Saturday, November 24, 2012

Mwana Mpotevu




Hadithi ya mwana mpotevu inafahamika kwa wasomaji wa Biblia. Vilevile, inafahamika kwa habari ya uhusiano wake na mtu yeyote asiyeokoka; yaani mwana mpotevu anawakilisha watu ambao hawajaamua kumpokea Kristo awe Bwana na Mwokozi wao binafsi. Hadithi hii inaashiria jinsi ambavyo Mungu amempa mtu wa aina hiyo uzima, afya na baraka nyinginezo, lakini badala ya kukaa nyumbani mwa Baba, ameamua kwenda kule duniani na kuishi maisha ya utapanyaji. Hata hivyo, pale anapotambua kuwa amepotea na kuamua kurudi kwa Baba, muda wote Baba yuko tayari kumpokea kwa furaha na upendo mwingi. Sote tuko hivyo. Hapo ndiko tunakoanzia.


Lakini huenda jambo ambalo halizungumzwi sana ni kuwa, hadithi hiyo haina mwana mpotevu mmoja, bali wawili. Pamoja na kwamba mwana mdogo alitenda makosa, pale aliporudi baba yake hakusema, “We mtoto, yaani umeenda huko ukala kila kitu; sasa umeona kuwa umeishiwa halafu unajidai eti ‘nimekosa, nimekosa’, ukome kabisa! Rudi huko huko! Mjinga mkubwa we!”

Baba hakusema hata neno moja la kumlaumu mwanawe au kuhusiana na makosa yake; hata moja! Kwa nini?

Maandiko yanasema: Tuikiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote. (1 Yohana 1:9).

Mara nyingi tunamkosea Mungu na mawazo ya hatia yanatujaa mioyoni kiasi kwamba tunakosa amani, na kushindwa tena hata kuomba. Hata mwana mpotevu naye alijawa na mawazo ya hatia vivyo hivyo. Anapojadili moyoni mwake kwamba: Nitaondoka, nitakwenda kwa baba yangu na kumwambia, Baba, nimekosa juu ya mbingu na mbele yako. (Luka 15:18).

Kimsingi, hii ilikuwa ni hatia inayomtafuna moyoni mwake.

Tunapovamiwa na roho ya hatia, kunakuwa na mambo mawili yanayokuwa mbele yetu, na mojawapo linaweza kutokea.
1. Hatia ile inaweza kuwa kubwa na mtu akakubaliana nayo, hivyo akakata tamaa, akanyong’onyea, akajiona hafai na akaanza kumwogopa Baba. Matokeo yake ni kwenda mbali zaidi na zaidi. Yuda Iskariote alikosa, lakini alilemewa sana na hatia ya kosa lake kiasi kwamba, badala ya kwenda kwa Baba, alienda kujinyonga.
2.  Jambo jingine linaloweza kutokea baada ya kukosa na moyo kujawa na hatia ni kwenda kwa yule uliyemkosea, yaani kwa Baba. Mwana mpotevu alisema, “Nitakwenda kwa baba…” Petro alipomkana Yesu, badala ya kukimbia mbali kama Yuda, alipiga magoti na kumwomba Baba msamaha.

Mwana mpotevu alirudi kwa baba yake na matokeo yake, badala ya kubaki akiwa amepotea, alipatikana; badala ya kubaki akiwa mfu, alifufuka.

Ni muhimu kukumbuka jambo hili: Pendo la Mungu kwetu halitegemei uzuri wetu. Baba hasemi kuwa, ‘Kwa vile mwanangu huyu amekuwa na tabia nzuri, basi sasa ninampenda.’ Hapana! Mungu ni pendo usiku na mchana! Uwe mtii au muuaji, Mungu anakupenda tu kwa pendo kamilifu katika Kristo Yesu. Pendo hili halibadiliki kamwe.

Shetani asikudanganye kwamba wewe ni mwovu mno kwa hiyo Mungu ana hasira sana na wewe. Mungu hapendi dhambi; lakini wewe na mimi anatupenda kwa upendo wenye nguvu kuliko mauti.

Hii haina maana kuwa tuko huru kutenda dhambi na kwenda kutubu tena na tena kisa eti Mungu anatupenda. La hasha!!! Kati ya maandiko yanayoogopesha sana ni pamoja na hili: Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, haibaki tena dhabihu kwa ajili ya dhambi. (Waebrania 10:26).

