nguvu za giza, kuanzisha makundi mapya ya siri ambayo kwa nje yanaonekana hayana madhara, hivyo kuwavuta vijana na wale waendao Kanisani kwa wingi kadiri iwezekanavyo.  


Alisema, kama ningemsindikiza, kilichokuwa kikiningoja ni kupandishwa cheo mara mbili pamoja na baraka nyingine nyingi. Alikiri kuwa wao ndio waliohusika na kukamatwa kwa bidhaa zangu na kuibiwa. Pia wao ndio waliomfanya mjomba wangu abomoe nyumba yangu na kunitishia maisha. Akasema kuwa, kama ningekataa kufuatana naye, wangefanya zaidi ya hayo na kuhakikisha kuwa sifanikiwi. Kwamba wameamua kupigana na mama yangu wa kiroho: “Kama tukimpata, tutakuwa tumekupata na wewe,” alisema. Alipofika hapo, nilianza kumhubiria. Alisimama na kusema, “Wanakudanganya,” kisha akaondoka. Haya yalitokea jioni ya tarehe 28/9/85.

Hazikupita dakika zaidi ya kumi na tano, nikasikia mlango ukigongwa tena. Safari hii walikuwa wanaume wanne. Waliniashiria kwa mkono nitoke na nikajiona naondoka na wao. Tulitembea kidogo na mmoja wao akaniuliza, “Unatujua sisi ni akina nani?” Nikasema, “Hapana.” Akaendelea kusema, “Tumekodiwa na mwenye nyumba wako tukuue.”

Wakati akiendelea kusema hayo, mmoja wao alitoa bunduki na mwingine akatoa panga. Nilikuwa sina ulinzi wowote na nikajua kuwa wataniua tu. Lakini Mungu kwa njia zake, alifanya muujiza ambao ulinishangaza mimi na hata wao. Yule aliyekuwa ana bunduki aliipiga kwangu lakini hakukuwa na sauti yoyote. Aliyekuwa na panga alipiga mgongoni kwangu lakini halikupenya badala yake lilitoa tu sauti kama fimbo. Waliogopa sana kama nilivyokuwa mimi pia. Roho wa Mungu alikuja juu yangu na nikaanza kuhubiri. Watatu walikimbia, lakini wa nne alianguka chini na kuanza kulia na akanisihi nimwombee. Hata sikujua niombe kitu gani wakati ule lakini nilisema tu, “Bwana, nakuomba umsamehe, usahau, amen!” Alimpa Yesu maisha yake, kwa hiyo nilimpeleka kwenye Kanisa la Pentekoste na kumwelezea Mchungaji kile kilichotokea. Nilipomkabidhi, niliondoka. Wakati nikienda kwenye nyumba yangu, mwenye nyumba alitoka nje na kuja kupiga magoti na kuanza kuniomba akisema, “Tafadhali, naomba unisamehe. Nilidhani uliamua kukimbilia Port Harcourt kwa sababu ya fedha zangu (N1,000).” Nilimsamehe na hatimaye tukakubaliana kuwa fedha hizo nitazilipa kidogokidogo.  

Usiku uleule, kwenye saa 8:00 usiku, Bwana aliniamsha. Sikujua kwa nini niliamka, kwa hiyo nilienda hadi sebuleni, na nilichokiona hapo ni kobe mkubwa sana akiniangalia. Mara moja nilikumbuka mafunzo yangu ya Biblia kule Port Harcourt kuhusiana na nguvu ya Neno. Kisha nikasema maneno haya: “Kobe, tangu nizaliwe, nyumbani kwa kobe, ama ni porini au baharini, lakini kwa wewe kuja kwenye nyumba yangu huku madirisha na milango ikiwa imefungwa, umetenda dhambi, na kwa ajili hiyo, ni lazima ufe!” Mara niliposema hayo, alitoweka. Nilirudi chumbani na kulala. Mara ya pili tena, niliamka na kusikia sauti sebuleni. Nilienda na kukuta hapo mbele yangu, amesimama tai mwenye sura mbaya sana! Nilirudia maneno yaleyale; na mara nilipoyasema, “Kwa kutenda dhambi hii, ni lazima ufe,” alitoweka pia. Wakati wa safari hii ya Lagos, niliuona wema, ukuu na uaminifu wa Mungu.

Asubuhi iliyofuata tarehe 29/9/85, nilipanda basi hadi Port Harcourt. Nilipofika Ore, basi liligonga mti. Liliharibika lakini hakuna aliyeumia. Dereva alilirudisha barabarani na alipokuwa akiendesha, nilikumbuka vitisho vya NINA. Kwa hiyo, nilisimama kwenye basi na kuanza kuhubiri kwa abiria na nikahitimisha kwa kusema, “Ajali hizi zinatokea kwa sababu yangu. Lakini kuanzia sasa, hakutakuwa na ajali tena hadi tunafika Port Harcourt, katika Jina la Yesu!” Kisha nikakaa. Kimsingi, nilipokaa nikaanza kushangaa yale niliyoyasema. Na ikawa hivyo. Gari lilienda salama hadi Port Harcourt. Hakukuwa na ajali tena wala kuharibika kwa gari. Maandiko yanasema sahihi kwamba, “Tazama, yamkini watakusanyana; lakini si kwa shauri langu. Watu wo wote watakaokusanyana juu yako wataanguka kwa ajili yako.” (Isa 54:15) 

Malkia wa pwani na maajenti wake walijaribu, lakini kwa kuwa kukusanyana kwao hakukuwa ni kwa shauri la Bwana, bali ni kinyume cha mtoto wake, wote walijikwaa na kuanguka.

