Sunday, April 27, 2014

Niliokolewa Toka Kwenye Nguvu za Giza - Sehemu ya 5



Kufanywa kuwa ajenti wa shetani

Sikuwa na hisia za kibinadamu wala huruma ndani ya moyo wangu tena. Niliingia kazini mara moja na kuharibu nyumba tano kwa wakati mmoja. Nyumba hizo zilizama ardhini pamoja na wakazi wake wote. Tukio hili lilitokea Lagos  Agosti 1982. Kontrakta aliyejenga nyumba hizo alishikiliwa kwa kosa la kutoweka msingi imara na alilipa faini kubwa sana. Uharibifu mwingi unaotokea duniani hivi leo hausababishwi na wanadamu. Kazi ya ibilisi ni kuiba, kuchinja na kuharibu. Nasema tena,  shetani hana zawadi za bure!”


Niliingia kwenye kusababisha ajali barabarani, n.k. Moja ambalo ningependa kulitaja lilikuwa linamhusu kijana mmoja ambaye ndio kwanza alitoka kuokoka na akawa anashuhudia kuhusu wokovu na ukombozi wake. Alikuwa anasababisha uharibifu mkubwa sana kwenye ulimwengu wa roho wa giza kwa kufanya hivyo. Kwa hiyo, nilipanga ajali kwa ajili yake. Siku moja alikuwa akisafiri kwa basi kuelekea Lagos. Kule nako alikuwa anaenda kutoa ushuhuda wake mahali fulani. Wakati basi likiwa kwenye mwendo mkali, nililitoa nje ya barabara na likaenda kujigonga kwenye mti. Abiria wote walikufa isipokuwa huyu mwokovu mpya!  


Kupona kwake kulikuwa kwa miujiza maana alitoka nje ya basi kupitia kwenye buti na akapaza sauti, “Nimepona! Nimepona!” Tulijaribu kila njia kumfanya aache kushuhudia lakini tulishindwa.


Kupitia kwenye TV, tuliweza kumjua mtu ambaye ameokoka hivi karibuni na tungemfuatilia kwa nguvu ili kuona kama tunaweza kumfanya arudi nyuma. Iwapo baada ya miezi sita hatujafanikiwa, tunaenda kwenye biashara yake na kuifanya ifilisike. Kama ni mfanyakazi wa umma, tunamnyanyasa kupitia kwa bosi wake; na ikiwezekana, tunasababisha bosi wake amfukuze kazi. Iwapo baada ya yote haya bado anashikilia wokovu wake, ndipo tunakata tamaa. Lakini kama ikitokea akarudi nyuma, anauawa palepale ili kuhakikisha kuwa hapati nafasi ya pili ya kutubu.


Niliharibu maisha ya watu kwa kiwango kikubwa kiasi kwamba Lusifa alifurahi sana na kunifanya kuwa  mwenyekiti wa wachawi. Mwezi mmoja baada ya kupewa uenyekiti huo, mkutano uliitishwa. Tulihudhuria mkutano huo tukiwa ndege, paka, nyoka, n.k. Viumbe hawa ni wa muhimu sana kwa sababu zifuatazo:  

  • Kujigeuza ndege humfanya mchawi awe hatari zaidi.
  • Kujigeuza paka kunamfanya mchawi aweze kuwafikia mapepo na pia kuwafikia wanadamu.
  • Kujigeuza panya kunamwezesha mchawi kuingia kwenye nyumba za watu kirahisi, na usiku anageuka kuwa kivuli, na kisha mwanadamu na kunyonya damu ya mtu aliyelengwa.

Kwenye mkutano huu tulikuwa na ajenda moja tu: “Wakristo.” Kisha tulipanga kuwa na mkutano mkuu wa wachawi wa Afrika kwenye jiji la Benin mwaka 1983. Tulitangaza mkutano huo kwenye magazeti mbalimbali na kwenye vyombo vingine vya habari. Nguvu zote kubwakubwa za giza zilikusanywa na tulikuwa na uhakika kwamba hakuna kitakachoharibu mkutano wetu. Kimsingi, kila kitu kilipangwa vizuri sana na hakukuwa na mwanya wa kutokea kosa.


Lakini ghafla, Wakristo wa Naijeria waliingia kwenye maombi na sifa kwa Mungu wao. Mipango yetu yote ilisambaratika! Si tu hivyo, lakini pia walisababisha vurugu kubwa sana kwenye ulimwengu wa giza. Matokeo yake, mkutano ule wa  wachawi haukuweza kufanyika Naijeria.  Wakristo ni lazima watambue kuwa mara waingiapo kwenye sifa za kweli kwa Mungu Mwenyezi, kunakuwa na matatizo na kuchanganyikiwa baharini na angani; na maajenti wa shetani wanakosa mahali pa kupumzikia. Maombi ni kama kutupa mabomu na kila mtu anakimbia ili kuponya maisha yake.
Kama Wakristo wangetambua na kutumia nguvu na mamlaka ya Mungu waliyopewa, wangetawala masuala ya mataifa yao! Ni Wakristo tu ndio wana uwezo wa kuokoa taifa.


Baada ya mkutano ule kushindikana, ambapo baadaye ulifanyikia Afrika Kusini, niliitwa tena baharini. Nilipofika kule, niliambiwa kuwa baharini ndiko kutakuwa nyumbani kwangu kwa kudumu, na duniani nitakuwa nakwenda tu kama kuna jambo gumu la kufanya. Nilikabidhiwa majukumu mapya – kubuni hirizi na dawa kwa ajili ya waganga wa kienyeji, kuwa msimamizi wa chumba cha kuongozea (control room) na kutuma zawadi, kufungua makanisa ya majoho meupe - white garment churches (nyumba za maombi), kufungua zahanati za uzazi (maternities), kufungua maduka na kuyafanya yakue, kutoa ‘watoto’ na fedha. Nitayaelezea mambo haya moja baada ya jingine:

  • Kufungua makanisa ya majoho meupe - white garment churches
Mtu anapokuja kwetu kutaka msaada wa kujenga nyumba ya maombi na kupata nguvu za kufanya miujiza, n.k.’ atapewa masharti kadhaa:

  • atakubali kutupatia roho moja au mbili kila mwaka.
  • akifikia ngazi fulani kwenye kanisa, ataingizwa kwenye kundi letu.
  • hakuna mshirika atakayeruhusiwa kuingia kwenye nyumba ya maombi akiwa amevaa viatu. 


Anapokubaliana na masharti haya, anapewa kitu kama “white gravel”, mifupa wa binadamu, damu na hirizi, vyote vikiwa kwenye mtungi wa kienyeji. Kisha ataelekezwa akaufukie mtungi huo na vitu vilivyomo mbele ya kanisa na kuchimbia msalaba juu yake. Baada ya kufanya hivyo, ni msalaba tu ndio utakaokuwa unaonekana. Atashauriwa ajenge kidimbwi au beseni ambamo mapepo yataendelea kuweka maji maalum. Haya ndiyo maji ambayo utawasikia wachungaji hao wakiyaita "maji matakatifu."


Watu wengi wanaposumbuliwa na mapepo wanaenda kwa hawa “manabii” ili yakatolewe. Ukweli ni kwamba, wanaenda kuongezewa tu mapepo zaidi. Shetani hawezi kumtoa shetani mwenzake. (Luka 11:17-19). Atakachofanya huyu nabii ni kumwombea huyo mshirika, kisha anampa kitambaa chekundu akaweke nyumbani kwake. Halafu atamshauri awe anaomba huku amewasha mshumaa na ubani. Kwa kufanya hivi, mtu huyo anakuwa anatukaribisha sisi kwenye nyumba yake. Wakati mwingine mshirika anaweza kuambiwa alete mbuzi, n.k. kwa ajili ya kafara. Kafara hizi ni kwa jili yetu ili tuweze kuja kusaidia kumponya. Nabii anakuwa hana nguvu ya kutibu au kuponya.  

  • Kufungua zahanati za uzazi

Kama mwanamke akija kwetu kutaka msaada wa kufungua zahanati ya uzazi na kuifanya ikue, atapewa masharti:



Mwezi mmoja utateuliwa na sisi ambapo watoto wote watakaozaliwa katika mwezi huo kwenye zahanati hiyo, watakufa. Lakini wale wanaozaliwa kwenye miezi mingine, wanaishi.


Kama akikubali, naye pia atapewa hirizi inayowavuta watu kuja kwenye zahanati yake. Zahanati za namna hii zipo Onitsha, Lagos, n.k. Viatu haviruhusiwi ndani ya zahanati hizo.

  • Kufungua maduka
Mtu anapokuja kutaka msaada wa kufungua duka kubwa, anapewa pete ambayo ina sharti kwamba, mwanamke yeyote asiiguse. Pia ni lazima akubali kuwa mwanchama wetu. Akikubali masharti haya, kila wakati duka lake litajazwa na sisi vitu vizuri na vya kisasa.

  • Kutoa watoto
Kama mwanamke tasa akienda kwa mganga wa kienyeji, ataambiwa akalete vitu vifuatavyo: jogoo mweupe, mbuzi, chokaa ya kienyeji (native chalk) na “baby care”. Halafu ataambiwa aondoke, na arudi siku nyingine. Kisha huyo mganga atakuja kwetu na vitu hivyo. Sisi tutachanganya vitu fulani ambavyo si rahisi kuvielezea kwa kuandika, kukiwamo majivu ya mwanadamu. Atatumia dawa hii kupika chakula kwa ajili ya mwanamke huyo. Hatimaye atapata mimba na kuzaa; lakini kitakachozaliwa si binadamu wa kawaida. Kama mtoto huyo atakuwa mwanamke, ataishi, atakua na hata kuolewa lakini atabakia tasa maisha yake yote. Kama ni mwanamume, ataishi na hata kusoma, lakini atakufa ghafla. Hawa huwa hawaishi kufikia kuja kuwazika wazazi wao.  


Ningependa kusema kuwa utasa mara nyingi husababishwa na mapepo hapa duniani, lakini mtu wa namna hiyo atakuwa na watoto baharini. Kwa hiyo, ningependa kuwausia wana wa Mungu kuwa ni vema kumsubiri Mungu maana Yeye hutoa watoto halisi.

  • Kutoa fedha
Kama mtu akija kwetu kutaka fedha, atapewa masharti yafuatayo: ataambiwa atoe kiungo cha mwili wake au kama ana familia, ataambiwa amtoe mwanawe wa kiume. Vinginevyo, ataambiwa amtoe mkubwa wake au mdogo wake.


Chochote atakachoamua kutoa ni lazima kitoke kwenye tumbo lililomzaa na yeye. Jambo muhimu la kukumbuka ni kuwa, wakati wa kumuua huyo aliyetolewa, mtu aliyemtoa atapewa mkuki au mshale. Ndugu zake watafanywa wapite kwenye kioo. Mara atakapomwona yule aliyemchagua, ataambiwa amchome na anapofanya hivi, nduguye huyo atakufa papohapo kokote kule aliko.


Ziko njia nyingine mbalimbali lakini katika zote hizo, kitu kimoja anachofanya shetani ni kwamba, anahakikisha kuwa kwenye hizo njia mbalimbali, mtoaji  kafara ndiye anayehusika na kifo cha aliyetolewa kafara kwa kumfanya ampige au amchome mtu huyo.


Kumbuka, shetani hana zawadi za bure!!

11 comments:

  1. asante sana na mungu akubariki. mbona sehemu ya pili na ya tatu hazipo? kuna ya 1,4 na 5 tu .kama ni ukijaliwa plz ziweke pia

    ReplyDelete
    Replies
    1. Shalom, shalom.

      Sehemu zote zipo angalia tu vizuri utaziona.

      Bwana akubariki.

      Delete
    2. Shalom hongera sana kwa shuhuda kemkem unazotupa. Mungu akubarikisana. Tupe basi mwendelezo Wa 6 na 7

      Delete
    3. Shalom mpendwa.

      Nimekuwa kwenye ratiba ngumu sana kwa kipindi sasa ndio maana sijaweza kuendeleza sehemu zinazofuata, lakini Bwana ni mwema, sehemu hizo naziweka ndani ya siku tatu hivi.

      Ubarikiwe nawe pia.

      Delete
    4. SHUHUDA HIZI ZINAJENGA SANA UFALME WA MUNGU.HASA SISI WAHUBIRIRI TUNAPATA UJASIRI SANA KWA KUJUWA SIRI ZA ADUI YETU MKUU SHETANI.UBARIKIWE SANA TUNASUBIRI MUENDELEZO WA SHUHUDA HII KUOKOLEWA NGUVU ZA SHETANI.

      Delete
  2. MUNGU AKUBARIKI SANA MTUMISHI KWA KUWEKA SHUHUDA HIZI ZINATUYSAIDIA SAANA KUSIMAMA NA KUTAMBUA YA KUWA MUDA WETU U MFUPI SAANA...ENDELEA KUTULETEA SHUHUDA ZINGINE..

    ReplyDelete
    Replies
    1. shalom, shalom. asante sana kwa maoni yako na Mungu azidi kukubariki na kukuinua. Namshukuru Bwana sana kama kazi hii inaleta mchango kwenye mwili wa Kristo.

      Delete
  3. umekuwa kimya sana mtumishi kwa sehemu ya 6 na ya 7 ya ushuhuda huu.nimeifuatilia kwa wiki 3 sasa bila mafanikio.tafadhali mtumishi ninaomba utuwekee sehemu hizo.shuhuda hizi zinatujenga sana na kuinua imani zetu.na MUNGU muweza wa yote akubariki sana.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Shalom, najitahidi kufanya hivyo ndugu yangu. Mungu wetu ni mwaminifu, atafanya uwezekano upatikane tu. Bwana akubariki.

      Delete
  4. ni ushuhuda mzuri hongera na pole

    ReplyDelete
  5. Kaka mbona kimya sana siku hizi,tume miss shuuda na mafundisho yako tafadhari tukumbuke tafadhari!!!

    ReplyDelete