Saturday, November 23, 2013

Wakristo walio kwenye giza la nje




Dada Liyan ni mwenyeji wa China. Bwana alisema naye kwa njia ya maono na hata kumpeleka mbinguni na kuzimu. Anayo mafunuo mengi ya muhimu sana ambayo tunayahitaji mno, hasa katika nyakati hizi za mwisho. Tafadhali fuatana naye katika ushuhuda huu muhimu na Bwana atasema na moyo wako kwa namna ya ajabu sana.

……………………..

Hivi karibuni nimekuwa nikipata maono mengi kutoka kwa Mungu.
Hebu nianze kukushirikisha yale ambayo nimeyaona kwenye miaka michache iliyopita.

Tangu 1996, nimekuwa nikimjua Bwana, na nimekuwa nikiona ukweli wake. Mimi nimekulia kwenye familia ya Kikristo, huku nikimwamini Yesu Kristo, lakini kusema kweli sikuwa nikimjua kiukweli. Kuwa na imani katika Yesu ni tofauti na kumjua Yesu. Katika 1 Samweli 3:7, licha ya kukulia kwenye Hekalu, Samweli hakumjua Bwana. Kama ilivyokuwa kwa Samweli, mimi nami sikumjua Bwana hadi mwaka 1996 nilipokuwa na umri wa miaka 16. 

Tangu nilipokuwa mtoto, nilikuwa nina matatizo ya kiafya, tofauti na mama na dada yangu. Mama yangu ni mtu mwenye bidii sana nyumbani na hata kazini. Mara nyingi alinikasirikia kutokana na kuumwa kwangu kila wakati, na hakujua ni kwa nini nilikuwa hivyo, ilhali dada yangu alikuwa ni mtu mwenye afya tu. Nyumbani sikuweza kusaidia kazi yoyote, hata kupika, maana nilikuwa nikianguka na kupoteza fahamu mara kwa mara. Madaktari hawakuweza kugundua ugonjwa wangu hadi nilipofanyiwa kipimo cha CT scan, ambacho kilionyesha kuwa nilikuwa na magonjwa sugu ya gastritis, sinusitis, na periostitis. Lakini hata baada ya ugunduzi huo, madaktari hawakuweza kunitibu. Magonjwa haya yalinizuia kuwa wa msaada pale nyumbani. Kwa hiyo, hata mama yangu aliniona sifai, jambo ambalo liliyafanya maisha yangu kuwa machungu hata zaidi.

Nilipofikisha miaka 16, nilikuwa bado ziwezi kusaidia kazi za nyumbani. Kwa hiyo, mara kwa mara mama yangu alinitishia kwa kusema,  "Kama utakufa, basi ni bora ufe tu mapema utupunguzie matatizo. Hebu jiangalie. Huna maana yoyote kwenye dunia hii. Huna uwezo wa kuyaondoa maisha yako wala kuishi maisha mazuri. Tukufanyie nini sasa?”  Hata mimi mwenyewe nako sikuwa na jibu. Kuanzia hapo, nilianza kumwomba Mungu: "Ee Mungu, kama kweli wewe upo, tafadhali nisaidie kuondoa uhai wangu hapa duniani.” Mara nyingi niliwaza juu ya kujiua – kwa mfano kwa kujinyonga, kunywa sumu na kuruka kutoka kwenye ghorofa – lakini kila mara wazo la kujiua lilinitia hofu. Nilikuwa nikiwaza,  Vipi kama nitajaribu halafu nisife?” Nilijua kuwa, kama hilo litatokea, basi hali yangu itakuwa mbaya zaidi. Kwa hiyo, sikujaribu kujiua. Baadaye nilikumbuka jinsi Biblia inavyosema, “Kama mtu akiliharibu hekalu la Mungu, Mungu atamharibu mtu huyo. Kwa maana hekalu la Mungu ni takatifu, ambalo ni ninyi.” [1 Kor. 3:17]; kitu kinachomaanisha kwamba mtu akijiua hawezi kuokoka.

Tarehe 1 Juni, sikufanya maombi yoyote maalum, lakini nilisema tu, "Mungu, kama wewe kweli upo, tafadhali niondolee uhai wangu Bwana; tafadhali pokea roho yangu." Mama yangu alipoondoka saa 9:30 mchana kwenda kazini, nilipiga magoti pembeni mwa kitanda changu na kuendelea kuomba. Ghafla, roho yangu ilitoka kwenye mwili na nikawa nauona mwili wangu ukiwa unaendelea kuomba lakini ukaanguka. Roho yangu ikaendelea kuwapo pale. Wakati huo, sikuwa ninaogopa. Badala yake, nilijisikia tu vizuri kwa kuwa sasa sikuwa nahisi tena maumivu yoyote au kuumwa na kichwa. Hapo nilielewa pale Biblia inaposema kuwa roho ndiyo itiayo uzima na mwili haufai kitu (Yohana 6:63). Sikujisikia kuwa nauhitaji tena mwili wangu badala yake nikawa najisikia vizuri sana.  

Roho yangu ilipotoka kwenye mwili, nilijua hakika kuwa naenda
mbinguni; maana nilidhani kuwa wale wanaomwamini Yesu wana uhakika wa kwenda mbinguni baada ya kufa. Pia niliamini kuwa njia ya kwenda mbinguni inaelekea juu huku ile ya kwenda kuzimu ikieleka chini. Roho yangu ilipaa na kutoka nje kupitia dirishani na ikaendelea kupaa kwenda juu mbinguni. Ah! Kulikuwa kuzuri mno! Nilikuwa naelekea mbinguni! Sikujisikia kuwakumbuka familia yangu hata kidogo.

Giza la Nje
Kisha roho yangu ilienda kwenye sehemu yenye giza. Giza la pale ni tofauti na giza la hapa duniani. Giza hilo litaishtua roho yako kiasi kwamba hutaweza hata kuiona mikono yako hata kama ukiiweka karibu kabisa na macho yako! Nilikuwa na uhakika kabisa kwamba hapa hakukuwa mbinguni, japokuwa sikuwa nimewahi kwenda huko. Nilijua kuwa mbinguni hakutakiwi kuwa na giza; kunatakiwa kuwe kumejaa nuru. Niliwaza, “Hapana! Ina maana hapa ni kuzimu?” Sikuweza kujua pale ni mahali gani maana nilipokuwa mdogo nilisikia kuwa kuzimu kuna moto; lakini hapa hakukuwa na moto, ni giza tu. Nikasema, "Ni mahali gani humu?" Nikawasikia watu wengi wakilia [Mt 25:30], lakini sikuweza kutambua walikuwa wako wapi. Ghafla, nilisikia sauti iliyosema kwa kurudiarudia, "Endelea mbele, endelea mbele.

Nilitembea kwenye giza lile na kadiri nilivyoendelea kutembea, vilio vya watu vikasikika kwa karibu zaidi kiasi kwamba ingetakiwa niweze kuona nyuso zao; lakini bado nilikuwa siwezi kuona chochote! Mara niliweza kutambua sauti ya minyororo ya chuma, na nikasikia kufuli likifunguliwa. Ghafla mlango ulifunguka na kulikuwa na chumba mbele yangu  ambacho kilikuwa kina mwanga kwa mbali. Niliona watu wengi, na ninapotafakari, naona walikuwa ni Wakristo. Wazo lililonijia kwanza lilikuwa kwamba Ukristo ulikuwa ni uongo; maana Wakristo wale hawakwenda kamwe mbinguni. Walikuwa wako gizani; na sehemu hii ilikuwa imejaa Wakristo. Kwa nini wote walikuwa hapa? Baadhi walikuwa ni Wakristo wanawake kutoka kijijini kwangu ambao walishakufa na niliwafahamu fika; lakini kumbe wamekuja kuishia humu!  

