Monday, March 26, 2012

Jinsi ya Kuenenda kwa Roho



Maandiko yanasema kwamba: Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani. Kwa kuwa ile nia ya mwili ni uadui juu ya Mungu, kwa maana haitii sheria ya Mungu, wala haiwezi kuitii. (Warumi 8:6-7).

Ndugu, yapo mashindano makali sana ndani mwetu ambayo yanaendelea kila dakika ya maisha yetu. Mwili unataka hivi na roho inataka vile. Wewe na mimi tuko hapo katikati. Uamuzi unatoka kwetu – ama kufuata mwili au kufuata roho!

·          Ukipanda daladala, halafu kondakta akawa hajakudai nauli kabisa hadi ukafika wakati na kushuka, iko sauti inayokwambia, “Lipa.” Sauti nyingine inasema, “Nenda tu.”
·          Ukivaa vazi lisilo sawa, sauti moja inakwambia, “Badili uvae nguo nyingine.” Sauti nyingine inasema, “Mbona wanaovaa hivi wengi tu.”
·          Mtu akikukosea, sauti moja inasema, “Msamehe.” Ya pili inasema, “Asikuchezee huyo!”

Kwa kifupi, sauti ya kwanza ni hiyo inayoitwa “nia ya roho” katika andiko la Warumi hapo juu. Na ile ya pili ndiyo “nia ya mwili.”
Na tunaambiwa wazi kwamba nia ya roho mwisho wake ni uzima na amani, lakini nia ya mwili inamfanya mtu awe na uadui na Mungu!

Sauti hizi zipo kwenye karibu kila eneo la maisha yetu; tangu asubuhi hadi asubuhi inayofuata; kila siku; kila dakika!
Lakini mara nyingi tunajikuta tunaishi kwa kuitii ile nia ya mwili (japo wengi wetu hatujitambui kama tuko namna hiyo). Paulo anasema: Kwa maana lile jema nilipendalo silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo. (Warumi 7:19).

Ndiyo! Hivyo ndivyo tulivyo mara nyingi. Tunaishi kwa kuifuata nia ya mwili.

Yesu anasema wazi, Makwazo hayana budi kuja. (Luka 17:1). Lakini sasa, yakija unatii nini? Unatii roho au mwili? Na matokeo ya huo uchaguzi ni nini? Imeandikwa: Hamjui ya kuwa kwake yeye ambaye mnajitoa nafsi zenu kuwa watumwa wake yule mnayemtii, kwamba ni utumishi wa dhambi uletao mauti au kwamba ni utumishi wa utii uletao haki. (Warumi 6:16).

Wengi tunasema, “Nataka kuisikia sauti ya Mungu.” Sikatai kwamba Mungu huzungumza wakati mwingine kwa sauti ya kusikika kabisa, lakini sauti ya Mungu ipo ndani yetu KILA DAKIKA! Na hapa ndipo pa kuanzia.

Jifunze na ujizoeze kusikiliza moyo wako katika kila jambo. Utaanza kuyaona kwa uwazi mambo yaliyo kinyume na Neno la Mungu (Hapa ieleweke kwamba lazima usome Biblia ili Neno hilo liwe ndani yako ndipo utaweza kujua lipi ni kinyume na Neno na lipi ni sawa na Neno). 

Pia utaweza kuitambua ile sauti ya Roho Mtakatifu inayokushauri katika kila jambo na kukupitisha kwenye njia ya haki. Atakushauri kupitia hilo Neno uliloweka moyoni mwako. Ndiyo maana ya neno lisemalo: Moyoni mwangu nimeliweka neno lako nisije nikakutenda dhambi. (Zaburi 119:11).

Kisha anza kuifuata sauti hiyo. Bwana anasema: Basi nasema, Enendeni kwa Roho, wala hamtazitimiza kamwe tamaa za mwili. Kwa sababu mwili hutamani ukishindana na Roho, na Roho kushindana na mwili; kwa maana hizi zimepingana, hata hamwezi kufanya mnayotaka. (Wagalatia 5:16).

·               Kondakta akikusahau, mkumbushe na umlipe.
·               Roho akikuambia samehe, tii kwa kusamehe hata kama una kila haki ya kumkasirikia aliyekukosea; n.k.

Biblia pia inasema kuhusu wana wa Israeli: BWANA naye akawatangulia mchana ndani ya wingu mfano wa nguzo, ili awaongoze njia; na usiku, ndani ya moto, mfano wa nguzo, ili kuwapa nuru, wapate kusafiri mchana na usiku; ile nguzo ya wingu haikuondoka mchana, wala ile nguzo ya moto haiukuondoka usiku, mbele ya hao watu. (Kutoka 13:21-22).

Hiyo sauti iliyo ndani yako na ndani yangu, ndiyo nguzo ya wingu na nguzo ya moto inayotuongoza mchana na usiku katika maisha haya. 

Bwana anasema na kila mwanadamu wakati wote. Ni uchaguzi wetu kutii au kukataa kutii. Lakini ni heri kutii kuliko kuasi.

Imeandikwa: Kondoo wangu waisikia sauti yangu; nami nawajua, nao wanifuata. Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe; wala hakuna mtu atakayewapokonya katika mkono wangu. (Yohana 10:27-28). Mtii BWANA!

Bwana akubariki unapoenda kumtii katika kila jambo maishani mwako; na hakika, utafika salama kwenye Kanaani iliyo mbele yako!

1 comment: