Saturday, June 7, 2014

Niliokolewa Toka Kwenye Nguvu za Giza - Sehemu ya 7



Sura ya 5: Kukutana kwangu na Yesu Kristo

Mwezi wa February 1985, tulikuwa na mkutano wetu wa kawaida baharini. Baada ya hapo niliamua kusafiri hadi Port Harcourt kwenye Jimbo la Rivers, kumtembelea mke wa marehemu mjomba wangu. Nilikutana na mtu aliyeitwa Anthony. Alikuwa na karakana yake kule Nwaja Junction, kwenye barabara ya Trans-Amadi, Port Harcourt, Jimbo la Rivers. Alituma ujumbe niende kwake na kwa kuwa kwenye kundi letu tuna sheria kwamba usikatae wito, niliamua kwenda. Nilienda kwake mchana siku ya Alhamisi. Alianza kwa kusema, “Mungu amenipa ujumbe kwa ajili yako.” Alitoa Biblia yake na kuanza kuhubiri. Kulikuwa na Wakristo wengine watatu wamekaa (mwanamume na wanawake wawili). Aliendelea na mahubiri yake kwa muda mrefu na sina uhakika kama niliyasikia yote. Hatimaye aliniambia nipige magoti kwa ajili ya kuombewa. Nilitii na nikapiga magoti kimyakimya.


Mara moja alianza kuomba. Nilisukumwa na Roho wa Mungu na nikaanguka chini. Nikawa nahangaika kuinuka na nikasimama kama chuma. Niliharibu viti vya chuma ndani ya ile karakana. Nilitazama nje na kuona watu watatu kutoka kwenye kundi letu la siri; mwanamume na wasichana wawili. Walikuja kwa maumbo ya kibinadamu na wakaelekea mlango lakini kutokana na nguvu ya Mungu, hawakuweza kuingia.

Nina uhakika kuwa alamu kule baharini iliwajulisha kuhusiana na tatizo lililokuwapo; na kupitia TV, walijua tatizo liko wapi na wakatuma timu ‘isiyo na nguvu’ kuja kuniokoa. Hii hutokea kila wakati mwanachama wetu anapofikwa na matatizo. Wakati wale wanaume wawili Wakristo wakinivuta nipige magoti, wale wasichana waliendelea kuomba na kuyafunga mapepo, lakini hawakuwa wakilenga mapepo yoyote maalum. Waliniuliza endapo nilikuwa namwamini Yesu Kristo, nikakaa kimya. Waliniambia niite Jina la Yesu, nikakataa. Waliniuliza jina langu nami nikawaambia. Walihangaika kwa saa kadhaa kisha wakaniacha niende. Hakuna pepo hata moja lililotolewa kwangu, kwa hiyo nilitoka kama nilivyokuja.

Tukio la Kanisani
Siku iliyofuata, Ijumaa, nilialikwa na yuleyule Anthony kwenye mkesha katika Kanisa la Assemblies of God, Silver Valley, Port Harcourt. Nilikubali mwaliko huu kwa sababu kwenda makanisani ili kusababisha usingizi na machafuko ilikuwa ni mojawapo ya majukumu yetu. Ibada ilianza kwa nyimbo. Tuliimba hadi mmoja wa washirika alipoanzisha wimbo maarufu wa bendi moja ya Kikristo, unaosema kuwa hakuna nguvu nyingine iliyo juu ya nguvu za Yesu.

Nilianza kucheka. Nilicheka kwa sababu nilipokuwa kwenye roho na kuwaangalia maisha yao, robo tatu ya waliokuwa wakiimba wimbo ule walikuwa ni watu wanaoishi kwenye dhambi. Nilijua hilo kwa sababu ya dhambi kwenye maisha yao. Walikuwa wako wazi kiasi kwamba wangeweza kudhuriwa vibaya sana na nguvu hizo. Ni muhimu kwa Wakristo kutii Neno la Mungu na sio kuruhusu dhambi kubakia kwenye maisha yao. Katika ibada ile, tulikuwapo wanne kutokea baharini na tulikuwa tukiimba na kupiga makofi pamoja nao. Nataka pia kusisitiza hapa kwamba, ibada inapoanza, ni muhimu waumini washauriwe kwanza kukiri na kutubu dhambi zao, ndipo waingie kwenye kipindi cha kumsifu Mungu.  Hii inamfanya ajenti wa shetani aliyepo humo akose kabisa raha na kimsingi atakimbia ili kuponya maisha yake.