Kisha sauti iliniambia: "Ingia ndani." Nikajibu, "Hapana kabisa! Sitaingia kamwe kwenye sehemu hii." Nilijua kuwa mara nitakapoingia, nitajiunga na kundi lile la wafu waliokuwa wanaangua vilio. Watu humo walikuwa wakilia mfululizo na mavazi yao yalikuwa ya rangi ya udongo na machakavu. Mara kulitokea nguvu fulani iliyonisukumia ndani, lakini mkono wangu ulibakia umeng’ang’ania mlango, na niligoma kuingia kwenye chumba kile. Kwa hiyo, nilipiga magoti na kulia kwa sauti, “Bwana, sitataka kujiua tena; tafadhali nirudishie uhai na uniruhusu kuishi tena. Kama sehemu yenyewe ninayokuja kuishi ni hii, basi bora nibakie duniani hata kama nitakuwa mgonjwa kwa miaka kadhaa. Kwa nini nije hapa? Hapana!” Wakati huo nilikuwa nikijiuliza swali ndani yangu, maana niliwaza kuwa hakuna kitu kama mbinguni na kuzimu; yote yalikuwa ni uongo. Wale wote walkoonekana kumwamini Yesu kule duniani, wote waliishia hapa. Kila mara niliwaza – hakuna mbingu wala kuzimu. 

Niliuliza, "Hapa ni mahali gani?" Ghafla sauti ilinijibu: "Hapa ni mahali
pa kilio na kusaga meno.” Nilimsikia mtu akiongea lakini sikuweza kumwona. Niliendelea kuuliza, "Nini? Hapa ni mahali pa kilio na kusaga meno? Mbona basi watu wote hawa ni Wakristo?" Akasema, "Watu hawa walimwamini Yesu bila kuwa na toba." Nikajibu, "Vipi sasa kuhusu wasioamini?" Akasema, “Wasioamini wanaenda moja kwa moja kuzimu." Kisha ghafla nilijikuta ninaelekea kuzimu.

Kuzimu
Sehemu ya kutisha waliko wasioamini haiwezi kulinganishwa na pale waliko wale waliomwamini Yesu bila ya toba. Niliwasikia watu kule kuzimu wakilia sana kwa maumivu makali. Kila mmoja pale alisema: "Ni joto sana! Nina kiu sana!" Niliona moto ukiwaka ndani ya miili yao. Na kila moto ulipounguza mwili, mtu alipiga kelele sana. Cha ajabu, minyoo ambayo haiathiriwi na moto, iliendelea kutoboa na kuingia na kutoka ndani ya mifupa yao. Kila ilipofanya hivyo, ilimsababishia mtu maumivu makali sana. 

Mateso ya roho ya mtu ni mabaya sana kuliko mateso ya mwili. Nilipotambua hili, nikajiambia, “Ni afadhali kumwamini Yesu bila toba kuliko kutomwamini na kwenda moja kwa moja kuzimu,” ukitilia maanani mahali pa kilio na kusaga meno, ambako kuna unafuu kuliko kuzimu.
Mbinguni
Niliwaza, hivi mbingu kweli ipo? Mara swali hili lilipoingia mawazoni mwangu, nilijihisi roho yangu ikielekea Mbinguni. Ha! Kulikuwa kuzuri! Uzuri wa mbinguni hauelezeki. Niliona maji yakitiririka, majani, milima, na maua. Mitaa ilikuwa mizuri mno kuliko mitaa yoyote iliyojengwa na wanadamu duniani. Milima ilitengenezwa kwa vito vya thamani; maji yalionekana kama vito vya lulu na shohamu (onyx); mitaa ilisakafiwa kwa dhahabu safi, na kuta zilijengwa kwa yaspi, rubi, yakuti samawi (sapphire), na zumaridi (emerald). Nilipigwa na butwaa na uzuri ule! Nikajisemea, "Siondoki hapa! Nataka kukaa mahali kama hapa.

Ghafla alitokea malaika na akaongea na mimi akisema, "Kulingana na
kiwango cha imani yako, unastahili kuwa kwenye mahali pa kilio na kusaga meno. Hautakiwi kuingia humu.” Nikasema, "Siondoki humu." Kisha malaika akasema, "Hapana! Ni lazima uondoke." Nikajibu, "Je, natakiwa kuteseka kwa maumivu ya ugonjwa wangu duniani tena?" Akasema, "Kama hauko tayari kurudi tena duniani, basi sehemu pekee nyingine unayostahili ni kubakia kwenye mahali pa kilio na kusaga meno." Nikasema, "Kama sehemu pekee nyingine ninayostahili kwenda ni kule kwenye giza, basi bora nirudi kwenye mwili wangu ulio mgonjwa kule duniani na kuendelea kuteseka kwa ugonjwa." Nilichagua kurudi duniani.  Sekunde iliyofuata nilikuwa tayari nimesharudi nyumbani.

Roho yangu iliondoka kwenye mwili wangu kwenye saa 10:10 jioni; na ilikuwa ni saa 4:30 usiku ndipo iliporudi. Saa za mama yangu kufanya kazi zilikuwa ni kuanzia saa 10:30 jioni hadi usiku wa manane. Muda huu dada na mama yangu walikuwa tayari wameshalala. Mwili wangu ambao haukuwa na ufahamu, ulikuwa uko chini, huku umepiga magoti pembeni mwa kitanda. Inasikitisha! Hawakujali kama nimekula au la – jambo linaloonyesha kiwango kilichokuwapo cha cha kutonijali kwao. Nikawaza, “Dada yangu! Yaani dada yako mkubwa, pembeni yako, amekufa na wewe hata haujali! Ulipanda tu kitandani na kulala?" Roho yangu iliendelea kurandaranda kwenye nyumba, na bila ya ugonjwa ilikuwa inajisikia vizuri.  Nilikuwa nasitasita kweli kurudi kwenye mwili wangu mgonjwa, maana nilijua kuwa mara nitakapoingia humo, nitaanza kupata maumivu tena; lakini pia kama nikikataa kuingia kwenye mwili wangu, nitarudi kwenye sehemu ya kilio na kusaga meno. Kwa hiyo, nikajua kuwa ni bora nirudi kwenye mwili wangu kuliko kwenye yale mateso niliyoyaona.  

Roho yangu ilienda kwenye mwili wangu, kisha niliamka, lakini mwili wangu wote ulikuwa hauna hisia. Nikagundua kuwa uso wangu umejaa machozi. Baada ya kusubiri kwa takriban dakika kumi hivi, miguu yangu ilianza kujisikia ganzi kidogo. Roho yangu ilipoondoka kwenye mwili, damu ilisimama mwilini. Nilianza kujisogeza kidogo na nikaanguka kutoka kitandani; machozi yalikuwa yakinitiririka. Nilishukuru sana na kusema, "Bwana, nakushukuru. Asante, asante kwa kunirudisha tena duniani." Roho yangu iliporudi, Mungu alinipatia maneno machache. Alisema, "Mwanangu, rudi. Umebakiwa na muda kidogo. Muda mfupi ujao utakuja mahali hapa nilipopaandaa kwa ajili ya watu wangu. Ukirudi duniani, ni lazima ukawaambie kile ulichokiona.” Niliposikia maneno yake akisema, “Umebakiwa na muda kidogo,” nilidhani ingekuwa ni siku chache tu. Nilifikiri angerudi mapema sana. Nikasema,  "Oh!Hakika! Ilmradi tu kama utaniruhusu kuja mbinguni, basi nitawaeleza nilichokiona.

Wakati ule nilipopokea ujumbe, nilidhani kuwa angekuja ndani ya siku chache, nami ningekutana naye mbinguni tena. Sikutarajia kuwa ningeolewa na kuwa na watoto wangu. Niliporudi duniani, nilikuwa nimejawa na pendo la Mungu na nilianza kuhubiri Injili. Nilianza na wasioamini kwa sababu walioamini hawakutilia maanani sana ushuhuda wangu. Wa kwanza kumweleza alikuwa ni mama yangu. Wakati huo tulikuwa sote tuko nyumbani nami nilikuwa narukaruka kwa msisimko. Mama yangu aliporudi nyumbani kutoka kazini saa kumi na mbili, nilimwambia, "Mama, nilikufa na roho yangu ikatoka kwenye mwili." Akasema, "Hivi siku nzima ya leo ulikuwa kwenye hali hiihii? Hauko sawa wewe; una wazimu!" Niliwaza, kama mama yangu tu haniamini, ni nani mwingine ataniamini?  Nakumbuka nilienda kumshirikisha dada mmoja wa kanisani ushuhuda wangu. Mara moja alisema, "Liyan! Hakika kuna tatizo kwako. Hilo haliwezekani! Hata siwezi kuamini.” Kwa hiyo, niliacha kuwashirikisha waumini wenzangu ushuhuda wangu.
Nilipowashirikisha wasioamini, mmoja baada ya mwingine walikuja kwa Yesu. Nilipowasimulia watu mbalimbali kwenye treni, wengi waliyatoa maisha yao kwa Bwana. Bwana asifiwe! Nilijua kuwa hii ilikuwa ni kazi ya Mungu. Hata hivyo, sijawahi kwenda shuleni na ninajihesabu kuwa mtu asiyesoma. Nilimwambia Mungu, "Unaenda kunitumia mimi; lakini sijasoma." Wakati fulani nilisikiliza mahubiri kuhusiana na kufufuka kwa Lazaro, ambaye alikufa na kukaa kaburini siku nne hadi akawa ananuka. Lakini Yesu alipotamka neno moja tu, Lazaro alirudi kutoka kwa wafu [Yohana 11:43]. Niliguswa sana na hadithi hiyo na nikajisemea, “Kama Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne, alikuwa amezikwa na hata kunuka vibaya, lakini bado alifufuliwa, vipi kama Bwana atataka nijifunze kusoma? Bila shaka itakuwa ni jambo rahisi zaidi.” Kuanzia hapo nilipata shauku kubwa ya kujifunza jinsi ya kusoma. Matokeo yake, sala zangu zikawa ndefu zaidi. Kila usiku niliomba hadi saa saba au nane usiku. 

Nakumbuka ilikuwa saa nane usiku kwenye mwezi wa kumi na mbili, nilipokuwa nimemaliza kuomba, nililala kisha nikaanza kuota ndoto. Ghafla, nilimwona mtu amevaa nguo nyeupe ambaye alikuwa anang’aa sana. Alikuwa na mng’ao ambao sijawahi kuuona duniani. Alisimama kwenye dirisha langu na kuniita, "Mwanangu, njoo kwangu." Uso wake uliangaza kama jua, na sikuweza kuuona sawasawa. Kisha alinitoa kwenye blangeti langu na kunikumbatia kama mtoto mchanga. Akasema, "Kuanzia leo na kuendelea nitakufundisha jinsi ya kusoma." Nikajibu, "Safi sana! Nina shauku sana. Nianzie wapi?" "Tutaanzia kwenye Injili ya Yohana." Alifungua Biblia kwenye Yohana 21:15 na kuanza kusoma, "Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? Akamwambia, Naam, Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda. Akamwambia, Lisha wana-kondoo wangu.” Kadiri tulivyoendelea kusoma, jina la Petro lilikuwa limeshabadilika na kuwapo jina langu; hata hivyo, wakati huo sikutambua jina langu wakati wa kusoma na Bwana aliendelea kunifundisha jinsi ya kusoma. Alisema, “Liyan, je, wanipenda kuliko haya?” Nikasema, “Unamaanisha nini?" Kisha akasema, "Ninaongelea mambo ya dunia; je, unanipenda kuliko haya?" Nikasema, "Bwana, wewe wajua kuwa nakupenda.” Tuliendelea kusoma hadi kulipopambazuka.

Kulipokucha, niliamka na kukuta kwamba niliendelea kusoma na kujikuta bado niko kitandani. Haraka nilichukua Biblia na kufungua kwenye Yohana 21:15. Nikasema, "Ha! Hiki ni kitabu cha Yohana." Lakini nilikuwa naogopa kufanya makosa, kwa sababu wakati huo baba yangu, mdogo wangu wa kike na kaka yangu walikuwa wote wapo. Nikamwambia mdogo wangu wa kike na wa kiume, "Njoni hapa. Leo nitawasomea baadhi ya aya za Biblia.” Wakasema, "Haya, soma.”Kitabu cha Yohana, siyo?" nikauliza. Wote walinitazama na kusema, "Ndiyo, ndiyo. Umepatia kabisa." Nikasema, "Nitasoma Zaidi kidogo. "Basi walipokwisha kula, Yesu akamwambia Simoni Petro, Je! Simoni wa Yohana, wewe wanipenda kuliko hawa? " Walishikwa na mshangao na kusema, "Dada, umejifunza wapi namna ya kusoma maneno haya?" Nikajibu, "Ninachowaza zaidi mimi ni endapo nimesoma kwa usahihi." Wakasema, "Ndiyo, ndiyo, kila neno. Umesoma maneno hayo kwa usahihi kabisa!

Taratibu, nilianza kutambua kila neno kwenye Biblia. Hata hivyo, sikuweza kutambua maneno kwenye kitabu kingine kisichokuwa Biblia, hata vitabu vya kiroho vinavyoongelea Kitabu cha Yohana. Maneno yalionekana nayajua, lakini sikuyaelewa. Matokeo yake, kwa miaka kadhaa Mungu aliendelea kunifundisha jinsi ya kujifunza Biblia, ambayo ilifanyika maji yangu ya uzima ya kiroho; na nilijifunza kwa bidii sana. Kasi yangu ya kusoma ilikuwa ndogo. Wakati mwingine ilinichukua siku kadhaa kumaliza mstari mmoja; lakini nilipokea ufunuo mwingi kutoka kwa Roho Mtakatifu. Kila siku nilitafakari, niliomba na kusoma. Kwa hiyo, maisha yangu yakawa yamejawa utajiri wa kiroho. Hivyo ndivyo nilivyojenga uhusiano na Yesu Kristo. 

Kisha nilijiunga na kanisa na kufanya kazi ya Bwana kwa miaka miwili. Ulikuwa ni uzoefu wenye matunda sana na ulinisaidia mimi pamoja na ndugu wengine katika maisha yetu ya kiroho. Lakini Bwana hakuridhishwa na kazi yangu katika miaka hiyo miwili. Hivyo, karama za rohoni wala miujiza haikubainisha maisha yangu ya kiroho. Kama alivyosema Paulo,   “isiwe, nikiisha kuwahubiri wengine, mwenyewe niwe mtu wa kukataliwa.” [1 Kor 9:27]. Ilikuwa ni mwaka 2004 ndipo nilipoungana na mchungaji mmoja kuanzisha kanisa kwenye nyumba yangu. Tulidhani tumefanya kazi nzuri. 

Kwenye siku ya pili ya mwaka 2006, Mungu alianza kufunua jambo ambalo lingenitokea mimi siku iliyofuata, na jambo hilo kweli lilitokea. Siku ya tatu nilipokuwa najiandaa kulala, Bwana aliniambia, "Kesho asubuhi, kuna mtu atakuja kukuomba ukamwombee bibi yake, nawe ni lazima uende." Siku ya nne nilianza kungoja nyumbani kuanzia saa 2 hadi saa 4 asubuhi, ndipo alipotokea huyo mwanamume. Nilishangaa kumwona akiwa kama vilevile nilivyoona kwenye ndoto. Kwa hiyo nilienda naye kumwombea bibi yake. 

Siku ya tano, nilishangazwa na ufunuo mwingine wa ghafla kutoka ndotoni. Mungu alisema, "Ninarudi, na ni lazima utubu!" Nilishtuka na kujibu, "Unarudi na ni lazima nitubu? Vipi kuhusu mchungaji ambaye tuko pamoja?" Akasema, "Hakuhusu. Mimi ninarudi na ni lazima utubu!" Nikawaza, "Nitubu kuhusiana na nini? Nimekuwa najibidisha kulea kanisa hili. Sasa, kwa nini nahitaji kutubu?” Akasema, "Nifuate Mimi, ninapenda nikuonyeshe mahali."

Moyo

Kufumba na kufumbua, nilifika kwenye nyumba moja ambayo kuta
zake na sakafu vilikuwa vichafu sana. Vilikuwa vichafu kiasi kwamba ilikuwa haiwezekani kuingia ndani. Nikauliza, “Hii ni sehemu gani? Mbona ni chafu kiasi hiki?” Bwana akasema, “Unajua kwamba huu ni moyo wako?” Kwa kweli sijui. Nilidhani nilikuwa ninamtumikia Bwana na kwamba ningekuwa niko safi. Kusema kweli, nilikuwa ninapingana na Bwana. Nikauliza, "Ni lini nilitenda dhambi nyingi kiasi hiki na sikutubu?" Ndipo akanifunulia dhambi hizo moja baada ya nyingine. Akasema, “Unatakiwa kukiri dhambi zako moja baada ya nyingine ili kwamba niweze kukusamehe dhambi hizo moja baada ya nyingine."

Mara niliona chombo safi cheupe kilichojaa damu. Yesu alivaa vazi jeupe na akashikilia brashi kama ile ya kupakia rangi. Akaniambia, “Kiri dhambi zako moja baada ya nyingine.” Nikasema, “Tafadhali ninaomba unifunulie ni lini nilitenda dhambi hizi?" Akaanza kunifunulia dhambi zangu kana kwamba nilikuwa ninaangalia sinema. Nikaanza mara moja kukiri dhambi zangu; na kila nilipofanya hivyo, alitumbukiza brashi ile kwenye chombo chenye damu na kufuta dhambi zangu. 

Baada ya kutubu dhambi zangu zote moja moja, nyumba yote ilipakwa
damu. Cha kushangaza, mahali pale ghafla, pakawa peupe na panapong'aa sana. Hapo, nikajua kuwa niko safi. Akasema,  "Usianzishe kanisa hapa. Unatakiwa uachane na kazi ya kanisa. Sitazikumbuka kazi ulizofanya kwa miaka hii miwili iliyopita." Nikasema, "Kama Bwana hatazikumbuka kazi zangu, basi ninafanya nini hapa?

Ghafla niliamka. Nilikuwa natokwa na jasho jingi na nguo zangu zote zililowana. Kwa kawaida familia yangu huamka mapema kila asubuhi ili kujifunza Biblia, isipokuwa siku ile. Ilitarajiwa kwamba mafunuo ya Bwana niliyokuwa nikipokea kila usiku yangetimia siku iliyofuata, na nilihofia kwamba ufunuo huu nao ungetimia, kwamba Bwana anarudi.  Natakiwa nifanye nini?” Nilikuwa nina wasiwasi na nikasema, "Kwa nini hamkuamka na kujifunza Biblia. Siku nyingine ni sawa, lakini sio leo! Hamjui ya kuwa Bwana anarudi?” Mama yangu alidhani ninachanganyikiwa tena; kwa hiyo alienda kuomba. Nilikuwa ninatetemeka kwa hofu nikidhani kwamba Bwana angerudi siku inayofuata. Niliamua kukaa tu nyumbani na kutubu. Kwa hiyo, niliahirisha usomaji wa Biblia na mkutano kanisani. Mchungaji aliniuliza,  "Kwa nini tuahirishe mkutano wa kanisani?" Nikasema, "Mara nyingi, baada ya watu kumwamini Bwana, maisha yao hubadilika na kufanywa upya. Lakini najua sasa kwamba Mungu anashughulika na mimi na moyo wangu. Tuahirishe mkutano kwa sababu Mungu hataukumbuka mkutano huu. Hatuwezi kuendelea.” Baada ya hapo, kama inavyosema Biblia, kuhubiri kwenye madhabahu si jambo la msingi [Mt 23:3]. Cha muhimu kabisa ni jinsi unavyoendesha uhusiano wako na Mungu; pia na watu mara unapoondoka kwenye viwanja vya kanisa. Sikutarajia kuwa Mungu angeshughulika na mimi kuhusiana na nyumbani kwangu.  

Nikasema, "Bwana, niambie kinachokupendeza nami nitakifanya. Ni kazi zipi ambazo ni kazi za dhahabu, fedha na mawe ya thamani, niambie tafadhali!" [1 Kor. 3:12]. Bwana akasema, “Ni kweli kabisa unataka kufanya mambo yanayonipendeza?" "Ndiyo!" nikajibu. Bwana akasema, "Sawa, nenda ukawajali watoto wako na mume wako na kuifanya nyumba yako iwe safi. Hilo ndilo unalotakiwa kulifanya." Kwa kweli sikuamini kwa nguvu sana kwamba kuwa hili limetoka kwa Mungu, maana nilikuwa najibidisha sana na kazi za kanisa kiasi kwamba nilikuwa nikifua nguo zangu lakini si za mume wangu. Nilikuwa na kazi nyingi kiasi kwamba sikuwa hata na muda wa kufua soksi zake maana ilinibidi kuangalia watoto na kuandaa mikutano ya kanisa. Nilikuwa na kazi nyingi mno! Mume wangu alifua nguo zake mwenyewe nami nilifua zangu. Baada ya kurudi kutoka kwenye kazi za siku nzima, mume wangu alilazimika kufua nguo zake na kufagia nyumba, ambayo kila mara ilikuwa imevurugikavurugika. 

Nikawaza, "Ee Bwana, hivi haya yanatoka kwako kweli? Hivi niache kufanya kazi yako, nikafanye mambo haya, kweli?" Bwana akasema, "Ndiyo!" Hatimaye, nilianza kufua nguo za mume wangu. Nilipofanya hivyo, Bwana aliendelea kunifundisha. Aliendelea kugusa moyo wangu, na kusema: "Unajua kuwa kufua hii soksi moja ni kazi ya dhahabu, fedha na mawe ya thamani, ambayo ninaikumbuka?" Hilo lilinishangaza kweli. Nikamwambia mume wangu, "Kuanzia sasa nipatie soksi zako zote chafu; nitazifua!” Mume wangu alionekana kushtuka na kuogopa. Akaniambia, "Kwa nini umebadilika ghafla kiasi hiki? Umekuwa mwema ghafla." Nikasema, "Kwa kweli, nimefundishwa na Mungu. Kuanzia sasa, sitakuruhusu ufue nguo zozote.” Kisha mikutano yote kanisani ilifutwa na nikaanza kukaa nyumbani muda wote. Sikutarajia kwamba Mungu angegeuza maisha yangu kwa namna ile. Kusema kweli, nilipokea upako wangu mwingi kutokana na kule kufutwa kwa vikao vya kujifunza Biblia na ile mikutano ya kanisani katika kipindi kile. 

Ni wazi kuwa hii haikutosha. Baadaye, Mungu alinipeleka kwenye nyumba ya mama mkwe wangu. Niliishi Yongnian Handan, na mama mkwe wangu aliishi kwenye nyumba iliyokuwa Cangzhou, kama km 600 kutoka kwangu. Kwa kuwa wao hawakuwa waamini, nilipata manyanyaso sana kutoka kwao. 

Nakumbuka nilipanda basi kwa siku nzima ili kufika kule aliko mama mkwe. Niliwasili wakiwa ndio wakiwa tayari kula. Kila mara nilimfundisha binti yangu kuomba kabla ya kula. Kwa hiyo, kama familia, mara zote tuliomba kabla ya kula. Kwa wakwe zangu, baada ya kuandaa chakula na kumwita kila mmoja, binti yangu wa miaka 2 alisema, "Mama, tuongoze kwenye sala." Babu yake hakuelewa kile binti yangu alichokuwa anasema. Hivyo akauliza, "Liyan, anasema nini?" Nikajibu, "Oh, amesema tuombe, vinginevyo hatakula." Baba mkwe wangu mara moja alimwambia wifi yangu, "Yunyun! Nenda kalete chombo cha ubani. Mwaga mchanga ulio kwenye chombo hicho, kioshe kisha ukijaze tambi kwa ajili ya wifi yako."

Hiyo ndiyo aina ya manyanyaso waliyonipa. Basi, akaniletea chombo kile kikiwa na tambi na kusema, "Haya, chukua ule kutoka kwenye chombo hiki ambacho kina baraka nyingi sana." Ukweli ni kuwa walikuwa kinyume nami. Japokuwa ndio nilitoka tu kuolewa kwenye familia yao, walinitendea kwa namna hiyo. Nikamwuliza Bwana, "Bwana, nifanye nini sasa?" Bwana akasema nami, "Sanamu si lolote; vivyo hivyo chombo kinachotumika kuchoma ubani kwa ajili ya sanamu nacho si lolote." Nikasema, "Bwana asifiwe. Mambo haya si lolote!"

Binti yangu aliendelea kusema, "Mama, omba basi!" Nilikuwa nafikiri, niombe nini sasa? Tayari walishaniwekea chakula kwenye chombo wanachotumia kuabudia sanamu. Nikasema, "Haya! Tuombe! Bwana Yesu, nakupa shukrani na sifa." Mwanzoni nilikuwa nina hofu ya kuomba, lakini kadiri walivyozidi kuniwekea vikwazo, ndivyo nilivyoomba kwa ujasiri. Maneno kutoka kwenye Biblia yalikuja kwenye akili yangu, "usali mbele ya Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi.” [Mt. 6:6]. Mungu akasema nami, “Hii ndiyo kazi ya dhahabu, fedha, na mawe ya thamani.” “Ha, kweli?” nikasema. Vijiti vyangu vya kulia (chopsticks) vilitupwa chini na mtu.Na hii nayo ni kazi ya dhahabu, fedha, na mawe ya thamani? Nikasema, "Sifa kwa Bwana." Nilisimama haraka na kufuta machozi yangu, na mara moja mateso na hasira iliyokuwa ndani yangu vilitoweka. Hakika Neno la Bwana ni faraja kubwa. Kwa hiyo, nilianza kutafuta vijiti vyangu vya kulia sakafuni na nikavipata. Baada ya kula, nilikuwa nikiosha vyombo mara moja tu, lakini safari hii niliosha mara 3, maana Bwana aliniambia kuwa hii ilikuwa ni kazi ya dhahabu, fedha, na mawe ya thamani. Kwa hiyo, nilitaka kuviosha viwe safi kabisa. Na kadiri nilivyoviosha, ndivyo furaha ilivyozidi ndani yangu. 

Halafu, mume wangu alikuja kututembelea bila kutarajiwa. Aliona jinsi nilivyojishughulisha na mapishi na usafi na ndugu zake walikuwa hawafanyi chochote zaidi ya kucheza tu mahjong na kamari. Mume wangu hakuweza kustahimili kile alichokiona; kwa hiyo aliwakasirikia sana familia yake. Kwa kweli, kustahimili mateso imekuwa ni kama jambo la kawaida kwangu. Nikamjibu, "Hakuna tatizo!" Akasema, "Acha kufanya kazi zote za ndani." Nikasema, "Sikuwa nazifanya kwa ajili yao." Akasema, "Tuondoke zetu!" Nikamjibu, "Hapana, hii ni kazi ya dhahabu, fedha, na mawe ya thamani mbele za Mungu." Hakuelewa nilichokuwa nasema. Alitaka niondoke pamoja naye, lakini nilikataa. Kwa hiyo akaenda kunywa mvinyo.

Baadaye alirudi na kukawa na mvutano mkubwa kati yake na wazazi wake. Nikajisemea, “Bwana! Kazi ya dhahabu na fedha itafikia mwisho hivi karibuni.” Mwanzoni, tungeweza kuondoka mahali hapa pamoja kwa furaha, lakini ghafla mume wangu akaamua kuvutana na ndugu zake kwa namna ile. Kutakuwaje na mwisho mwema? Mume wangu alipomaliza kubishana na baba yake, alisema, “Liyan, fuatana nami. Hatutarudi tena kwenye nyumba hii na sitaingia tena kwenye chumba hiki. Kama nitakanyaga tena kwenye chumba hiki, basi sitakuwa mwanafamilia hii." Lakini Bwana akaniambia, "Hapana, huwezi kuondoka sasa." Nilimwambia mume wangu naye alikasirika sana kutokana na jibu hilo na akasema, “Kwa sababu yako, wazazi wangu wananilaani.” Nikasema, "Bwana aliniongoza kuja kuwa sehemu ya familia yenu. Inanibidi nitii mwongozo wa Bwana wangu. Kwa hiyo, unaweza kuondoka." Kisha akasema, "Sawa, nitaondoka. Unaweza kukaa hapa milele na usiondoke kamwe!" Nikasema, "Nitaondoka Bwana atakaponiongoza kufanya hivyo."

Mume wangu aliondoka kwa hasira na kuniacha mimi kwenye nyumba ya wakwe zangu. Nikauliza, "Ee Bwana, nitaondoka lini kwenye nyumba hii?" Bwana akasema, "Subiri kwa muda. Bado si muda mwafaka." Nikasema, "Sawa!

Kila wakwe zangu walipotoa nguo zao, haraka nilienda kuzifua. Kisha ghafla, kwa namna fulani, Mungu akafungua mioyo yao na wakatambua kwamba kazi zote za nyumbani hazikutakiwa zifanywe na mimi peke yangu. Walikuwa wakiwaza, “Huyu mwanamke ameolewa kwenye familia yetu kutoka mbali. Hizi kazi za kufua zinatakiwa kufanywa na binti yetu maana ni wajibu wake kwa kuwa yeye ndiye tuliyemzaa na kumlea.” Baadaye, wakwe zangu ghafla walianza kuwa wema kwangu, kitu ambacho kilinishangaza sana. Nilipokuwa nje nikifua, mama mkwe wangu alitoka na kuja kunifunika kwa nguo, maana kulianza kuwa baridi zaidi. Alisema, “Liyan, hebu jifunike nguo hizi." Baba mkwe wangu aliniletea kikombe cha chai ya moto na kusema, “Njoo, njoo. Kunywa chai ya moto." Nilishangaa sana maana mara zote walikuwa wakininyanyasa; lakini ghafla wakawa wamegeuka na kuwa wema kwangu. Hili lilikuwa jambo gumu kulizoea. Nilijiuliza ni kwa nini wamegeuka ghafla kiasi hicho na kuwa wema kwangu. Baba mkwe hata aliniuliza ni mablangeti mangapi nilikuwa ninahitaji nyumbani.  Alisema, “Nitayaandaa kwa ajili yako. Kama ukiona kitu chochote katika nyumba hii ambacho unakihitaji, wewe kichukue tu. Tutajisikia furaha kukupatia." Nikasema, "hapana, hakuna ulazima wa kufanya hivyo. Sihitaji kitu chochote." Ghafla Bwana akasema nami, "Ni muda umefika. Ondoka mapema kesho." Kulikuwa na tofauti ya siku moja tu kabla Bwana hajaniambia kuondoka; mume wangu aliondoka siku moja kabla na mimi niliondoka siku iliyofuata.

Muda wangu wa kuondoka ulikuwa wa kimiujiza. Watu wa kijiji chote walikuja kuniaga na walinichukulia ungedhani ni mtu maarufu tajiri aliyekuja kutembelea kijijini. Kila mtu alisema kuwa huyu mkamwana ameteseka sana. Ndani ya zile siku 2, alifanya kazi nje na ndani ya nyumba. Ghafla Bwana akasema, "Ole wako, watu wanapokusifu." Nikasema , "Bwana, sikuweza kufanya lolote bila ya neno lako kunitia nguvu. Yote ni kwa sababu ya msaada wako usiokoma. Nisingeweza kuyafanya hayo kwa kiwango kile mimi mwenyewe. Wanakusifu Wewe nami napenda nirudishe utukufu wote kwako."

Safari ya Basi
Baba mkwe wangu alituangalia tukipanda basi ili kurudi ShiJiaZhuang. Tulipanda basi la masafa marefu. Basi lilijaa watu, maana ulikuwa ni msimu wa wanafunzi kurudi mashuleni. Nilipokuwa kwa wakwe zangu, moyo wangu ulipata nguvu, na kulikuwa na upako wenye mamlaka. Wakati nimekaa kwenye basi, niliona kwamba kulikuwa na kipindi kwenye TV chenye lugha chafu. Nilijisikia kinyaa na kusimama. Lakini nilipowaangalia watu walivyo wengi, nilirudi kukaa. Nilifanya hivi mara tatu. Nilifumba macho yangu na kuomba, "Ee! Bwana, nina aibu. Nifanye nini?" Ghafla Bwana alinipa maono ya Yesu ndani ya hekalu, akiwa na hasira ya haki, akisokota kamba ili kulitakasa hekalu. Nilipoyaona maono hayo, sikuvumilia tena. Ghafla, nilisimama na kumwambia dereva wa basi, "Dereva wa basi! Zima TV yako! Unawezaje kuonyesha video ya aina hii mbele za watu? Unaweza kwenda kuiangalia huko nyumbani kwako; lakini je, ni sahihi kuionyesha hapa?

Dereva yule alishtuka. Yeye na mwanamke wa tiketi wa humo ndani ya basi walitazamana. Dereva akauliza, "Kitu gani kimetokea kwake?" Yule mwanamke akasema, "Sijui." Dereva akasema, “Wewe ni nani?" Nikajibu, "Wacha nikuambie. Huhitaji kuuliza mimi ni nani. Kama ukijua mimi ni nani, nitaivunja TV yako na CD yako, nawe utahitaji kulipwa faini!" Sikujua ni kwa nini nilipata ujasiri kiasi hicho. Dereva alipigwa butwaa na kasema, "Haya! Haya! Naizima! Naizima!" Mara moja alizima TV na kuisukumia pembeni. Dada wa tiketi alikaa chini na hakusogea. Kukawa na ukimya mkubwa kwenye basi; mtu angeweza hata kusikia pini ikidondoshwa. Basi lilifika Hengshui, kituo cha kupumzikia, ili kuruhusu abiria kwenda maliwatoni. Watu walipotoka kwenye basi, wengi wao walinitupia jicho huku wakibasamu. Nami pia nilitabasamu. Ilionekana kwamba kila mmoja alikubali kuwa haikuwa sahihi kuonyesha video kama ile pale, lakini hakukuwa na mtu wa kusema, maana dunia na jamii zimeshaporomoka kimaadili hadi kiasi hicho. 

Baadaye, mama mkwe wangu alikuja kukaa nasi. Nilimwongoza sala ya kumkubali Yesu kama Mwokozi wake. Ilikuwa ni Julai, wifi yangu akiwa chuoni alibishana nami sana. Miezi mitatu baadaye, alikuwa kwenye mfadhaiko mkubwa baada ya kuachana na rafiki yake wa kiume. Alijaribu mara nyingi kujiua. Kila mara alibishana nami kuhusiana na masuala ya imani yake. Alijua kuwa ninaweza kumsaidia, lakini alikuwa anasikia aibu kuniomba msaada. Hatimaye baadaye alinipigia simu na kusema, "Wifi, njoo unisaidie. Wewe peke yako ndiye unaweza kuniokoa." Nikasema, "Mimi siwezi kukuokoa. Ni Mungu tu ndiye mwenye uwezo wa kukuokoa. Ungependa kuomba nami ili umpokee Yesu kama Mwokozi wako?" Akasema, "Ndiyo!" Kisha nikaomba naye ili ampokee Yesu Kristo kama Mwokozi wake. Mambo haya yote yalinionyesha kwamba baada ya kuwa kwenye ndoa kwa miaka mingi, kupigana na kubishana hakukumbadilisha yeyote. Lakini nilipoanza kujinyenyekeza, Mungu aliendelea kunishusha ili kwamba siku moja aweze kuniinua. 

Maneno niliyotamka kwenye basi yalikuwa ni matokeo ya mafunzo yangu ya kiroho kwenye nyumba ya mama mkwe wangu wakati nikiosha vyombo, nikifua nguo na kufanya kazi zote za ndani. Mafunzo yangu yote yalitokea kipindi hicho. Nilitambua kuwa kile ambacho ninashughulika na kushindana nacho si mwili wa nje bali ni roho iliyo ndani. Unapotambua kuwa Mungu ndiye nguvu ya moyo wako, nguvu hiyo ni kubwa sana. Nilipambana na magonjwa mengi kwa muda mrefu, lakini mara moyo wangu ulipoungamanishwa na Bwana, magonjwa yote yaliondoka mwilini. Hivyo ndivyo Bwana alivyo halisi!!  
Nakumbuka zamani kila nilipopata ugonjwa, Bwana alikuwa pamoja nami. Hivyo, hata nilipoumwa, nilikuwa nimejawa na furaha tu. Wapendwa wengi kanisani walidhani nina wazimu. Baadaye, niliwaza labda kulikuwa na tatizo kwenye maneno: “furahini katika mateso”. Wiki mbili za mwisho katika mwezi, nilipokuwa na ushirika na Bwana, nilijumuisha maneno: “Sifurahii mateso, lakini nafurahia uwepo wa Bwana wakati ninapopitia mateso.” Niliwaza: Ni lini huwa ninakuwa na uhusiano wa karibu na Bwana? Jibu ni wakati ninapopitia mateso. Kwa hiyo, ninamsifu Mungu kwa ajili ya mateso yote. Nilicheza na kupiga ngoma nyumbani wakati ninamsifu Mungu. 

Usiku mmoja, nilikuwa na shauku kubwa ya kuwa na ushirika na Bwana kiasi kwamba nilikuwa ninashindana na Bwana na kukataa kabisa kumwacha aondoke. Siku iliyofuata nilipoamka, sikuweza hata kusogeza miguu yangu maana misuli yote ilikuwa imekufa ganzi, kitu ambacho kilinikumbusha habari ya Yakobo juu ya kushindana na Bwana. Bwana aliniwezesha kutambua hilo kidogo kidogo. Ni lazima nimsifu Mungu kwa ajili ya mateso yangu yote. Nilisema, "Ee Bwana, sikujua kuwa umejaa hekima.” Unapomsifu Mungu kwa ajili ya mateso yote unayopitia, ni hekima kutoka kwa Mungu kwa sababu, hekima ya Mungu siku zote huwa juu ya hekima yetu. Alimtuma Mwanawe wa pekee kuja kufa kwa ajili yetu; na alikufa msalabani. Ni hekima ya Mungu na nguvu ya Mungu! Machoni petu, ni jambo la aibu na la kipumbavu; lakini machoni pa Mungu, ni hekima ya kutuokoa sisi sote.

Safari ya Treni
Nakumbuka wakati fulani nilisafiri hadi kaskazini mashariki mwa China pamoja na watoto wetu. Basi lilichelewa kuja. Lilitakiwa kufika saa mbili, lakini lilifika saa tatu. Wanangu walichoka na kulala. Tulipokuwa tunaingia kwenye basi, wanangu waliamka ghafla na kusema kwa kilio, “Nataka kulala. Nataka kwenda nyumbani!” Mume wangu akanipa changamoto kwa kusema, "Hata hivyo, hakuna viti vilivyobaki wazi. Bora tu kurudi nyumbani na kwenda kulala. Tuondoke zetu." Wakati huo, kwa kweli sikujua cha kufanya. Kusema kweli nilisikia kusukumwa na Mungu niondoke. Nikasema,  "Bwana, maisha yangu yote ni kwa ajili yako. Sijali juu ya maisha yangu, lakini nisingependa mume wangu na wanangu wateseke pamoja nami." Ghafla Bwana akasema nami, "Unajua nitakavyokuja kuwapa thawabu hapo baadaye? Nataka na wao waje wapate thawabu sawasawa na wewe." Kisha mume wangu akasema, "Ama twendeni nyumbani au tukakate tiketi." Bwana alinipa neno, kwa hiyo nikasema, "Twendeni tukakate tiketi."

Mwishowe, tulijipenyeza hadi tukaingia ndani ya treni. Lakini kulikuwa na watu wengi sana. Hivyo, tuliweza tu kusimama mlangoni. Ghafla Bwana akasema, "Liyan, nisifu Mimi. Nataka kusikia ukinisifu Mimi!" Nikasema, "Ee Bwana, usinitanie. Nawezaje kukusifu wewe kwa sauti kwenye muda kama huu?" Bwana akanipa changamoto akisema, "Jaribu na unisifu Mimi. Nataka kusikia." Nikasema, “Bwana, hapana." Bwana akasema, "Ndiyo. Nisifu Mimi!” Nikasema, "Bwana, hata kama nikikusifu Wewe, nakwambia ukweli, nitakuwa naongopa. Sifa hizo hazitatoka moyoni mwangu." Kisha Bwana akasema, "Hata kama si kutoka moyoni mwako, hakika bado nataka kusikia sifa kutoka kwako; na nataka kusikia ukinisifu Mimi katika muda kama huu." Nikasema, "Bwana, ina maana unaniruhusu kukudanganya? Sina sifa zozote ndani yangu." Hapo Bwana alizungumza kutokea ndani yangu akisema, "Kama hunisifu Mimi katika hali kama hii, basi hauna tofauti na watu wengine. Una tofauti gani na wasioamini? Hao wasioamini humshukuru Mungu kwa kufanikiwa kuingia kwenye treni. Kuna tofauti gani kati yako na wao?"  "Ndiyo, niko tofauti na wao … Ee Bwana. Mimi ninakusifu Wewe!

Wakati nikijaribu kumsifu Mungu, kulikuwa na watoto wakilia, watu wamejaa, kuna harufu mbaya kila mahali, na jasho la moto kwenye ngozi yangu. Nikasema, "Bwana, ninakusifu Wewe kwa sababu ninaweza kujipenyeza kwenye treni hii." Mara nilipoanza kumsifu Mungu, moyo wangu ulitulia. Nikasema, "Bwana, nasifu hekima Yako kwa sisi kutopata viti. Naamini utanipa nguvu ya kusimama hadi mwisho wa safari na ninaamini unazo nguvu nyingi." Kadiri nilivyozidi kumsifu Mungu, ndivyo watoto walivyopunguza kulia. Kadiri nilivyoendelea kusifu, ndivyo furaha ilivyoongezeka ndani yangu. Kisha Mungu akanipa changamoto wakati nimesimama kwenye mlango wa choo nikiwa nimemshikilia mwanangu mikononi; na nikaanza kurukaruka na kusema, “Bwana, pokea sifa. Nakushukuru. Nakupenda. Yehova Mungu ni nguvu zangu. Nakupenda. Nakusifu. Nakusifu." Nilisifu mfululizo. Kulikuwa na watu wa kila aina wamenizunguka kwenye treni, lakini hawakusikia nilichokuwa nasema. Niliendelea kusifu na kusifu. 

Baada ya muda, mume wangu akaniambia kuwa alitaka kutafuta tiketi ya daraja la juu zaidi ili aone kama tunaweza kupata sehemu yenye kiti cha kitanda. Ukweli wakati huo moyo wangu haukujali kama tutapata au la.  “Ee Bwana, Wewe uko na mimi. Utanisaidia kusimama hadi mwisho wa safari. Nina imani kubwa ndani yangu. Ninakushukuru sana.” Watu wengi walisimama mstari ili kupata tiketi hizo. Hatimaye, mume wangu akasema, "Sifa kwa Bwana!" Nikasema, "Nguvu ya ndani ya kutoa shukrani kwa kupata kiti cha kitanda ni kubwa; lakini nguvu ya ndani ya kutoa shukrani ni kubwa zaidi kama nisingepata hicho kiti."
Wakati maisha ya kiroho ya watu wengine yanapokuwa hayajafikia ngazi sawa na ya kwako, utakuta kwamba maisha yako ya kiroho yako juu zaidi. Maisha yako ya kiroho yanapofikia ngazi ya juu zaidi, unafanya nini? Utaona mbali zaidi! Mateso yote mbele za macho yako yanakuwa ni jambo dogo sana. Mateso ni chakula cha kiroho. Ni virutubisho vya maisha ya kiroho. Njoo ule na mwili wako utakuwa na afya. Kwa hiyo, hivi karibuni nilipokuwa niko nyumbani, nilijisikia maumivu kwenye mguu na kiunoni. Kwa kawaida, kunapokuwa na maumivu, huwa nayafukuza maumivu hayo kwa jina la Yesu. Hivyo niliyakemea maumivu hayo, “kwa kupigwa kwa Yesu Kristo, nimepona!” Kila mara ninaposema hivyo, maumivu huondoka mara moja. Lakini safari hii hakuna kilichotokea. “Ni kwa nini?” nikajiuliza. Kisha nikaingia kwenye maombi mazito, na nikamwuliza Bwana kwa njia ya Roho Mtakatifu. Bwana akasema, "Unajua jinsi ambavyo hauna utii? Kwa nini una maumivu ya mguu? Unahitaji kumsifu Mungu! Kwa nini una maumivu ya kiuno? Unahitaji kumsifu Mungu!" Ndipo nikaelewa kwamba nilikuwa sitoi ushirikiano. Nikasimama, nikajinyosha miguu yangu na kunyonga kiuno changu, maana mwili wangu wote utamsifu Bwana wangu! Nikajibiringisha kwenye sakafu. Nilifunga mlango ili mume wangu asinione akadhani nimechanganyikiwa. Mara nyingi huwa namsifu Bwana kama mtu mwenye wazimu. Nilipokuwa nabiringika sakafuni nikimsifu Mungu, ghafla nilibaini ukweli, pale Bwana aliposema, "Haujaona waigizaji kwenye jukwaa hutumia kila njia kuigiza ili waweze kupigiwa makofi na kutiwa moyo kila mtu? Je, unajua jinsi ninavyojawa na furaha pale unaponisifu Mimi?