Ni hakika kabisa kuwa Mungu anatupenda SANA lakini pia Neno lake halitapita bure, lazima yote yatimie. Atakapotoa hukumu siku ya mwisho, hatafanya hivyo kwa kuwa anawachukia wale atakaowatupa motoni, bali ni kwa sababu hawezi kutenda nje ya Neno lake ambalo ndilo sheria isiyobadilika ya maisha haya na yale yajayo. Neno linasema … mshahara wa dhambi ni mauti. (Warumi 6:23). Sasa, kama mtu ameishi katika dhambi maishani mwake; alikataa neema ya wokovu kwa hiari yake mwenyewe, Mungu hana jinsi isipokuwa kutekeleza kile ambacho Neno linasema kuhusiana na mtu kama huyo.

Hebu turudi sasa kwa mwana mkubwa. Moyo wa toba wa mwana mdogo ulimwezesha kupokea pendo la Baba ambalo lipo tu na halibadiliki wala kupungua na halikuwahi kubadilika au kupungua tangu aondoke nyumbani.

Lakini kitendo cha kumpokea tena mwana mpotevu huyu kiliamsha hisia za uchungu, wivu, masikitiko na hata chuki ndani ya moyo wa mwana mkubwa. Alisema, Tazama, mimi nimekutumikia miakamingapi hii,wala sijakosa amri yako wakati wowote, lakini hujanipa mimi mwana-mbuzi, nifanye furaha na rafiki zangu; lakini, alipokuja huyu mwana wako aliyekula vitu vyako pamoja na makahaba, umemchinjia yeye ndama aliyenona. (Luka 15:29-30).

Sijui ndugu msomaji umekuwapo kanisani au ndani ya wokovu tangu lini. Huenda unasema, “Nimekuwa mwombaji, nimekuwa mtii, ninatoa sadaka na zaka, ninawahi kanisani, ninashuhudia wasiookoka, n.k., n.k., lakini Bwana uko wapi? Baba, hata kuniponya? Hata kunipa mume/mke? Hata kunipa mtoto? Hebu ona hawa wengine; mbona wameokoka hivi karibuni tu na umewajibu? Hii ni halali kweli?”

Siku moja Bwana Yesu akaongelea juu ya maombi ya mtoza ushuru na farisayo. Wakati mtoza ushuru anajuta kwa kujiona asivyo na haki na alivyo mpungufu mbele za Mungu, farisayo yeye anaeleza jinsi alivyo na haki na namna  anavyostahili. Alisema: Ee Mungu, nakushukuru kwa kuwa mimi si kama watu wengine, wadhalimu, wanyang’anyi, wazinzi wala kama huyu mtoza ushuru. Mimi nafunga mara mbili kwa juma; hutoa zaka katika mapato yangu yote. (Luka 1811-12).

Na Bwana anatueleza hukumu ya Mungu juu ya hali hii. Anasema: Nawaambia, huyu (yaani mtoza ushuru) alishuka kwenda nyumbani kwake akiwa amehesabiwa haki kuliko yule; (yaani farisayo) kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa. (Luka 18:14).

Hii ni kusema kwamba, kati ya wale watoto wawili wa yule baba, mtoto yule ambaye, kwa moyo wa unyenyekevu, alijiona jinsi ambavyo hana kitu alipata; na yule aliyejiona ana kitu, alipoteza vyote.

Maana yake ni kuwa, sisi binadamu hatuna chochote  cha kujisifia mbele za Mungu isipokuwa katika kile ambacho tumepokea kutoka kwake. Maandiko yanasema: … matendo yetu yote ya haki yamekuwa kama nguo iliyotiwa unajisi. (Isaya 64:6). Matendo ya haki ni matendo yote mazuri kama kutoa sadaka, kusali, kusaidia wenye shida. Lakini kinachoyatia unajisi ni  ile hali ya kudhani kuwa hayo ndiyo yanayonunua au kugharamia baraka na upendo wa Baba.

Kwanza tunatakiwa kutambua kuwa baraka na upendo wa Baba tunaupokea kwa kuwa tu tumemwamini; si kwa vile tumesali sana au tumetoa sadaka sana. Ndipo matendo ambayo Roho Mtakatifu atayafanya kupitia sisi baada ya hapo ndiyo yanayokubalika mbele za Mungu. Hayo ndiyo sadaka yenye harufu nzuri mbele za Baba.

Ninaponung’unika, hiyo ni ishara kwamba nilikuwa ninatenda matendo mema kwa lengo la ‘kulipia’ au ‘kununua’ wema na baraka za Mungu.

Mwana mpotevu pamoja na mtoza ushuru waliua kila kitu ndani yao ili kuvipata. Kwa kawaida nafsi huwa inatuambia, “Hili jambo ni halali yako kabisa. Usikubali kunyang’anywa. Huyo mwingine anayepewa hata hastahili.” Maandiko yanasema: Mwenye kuiona nafsi yake ataipoteza; naye mwenye kuipoteza nafsi yake kwa ajili yangu ataiona. (Mathayo 10:39).