Katika ibada hii, tulikuwa na amani kabisa na hata tulianza kufanya mambo yetu. Wengi walianza kusinzia, nyimbo ziliimbwa kwa udhaifu na mambo yalikuwa hovyohovyo tu. Anthony alishawaeleza kuhusiana na mimi, hivyo kwenye saa 8:00 usiku waliniita ili waniombee. Mara tu nilipotoka mbele, walianza kusihi damu ya Yesu. Niliwasimamisha na kuwaambia, “Kusihi damu ya Yesu si suluhisho. Mimi ni mwanachama wa kundi la siri. Kama mkikubali kuwa mnaweza kunifungua mimi, basi nitapiga magoti.” Maneno haya sikuwa nimeyapanga kuyasema. Damu ya Yesu huwatisha mapepo na inawalinda waamini, lakini haiwafungi mapepo. Mapepo hufungukika pale tu Mkristo anapotumia mamlaka yake na kutoa amri.

Walikubali na nikapiga magoti. Wakati huu, dada mmoja akiongozwa na Roho wa Mungu alipaza sauti na kusema, “Kama unajijua hustahili, usikaribie hapa!” Nina uhakika wengi hawakumwelewa alichomaanisha. Ni hatari sana kwa Mkristo anayeishi katika dhambi kukemea mapepo. Wengi waliondoka na wachache wakaja kuniombea. Walipoanza kusema “kwa Jina la Yesu”, nilisikia kishindo kikubwa ndani yangu na nikaanguka chini! Mara moja pepo lirukalo ndani yangu lilianza kazi. Nikaanza kukimbia kwa kifua changu. Mtu yeyote mwenye pepo hili lirukalo huwa ni mwovu na wa hatari sana. Ndugu wale hawakuona kilichokuwa kikiendelea kwenye ulimwengu wa roho. Nilikuwa ninakimbia kutokana na nguvu kubwa iliyokuwamo kwenye chumba kile.

Nguvu mbili zinazopingana zilianza kupambana na anga likawa limebadilika. Ghafla nilisimama na nikawa mkali sana, mwenye vurugu sana, n.k. Pepo lilitoka kwangu na kumvaa kijana mmoja katikati yao na likaanza kupambana nao kujaribu kuniokoa mimi. Ndugu hawakuhangaika naye, bali walimchukua yeye pamoja na wengine waliokuwa wakiogopa, na kwenda kuwafungia kwenye chumba kingine cha Kanisa. Mapambano yaliendelea hadi saa 1:00 asubuhi. Nilikuwa nimechoka sana kimwili na nikawa kimya. Kwa hiyo, ndugu walinizunguka na kuanza kupiga kelele, “Wataje! Ni akina nani hao?” n.k. Lakini nilibaki kimya tu.

Baada ya kungoja kwa muda mrefu na nikawa nimekaa tu kimya, walidanganyika kuwa nimefunguliwa. Waliomba na tukatawanyika. Nilikuwa dhaifu sana kimwili kiasi kwamba ilikuwa tabu kutembea ili kutoka nje ya Kanisa.  Lakini kuna jambo lilitokea; maana mara tu nilipotoka nje ya Kanisa na kuvuka barabara, niliingiwa na nguvu nyingi sana kimwili. Huenda baadhi ya mapepo yaliyokuwa yametoka yalirudi. Nilijawa na hasira sana na kuamua kulipiza kisasi kwenye Kanisa lile. “Watu hawa walikuwa wamenitukana,” nilijisemea mwenyewe. Kwa hiyo, kutokana na haya, niliamua kuwa nitakwenda Lagos kupata nguvu zaidi na wengine walio waovu kama mimi, kisha tutakuja tena Port Harcourt kulipa kisasi kwa waumini WOTE wa Assembly of God, Silver Valley.