Mara nyingi huwa namsifu Mungu nikiwa na dada mmoja hadi usiku wa
manane tukiwa sehemu fulani mbali na mji; mahali ambako tunaweza kumsifu Mungu kwa uhuru. Usiku mmoja, tulimsifu Mungu na kumwomba hadi saa 8 usiku, na dada yule akalala. Niliendelea kuomba kwa nusu saa nyingine ndipo nikaona maono. Niliona malaika wawili, kila mmoja ameshikilia kikombe cha dhahabu kikubwa sana. Malaika wale walikuwa wanadaka vitu kutoka kwetu. Wakati huo, sikuelewa kile ambacho malaika walikuwa wakikamata, lakini nilisisimka kweli kuwaona na nikawa nasifu na kuomba zaidi na zaidi. Niliimba nyimbo katika roho na malaika wale waliendelea kushikilia vikombe vile vya dhahabu na kukamata vitu kutoka kwetu…. Niliomba kwa muda mrefu hadi sauti yangu ikaanza kupungua, nilipoona kuna kitu kimejaa na kufurika kwenye kikombe kile; nami nikaacha kuomba. Nilikuwa na shauku ya kuona kuna nini ndani ya vikombe vya dhahabu. Nilidhani labda ni machozi, mvuke, au kitu kama hicho! Lakini nilioangalia kikombe kimojawapo, kilikuwa kimejaa manukato, huku kikombe cha malaika mwingine kikiwa kitupu. Kilikuja kitupu na kikarudi kitupu. Nilishangaa sana. Kulipokucha, nilijilaza na kupata usingizi kwa muda. Sikumwambia yule dada kile kilichotokea usiku ule. Alisema, "Nilijisikia usingizi sana, lakini nilikuwa nikikusikia ukiomba kwa bidii. Je, uliona maono?"

Baadaye, nilipopiga magoti pembeni mwa kitanda changu kumuuliza Bwana, ghafla Bwana alifungua ufahamu wangu na kusema, "Ewe mwenye welewa kidogo. Kuna malaika wawili. Mmoja wa kwako na wa pili wa rafiki yako.” Nikamwuliza Bwana, "Kwa nini malaika ameshikilia kikombe?" Bwana akajibu, "Ili kukamata maombi yako." Kisha nikaendelea kuuliza, "Kwa nini kikombe changu kimejaa na kufurika, na kwa nini kingine kilikuwa kitupu?" Bwana akajibu, "Mwenzako alilala usingizi." Nikasema, "Kirahisi hivyo?" Bwana akasema, "Ndiyo, kikombe kinajazwa na maombi yako. Malaika atakiinua mbele za Mungu. Mungu atatumia maombi yako kutengeneza upako na kuumimina. Kwa hiyo, maombi yanaweza kabisa kuharibu ufalme wa ugonjwa, hata kama ni kansa, kwa sababu upako unatengenezwa na Mungu, na unapomiminwa kutoka kwa Mungu, unakuwa na nguvu sana, na unaweza kuharibu mamia ya falme za shetani."

Mara nilipotambua jinsi upako unavyotokea, niliyapenda maombi ya usiku kuliko mwanzo, na nikawa naomba bila kukoma. Wakati mwingine mwili unapolemewa, Bwana anasema ghafla, "Liyan, amka." Nami ninasema, "Nahitaji kulala kidogo." Bwana aliuliza, "Utatengeneza nini kutokana na usingizi? Je, unaweza kuzalisha upako kutokana na usingizi?" Nikasema, "Hapana." Bwana akauliza, "Unaweza kuzalisha imani kutokana na usingizi?" Nikasema, "Hapana." Bwana akauliza, " Unaweza kuzalisha upendo kutokana na usingizi?" Nikasema, "hapana." Bwana akasema, "Vitu hivi vyote viko wapi? Viko ndani ya maombi yako." Mara moja nilielewa, na nikainuka na kupiga magoti sakafuni na kuomba. Nikaendelea kuomba ili upako huo wenye nguvu uje. Niligundua kwamba upako huo ni halisi kabisa.

Kwa hiyo, ni lazima tujenge madhabahu nyumbani, katika siku hizi za mwisho, maana Mungu anataka kutupatia baraka nyingi sana. Huu ndio ufunuo niliopokea pale nilipojifungia kwa siku nyingi na kuomba. Bwana alisema, "Hakuna kusubiri tena. Tuko kwenye kipindi cha kitabu cha Yoeli." Kitabu cha Yoeli kinasema: Hata itakuwa, baada ya hayo, ya kwamba nitamimina roho yangu juu ya wote wenye mwili. Usingoje zaidi; huu ndio wakati wenyewe. Hivi sasa Roho wa Mungu anamiminwa, na Bwana alisema kwamba katika siku hizi za mwisho anazo baraka nyingi. Baraka hizo si za mali za kimwili, bali mafunuo juu ya nyakati za mwisho. Kwa waamini, kujua mafunuo ya nyakati za mwisho kutaleta uamsho wa kanisa zima. Mara uamsho utakapokuja, ufalme wa Mungu utakuja mapema baada ya hapo. Kupitia sisi, ufalme wa Mungu utaenea kote.  

Hivi sasa tunaingia kwenye siku za mwisho. Tumia muda mwingi zaidi ukijenga uhusiano wako na Bwana, Mwokozi wako. Bwana anatamani kumpa kila mmoja ujumbe wa namna hii; na anatarajia kuwa kila mmoja ataamka. Huu pia ni ujumbe niliopokea siku chache zilizopita nikiwa peke yangu, katika ushirika na Bwana huku nikiomba mahali pangu pa siri. Roho wa Bwana atamiminwa kwa wote wenye mwili, ili kwamba sote tuweze kwenda na mwendo ya Roho Mtakatifu. Kama huwezi kwenye na mwendo ya Roho Mtakatifu, utaanguka; na mara ukianguka, umaskini, magonjwa na majanga ya dunia yataongezeka zaidi na zaidi. Utapata mateso kwenye kipindi cha mwisho, na hali itakuwa ngumu sana kwako!

………………………………………

Mpendwa msomaji wa blog hii, asante kwa kusoma Makala haya na Bwana atutie nguvu ili tuweze kusimama katika nyakati hizi za mwisho. Tutafute chakula, mavazi, nyumba na kadhalika, lakini tusisahau kuwa hivyo vyote ni vitu vidogo sana; si kipaumbele cha kwanza. Kristo na uzima wa milele wa roho zetu pamoja na utakatifu ndivyo kipaumbele namba wani.

Kama ungependa kusoma ushuhuda huu kwa Kiingereza, basi bofya HAPA.

Bwana akubariki, akushikilie na kukutia nguvu, katika Jina la Yesu.

9 comments:

  1. Barikiwa na Bwana mpendwa kwa kutuwekea shuhuda zenye kuimarisha imani yetu. Kwa kweli tumaini letu ni YESU TU

    ReplyDelete
  2. Ubarikiwe sana James ushuhuda huu umenijenga sana nimegundua kuwa kumbe Huduma tunazofanya tunatakiwa Mungu azihakikishe

    ReplyDelete
    Replies
    1. Amen mpendwa. Zidi kubarikiwa na kuinuliwa na Mzee wa Siku, Yesu Kristo.

      Delete
  3. Bwana atutie nguvu katika safari yetu.

    ReplyDelete