“When the enemy shall come in like a flood, the Spirit of God shall lift up a standard against him” (Isaya 59:19)

 [MAELEZO YA BLOGGER – Ninaacha andiko hili la Isaya 59:19 kwa kiingereza kwa kuwa kwa Kiswahili liko tofauti. --------------Tafsiri ya andiko hili hapa ni kuwa: Adui anapokuja kama mafuriko, Roho wa Mungu humwinulia upinzani.]

Nampa Mungu utukufu wote kwa kujionyesha kuwa mwenye nguvu kwa niaba yangu.
ITAENDELEA ………

5 comments:

  1. ndugu james nimetokea kusoma karibia shuhuda zako zote saa nilikuwa na maswali mawili sijui unaweza nisaidia?
    swali la kwanza je? mtu kuokoka ni maamuz ya mtu mwenyewe au ni neema ya mungu inayomjilia na gafla tu anaacha maovu?.......
    swali la pili..! je yesu alipokufa msalabani amri kumi za mungu ziliishia pale kama sivyo kwanini tena inaruhusiwa kusali hata jumapili.

    ReplyDelete
    Replies
    1. SWALI LA KWANZA JE? MTU KUOKOKA NI MAAMUZ YA MTU MWENYEWE AU NI NEEMA YA MUNGU INAYOMJILIA NA GAFLA TU ANAACHA MAOVU?


      Kuokoka ni mchanganyiko wa mambo kadhaa ingawaje mwisho wa yote, mtu mwenyewe ndiye anayehusika.


      Yesu alipokuwa anaondoka duniani aliacha maagizo haya: Basi, enendeni, mkawafanye MATAIFA YOTE KUWA WANAFUNZI, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku zote, hata ukamilifu wa dahari. (Mt 28:19-20).


      Wale walio ndani ya Kristo tayari wana wajibu wa lazima wa kuhubiri Injili. Ndio maana Bwana akasema:
      (Eze 3:18) Nimwambiapo mtu mbaya, Hakika utakufa; WEWE USIMPE MAONYO, wala husemi na huyo mtu mbaya ili kumwonya, kusudi aache njia yake mbaya na kujiokoa roho yake; MTU YULE MBAYA ATAKUFA katika uovu wake; LAKINI DAMU YAKE NITAITAKA MKONONI MWAKO.


      (Eze 3:19) Lakini UKIMWONYA MTU MBAYA, wala yeye hauachi ubaya wake, wala njia yake mbaya, atakufa katika uovu wake; bali WEWE UMEJIOKOA ROHO YAKO.


      Maandiko haya yanamaanisha kuwa kama mtu amehubiriwa ni wajibu wake YEYE kumkubali Kristo na wala si kwamba kuna jambo la ghafla litakalotokea. Maana ya maneno yasema kuwa TUNAOKOLEWA KWA NEEMA ni kuwa, sisi hatustahili mbele za Mungu kutokana na uasi wetu kwa Mungu aliye Mtakatifu. Lakini Yeye mwenyewe aliamua kuja kutlipia wokovu kwa mauti yake mwenyewe. Neema maana yake ni upendeleo. Kwa vile sheria ya Mungu inasema kuwa mshahara wa dhambi ni mauti, lakini Yeye akaamua aibebe hiyo mauti badala ya sisi tunaohusika, basi huo ni upendeleo mkubwa (neema).


      Ndipo Yesu akasema:

      Tazama, nasimama mlangoni, nabisha; mtu AKIISIKIA sauti yangu, NA KUUFUNGUA mlango, NITAINGIA kwake, nami nitakula pamoja naye, na yeye pamoja nami. (Ufunuo 3:16).


      UKIMKIRI Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, NA KUAMINI moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana, kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu. (Waebrania 10:9-10).


      .......nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; BASI CHAGUA uzima, ili uwe hai, wewe na uzao wako. (Kumbukumbu 30:19)


      Maneno niliyoandika kwa herufi kubwa yanaonyesha jinsi ambavyo mtu mwenyewe anahusika kukubali wokovu wa Kristo.



      SWALI LA PILI..! JE YESU ALIPOKUFA MSALABANI AMRI KUMI ZA MUNGU ZILIISHIA PALE KAMA SIVYO KWANINI TENA INARUHUSIWA KUSALI HATA JUMAPILI.

      Amri za Mungu hazijaishia msalabani. Ndio maana Bwana Yesu akasema:

      (Yoh 13:34) Amri mpya nawapa, Mpendane. Kama vile nilivyowapenda ninyi, nanyi mpendane vivyo hivyo. Ukiwa na upendo kwa watu, hutawafanyia kile ambacho wewe usingependa kufanyiwa – hutawakosea wazazi adabu, hutaiba, hutazini, hutadanganya, n.k.

      Kuhusiana na suala la kusali jumapili, naomba uende kwenye sehemu ya FREE E-BOOKS. Download e-book inayoitwa Je, Sabato ni Siku katika Juma? Humo nimeeleza kwa kirefu sana juu ya Jumamosi na Jumapili.

      Delete
  2. jina langu naitwa EMMANUEL MMBAGA .......
    nipo pia facebook natumia jina la frank mmbaga(faithfull) tafadhali nijibu .....au kama unatumia na wewe facebook njoo inbox kwangu .

    ReplyDelete
  3. nashukuru sana kwa ufafanuZi wako MUNGU akubariki sana john.

    ReplyDelete