Njiani kwenda Lagos
Nilipofika kwenye nyumba ya mke wa mjomba wangu, niliwaambia kuwa naondoka mara moja kwenda Lagos. Nilikataa kushawishiwa kubakia na nikachukua taksi hadi kituo cha magari cha Mile 3 ambako nilipanda taksi hadi Onitsha. Lengo langu lilikuwa kushukia Onitsha na kwenda kumwona rafiki yangu mmoja kisha niendelee hadi Lagos. Pale Mile 3 tuliondoka na tulipofika Omagwe, kwenye njiapanda ya uwanja wa ndege wa kimataifa, nilisikia sauti ikiniita kwa jina langu la nyumbani, “NKEM.” Niligeuka kuona kama kulikuwa na mtu niliyemfahamu kwenye taksi ile, lakini hakukuwa na yeyote. Sasa, huyo aliyeniita alikuwa ni nani? Ni marehemu mama yangu tu ndiye alikuwa akiniita kwa jina hilo. Wengine wote, ikiwa ni pamoja na mapepo kwenye ulimwengu wa roho, walinifahamu kwa jina la Emmanuel.

Wakati nikiendelea kushangaa, sauti ile iliita tena: “NKEM, utaenda kunisaliti tena?” Sikuitambua sauti ile lakini iliendelea kuniuliza: “Utaenda kunisaliti tena?” Ghafla nilipata homa kali sana. Joto lililotoka kwenye mwili wangu lilikuwa kali sana kiasi kwamba abiria wengine nao walilihisi. Mmoja wao aliniuliza,  “Mr., ulikuwa mzima kabisa kabla hujaanza safari?” Niliwaambia kuwa nilikuwa mzima kabisa na kwamba sikuwa hata na maumivu ya kichwa kabla ya kuondoka Port Harcourt.

Tulipofika Umuakpa kule Owerri, nilizimia ndani ya taksi. Nilichojua baada ya hapo ni kuwa, wanaume wawili, warefu na wakubwa sana, walikuja kunichukua – mmoja kushoto kwangu na mwingine kulia; na wala hawakunisemesha hata neno moja. Walinipitisha kwenye barabara mbaya sana iliyokuwa imejaa chupa na vyuma ambavyo vilinikata na nikaanza kulia lakini hawa wanaume bado hawakusema hata neno moja. Tuliendelea hadi tukafika kwenye barabara nzuri kubwa. Ni hapa ndipo mmoja wao alipoongea na kusema, “Wewe ni mtu unayetakiwa!” na tukaendelea na safari. Tulifika kwenye jengo kubwa na refu sana ambalo lilionekana kama ukumbi wa mikutano. Mara tulipopanda hapo, sauti ilisikika kutokea ndani ikisema, “Mleteni ndani!” Waliniingiza ndani na wakapotea; nikabakia peke yangu.

Kile nilichokiona ndani ya jengo hilo, ni vigumu sana kuelezea, lakini nitajaribu kadiri niwezavyo. Ukumbi ule ulikuwa umepambwa vizuri sana na ulikuwa mkubwa na mrefu sana kiasi kwamba hungeweza kuona mwisho wake. Mwishoni kulikuwa na madhabahu. Niliona mwezi na nyota zimezunguka jua. Kisha niliona kiti cha enzi na juu yake alikaa Mwanamume mzuri sana mwenye mavazi ambayo yaling’aa kama jua. Alisema, “Njoo!” Lakini kutokana na mng’ao wake, sikuweza kwenda. Kila nilipojaribu kusogeza mguu, nilianguka.

Niliinuka na kujaribu tena na kuanguka. Mara mwezi ulitoka kwenye kile kiti cha enzi na kuja pale nilikokuwa nimekaa na ukaenda kwenye dari juu yangu. Halafu mikono miwili ilitoka kwenye ule mwezi, ikashika kichwa changu, ikanitikisa na mwili wangu wa nyama ukavuka kama kuvua nguo. Halafu mimi halisi nikasimama. Ile mikono ikaukunja ule mwili kama kukunja nguo na kuudondosha kwenye kona. Halafu huo mwezi ukarudi kwenye kile kiti cha enzi na Yule aliyekaa juu yake akaniambia tena, “Njoo!” 

Utakaso wa kiroho
Nilitembea hadi hatua fulani kisha Yeye akashuka kutoka kwenye kiti cha enzi na kuja kwangu; akachomoa miguu yangu, mmoja baada ya mwingine na kumwaga kilichokuwa ndani yake na kuirudishia tena. Alifanya hivyohivyo kwa mikono yangu na kuirudishia mahali pake. Kimsingi aliendelea hivyo kwa kila sehemu ambayo yule malkia wa pwani aliweka nguvu zake.  Nilijiuliza kwa mshangao, “Huyu ni nani na amejuaje mahali ambako vitu hivi viliwekwa?” Baada ya hapo, alirudi kwenye kiti chake cha enzi na kuniita nimwendee. Nilipoanza kutembea, vitu vilianza kudondoka kutoka kwenye mwili wangu – magamba yalidondoka toka machoni mwangu, n.k.’  Lakini kabla sijafika kwenye madhabahu, viliacha kutoka. “UNAENDA WAPI?” Aliniuliza.

Nikajibu na kusema, “Naenda Onitsha kumtembelea rafiki yangu.” Akasema, “Ndiyo, lakini nitakuonyesha kile kilichomo kwenye mawazo yako.” Hadi wakati huu sikuwa nimejua alikuwa ni nani huyo. Lakini jambo moja lilikuwa la hakika; kwamba alikuwa na nguvu zaidi ya nguvu zote nilizowahi kukutana nazo! Aliita kwa mkono mwanamume mmoja kisha akamwambia anionyeshe kile ambacho nilikuwa nimekipanga kwenye moyo wangu. Mwanamume huyo alinipeleka kwenye chumba na kufungua kitu kama ubao wa kuandikia. Kimsingi, kama kungekuwa na njia ya kuponyoka pale, ningetoroka; maana mbele yangu yaliandikwa yote ambayo nilikuwa nimepanga dhidi ya Wakristo na mipango yangu dhidi ya Kanisa la Assemblies of God, Silver Valley. Hatimaye yule mwanamume alinirejesha tena kwenye madhabahu na kuondoka.

Yule mtu alishuka kwenye kiti cha enzi na kunishika mkono na kusema alikuwa anaenda kunionyesha mambo kadhaa. Tukiwa tunaenda, alisema, “Sitaki uangamie bali nataka nikuokoe na hii ni nafasi yako ya mwisho. Kama hutatubu na kuja kwangu na kunitumikia, utakufa. Nitakuonyesha mahali pa waliookolewa na mahali pa wasio na utii.” Aliposema haya, ndipo nikajua kuwa alikuwa ni Yesu Kristo.

Mafunuo ya Kiungu
Tuliingia kwenye chumba na akafungua kitu kama pazia. Nikauona ulimwengu wote, watu na mambo yote yanayoendelea. Niliona Wakristo na wasioamini, wakifanya hili na lile. Tulienda kwenye chumba kingine. Alifungua kitu kama pazia tena na kile nilichoona kilikuwa cha kusikitisha sana. Watu walikuwa wamefungwa minyororo! Aliwaita watu hawa kuwa ni “wanafiki.” Hawa walionekana wenye majonzi sana na akasema, “Watabakia hivihivi hadi siku ya hukumu.”

Tukaenda kwenye chumba cha tatu. Akafungua pazia na nikaona watu wengi wakifurahia, wakiwa wamevaa mavazi meupe. Safari hii nilimwuliza, “Hawa ni akina nani?” Akasema, “Hawa ni wale waliokombolewa, wanangoja malipo yao.”