Mwana mkubwa alijihesabia haki akifikiri kuwa pendo la Baba linapimwa kwa mizani – kwamba ukitenda zaidi, unapendwa zaidi; ukitenda kidogo, unapendwa kidogo. Hakujua kuwa Baba anawapenda watoto wake wote sawasawa – wawe wema au waovu.

Kwa hiyo, furaha ya mtoto yeyote haitegemei pendo la Baba – haina maana kuwa, ukiwa na furaha kidogo ni ishara kuwa umepokea pendo la Baba kidogo; au mwenye furaha kubwa amepokea pendo zaidi la Baba. Hapana! Maana malango ya pendo la Baba yamefunguliwa hadi mwisho. Baba ameshamwaga pendo lake lote kwetu sote.

Tofauti inatokana na upande wetu. Inategemea kiasi ambacho kila mtoto amefungua mlango wa moyo wake ili kuruhusu na kupokea mmwagiko wa pendo la Baba. Hatuna haja ya kujilinganisha na wengine ili kwamba eti tuweze kujua kama tunapendwa au la. Badala yake, tuna haja ya kujilinganisha na na ahadi ya Baba iliyo kwenye Neno lake. Basi!

Baba anakupenda; ananipenda kwa pendo kamilifu. Imeandikwa: … Mungu liupenda ulimwengu hata akamtoa mwanawe … (Yohana 3:16). Lakini pale tunapojilinganisha na wengine, kisha tukaona jinsi wao walivyo tofauti na sisi (yaani tunaona kuwa wamebarikiwa zaidi), ndipo tunapofungulia milango ya uchungu, wivu, hasira, n.k.; na kuufungia nje upendo wa Baba. Halafu tunageuka tena na kusema, “Baba hanipendi kama anavyompenda fulani.”

Aina hii ya mawazo ilimwingia pia Petro. Bwana aliwakuta Petro na wenzake wakiwa baharini wakivua samaki.  Baadaye Bwana akamwambia Petro: Nifuate. (Yohana 21:19).
Maandiko yanasema kuna mtu mwingine naye alisimama na kuanza kumfuata Bwana. Imeandikwa: Petro akageuka akamwona Yule mwanafunzi aliyependwa na Yesu anafuata. (Yohana 21:20). Huyu alikuwa ni Yohana. Bila shaka alifanya hivyo kwa kuwa alikuwa ana uhakika kuwa Baba anampenda hata kama aliyekuwa ameitwa ni Petro.

Lakini Petro, badala ya kutazama mwito alioitwa nao, na kusimama katika huo, alianza kumwangalia mwanadamu (Yohana), kisha inasema: Basi Petro akamwona huyo, akamwambia Yesu, Bwana, na huyu je? (Yohana 21:21).

Je, Baba alimjibu nini Petro? Alimwambia: Ikiwa nataka huyu akae hata nijapo, imekupasaje wewe? Wewe unifuate mimi. (Yohana 21:22).

Bwana anatuagiza kwamba: Msiwiwe na mtu cho chote, isipokuwa kupendana. (Warumi 13:8). Jambo lolote lisilotokana na pendo halitokani na Baba. Wivu, hasira, chuki, uchungu, manung’uniko …n.k.,  havitokani na Baba. Na kwa kiasi kikubwa, haya yanatokana na sisi kujilinganisha na wengine na kujihesabia haki kutokana na juhudi na bidii yetu katika Bwana.

Pamoja na uelekevu wake mkubwa, Ayubu naye alifika mahali ambapo alilemewa na majaribu. Matokeo yake alianza kuingiwa na hali ya kunung’unika. Ndipo Bwana akasema: Ni nani huyu atiaye mashauri giza kwa maneno yasiyo na maarifa? Basi jifunge viuno kama mwanamume, maana nitakuuliza neno nawe uniambie. (Ayubu 38:2-3).

Kisha Bwana alianza kumwuliza Ayubu maswali ambayo, hatimaye, Ayubu alitambua jinsi ambavyo hana cha kujisifia mbele za Bwana na wala hana cha kumdai Bwana hata kama angefanya juhudi au wema kiasi gani.

Mambo yote tunayopitia ni upendeleo tu kutoka kwa Bwana. Unapopitia shida kisha ukapata fursa ya kumwamini licha ya ugumu wa hali inayohusika, ni upendeleo na baraka kubwa kutoka kwake. Hatuwezi kuona kikamilifu maana yake sasa, lakini mwisho wa safari, kila aliyesimama na Bwana atachekelea.

Kutokana na hayo niliyoandika hapo juu, mtu anaweza kudhani kuona kama kwamba nataka kusema kuwa, “Usihangaike na watu wengine. Wewe angalia mambo yako na Mungu tu.”

Ni kweli nimesema hivyo. Lakini huo ni upande tu unaohusu kuchunga roho ya wivu, uchungu na kujilinganisha na wengine isivyo sawa. Lakini maandiko yanasema kuwa tuwe na nia ileile iliyokuwa ndani ya Bwana wetu Yesu Kristo (1 Petro 4:1). Ni lazima tuwapende, tuwaombee, na kuwatakia mema wengine. Mwana mkubwa alitakiwa kumwombea na kumtakia mema mdogo wake. Petro alitakiwa kufurahia pale Yohana naye aliposimama kumfuata Bwana.

Lakini tunawezaje kufanya haya? Hatuwezi! Ni Roho wa Baba ndiye anayetuwezesha. Bwana anasema wazi, Pasipo mimi hamwezi kufanya neno lolote. (Yohana 15:5).

Jambo la kujiuliza kila wakati ni je, nimechagua njia ya wivu, uchungu, manung’uniko na kujihesabia haki au nimechagua kumwomba Bwana anisaidie?

Upotevu wa mwana mdogo si hatari sana kama wa mwana mkubwa. Ule wa mwana mdogo unaonekana na kujulikana wazi lakini ule wa mwana mkubwa umejificha na si rahisi kuutambua kama mtu hayuko makini.

Baba alitoka kwenda kumlaki mwana mdogo na mwana mdogo akafungua moyo wake wote, akapokea mmwagiko wa pendo la Baba. Kwa kiwango kilekile cha pendo hakikumwacha mwana mkubwa. Imeandikwa, Basi babaye alitoka nje, akamsihi. (Luka 15:28).  

Lakini huyo mkubwa alifunga mlango wa moyo wake. Alifungia nje upendo wa Baba ambao ulikuwako kwa ajili yake kama ilivyokuwa kwa ajili ya mdogo wake.

Matokeo yake, aliyekuwa amekufa , alifufuka na kuingia kwenye furaha na pendo la Baba. Yule ambaye alikuwa hai, alikufa na kukosa furaha na pendo la Baba!

Ndiyo maana Mungu anatuasa kwa usahihi kabisa: Anayejidhania kuwa amesimama na  aangalie asianguke. (1 Wakorintho 10:12). Pia anasema, … wengi watakuja kutoka mashariki na magharibi ,nao wataketi pamoja na Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo katika ufalme wa mbinguni, bali wana wa ufalme watatupwa katika giza la nje… (Mathayo 8:11-12).
Ni hatari sana kujiona kuwa tunastahili sana baraka za Mungu kwa vile tu eti tunatoa sadaka, tunasali sana, tunaimba, tunawahi kanisani, n.k., na hasa pale tunapotumia vigezo hivyo kuwaona wengine kuwa hawafai.

Ni kweli unaweza kusema, “Baba, umeniambia niombe, nami nimeomba lakini sijapata nilichokuwa naomba. Ninaomba Roho Mtakatifu unisaidie kufanya kile ambacho kinapunguka hadi nifikie jibu langu.” Lakini usiseme, “Baba, mimi nimeomba kama ulivyoagiza, mbona fulani amepata jibu lake wakati yeye hata haombi kama mimi; hatoi kama mimi; hawahi kanisani kama mimi?”

Huku ni kujihesabia haki na kumdai Mungu. Hakuna mwanadamu anayeweza kumdai Mungu kitu chochote.

Ukristo na wokovu SI DINI! Ni uhusiano binafsi na Mungu aliye hai kila saa, kila dakika, kila sekunde. Ni maisha! Si mkusanyiko wa vitendo vya kusimama, kupiga magoti, kuimba, kufumba macho, n.k., vinavyofanyika wakati fulani tu katikati ya kusanyiko liitwalo “Kanisa” au “ibada.” Kanisa au ibada ni mwendelezo tu wa kile ambacho kinatakiwa kuwa ndiyo maisha yetu muda wote.

Unyenyekevu mbele za Mungu unaokiri kuwa “Siwezi bila wewe ee Bwana”; na uhakika kuwa pendo la Baba kwangu halibadiliki kamwe ni mambo muhimu kuwa nayo moyoni kila wakati.

Pendo la Mungu Baba na Mwana na ushirika wa Roho Mtakatifu viwe nawe siku zote. Amina.

3 comments:

  1. Asante John, nimekupata vizuri sana kwenye ujumbe huu wa Mwana Mpotevu

    ReplyDelete
  2. Asante Yesu Kristo. Nimejifunza na kuelewa jambo muhimu sana kupitia mafundisho haya ya mtumishi wako. Amen...

    ReplyDelete