Tulienda kwenye chumba cha nne na nilichokiona hapo ni cha kuogofya sana. Mpendwa msomaji, ni vigumu sana kuelezea. Ilionekana kama jiji zima linawaka moto. Kuzimu ni halisi na inatisha sana. Kama ulishaaminishwa kuwa Mbingu na Jehanamu ziko hapahapa duniani na kwamba mwanadamu akifa ndio basi, ni bora utambue sasa kwamba  kuna kuzimu halisi na kuna mbingu halisi! Si ajabu basi Yesu Kristo alipokuwa duniani aliwaonya watu juu ya kuzimu. Nasema tena, kuzimu ni halisi! Niliiona na ni mahali pa kutisha sana! Nikamwuliza, “Hii ni nini?” Akanijibu, “Hapa paliandaliwa kwa ajili ya shetani na malaika zake na kwa wasio na utii.” Aliwataja kama ilivyoandikwa kwenye Ufunuo 21:8. “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili.”

Tuliingia kwenye chumba cha tano na alipofungua pazia, nilichoona kinaweza tu kuelezwa kwamba ni UTUKUFU. Ilikuwa kana kwamba ninapaangalia pale kutokea juu ya mlima. Niliona jiji jipya. Jiji hilo lilikuwa kubwa na zuri sana! Barabara zake ni za dhahabu. Majengo yake hayawezi kulinganishwa na kitu chochote kwenye dunia hii. Akasema, “Hili ni tumaini la watakatifu. Je, utakuwa pale?” Mara moja nilijibu, “Ndiyo!” Baada ya hapo tulirudi kwenye kiti cha enzi na akasema, “Nenda ukashuhudie kile nilichokutendea.”

Akanichukua tena hadi kwenye chumba kingine na alipofunua pazia, niliona yote ambayo ningeenda kukutana nayo katika safari yangu ya kwenda Onitsha na Lagos na jinsi ambavyo mwisho wake ataniokoa na yote hayo. Baada ya hapo akasema, “Usiogope, nenda, nitakuwa na wewe.” Alinisindikiza hadi nje ya ukumbi ule na akatoweka.

Ndipo niliamka nikiwa kwenye kitanda kwenye nyumba ya mtu. Nilipaza sauti, hivyo huyo mtu na mke wake walikimbia kuja toka kwenye chumba chao. Kwanza walichungulia kisha wakaingia. “Mbona niko hapa?” niliuliza. Ndipo yule mwanamume alipoelezea jinsi ambavyo nilizimia ndani ya taksi na jinsi ambavyo walinibeba hadi kwenye Kanisa Katoliki pale Owerri; jinsi walivyomwita daktari, ambaye alikuja akanipima na kusema mapigo yangu ya moyo yalikuwa kawaida na kwamba wangoje waone kile ambacho kingetokea. Daktari aliwahakikishia kuwa fahamu zangu zingenirudia. Ndipo huyo mwanamume alinibeba kwenye gari lake hadi kwenye nyumba yake na alikuwa akingoja. Akakiri kuwa hakujua kwa nini alimwamini daktari na kwa nini alichukua jukumu la kunileta kwenye nyumba yake.

Waliniuliza jina langu na wapi nilikotokea , nikawaeleza, kisha nikakaa kimya, sikuwaleza yale yaliyonikuta. Nilibaki kimya na familia hii yenye ukarimu kwa siku mbili, kisha yule mwanamume na mke wake walinichukua kwenye gari lao hadi kwenye kituo cha magari cha Owerri, ambako nilipanda taksi hadi Onitsha. Yote ambayo Bwana alinionyesha kuhusiana na safari yangu yalitokea moja baada ya jingine. Asubuhi iliyofuata, nilichukua taksi nyingine hadi Lagos. Nilitii na kuondoka Lagos kwenye Port Harcourt asubuhi iliyofuata. Kila mara huwa najiuliza, “Kwa nini Bwana amwokoe mtu kama mimi? Mtu ambaye ni mwovu na mharibifu; ajenti wa shetani! Nilipata majibu kwenye maneno haya matatu: Mungu ni pendo. Hakika, Mungu ni Pendo! (1 Yohana 4:8, 4:16).

ITAENDELEA…..

No comments:

Post a Comment