Tuesday, July 17, 2012

Je, ni kweli hatutakiwi kuhukumu?


Naamini umeshasikia mara nyingi watu wakisema, “Usinihukumu bwana. Wewe si Mungu.”

Lakini swali ni kuwa, je, dhana hii hutumiwa na watu kwa jinsi ilivyo sawa? Kabla hatujajibu swali hili, hebu tuchunguze maandiko yafuatayo:


  1. Msihukumu msije mkahukumiwa. Kwa kuwa hukumu ile mhukumuyo, ndiyo mtakayohuku- miwa; na kipimo kile mpimiacho, ndicho mtakachopimiwa. (Mt. 7:1-2).
  1. Au hamjui ya kwamba watakatifu watauhukumu ulimwengu? Na ikiwa ulimwengu utahukumiwa na ninyi, je! Hamstahili kukata hukumu zilizo ndogo? Hamjui ya kuwa mtawahukumu malaika, basi si zaidi sana mambo ya maisha haya? (1 Wakor. 6:2).
Ukisoma maandiko haya unaweza kusema, “Mbona maandiko haya yanapingana?” Au kuna makosa yalifanyika hapa? Katika andiko la kwanza, Bwana Yesu anasema tusihukumu. Lakini katika andiko la pili, Paulo anasema tunatakiwa kuhukumu.

Ajabu ni kuwa, Paulo huyouhuyu ambaye hapa anayesema HUKUMUNI, ndiye anayesema kwenye sura iliyo nyuma tu kidogo kwamba: Basi ninyi MSIHUKUMU neno kabla ya wakati wake, hata ajapo Bwana; ambaye atayamulikisha yaliyositirika ya giza … (1 Wakor. 4:5).  

Nini basi maana ya ‘kupingana’ huku?

Hebu tuanze na maneno ya Bwana Yesu katika Mt. 7 hapo juu. Unapoendelea kusoma mistari inayofuata, utaona kuwa Bwana anasema kwamba: Basi mbona wakitazama kibanzi kilicho ndani ya jicho la ndugu yako, na boriti iliyo ndani ya jicho lako mwenyewe huiangalii? ... Mnafiki wewe,... (Mt. 7:3-5).

Lakini hata hivyo kuhukumu maana yake ni nini hasa? Kuna maana mbili za neno hili. Kwanza, ni kubaini kwamba jambo au hali fulani ni halali au si halali; ni sawa au si sawa; inakubalika au haikubaliki. Mathalani, ukimsikia mtu anasema uongo, moyoni mwako unatambua kuwa hilo ni kosa. Hapo umehukumu.

Maana ya pili ya neno ‘hukumu’ ni kutaja adhabu ya kosa.  Kama utamwambia huyo aliyesema uongo kwamba ‘usipotubu utaenda motoni’, hapo umehukumu.

Sasa je, ni kweli kwamba maandiko hayaturuhusu kufanya hayo? Jibu ni hapana! Ukweli ni kwana, Bwana Yesu hatuzuii hata kidogo kuhukumu. Tunatakiwa kuyafanya hayo. Maana kama tungekuwa haturuhusiwi, utawezaje kumkanya mtu ambaye amekengeuka? Utawezaje kumhubiria injili mtu asiyemjua Yesu? Utawezaje kusuluhisha ugomvi kati ya waliogombana? 

Hata hivyo, ni kweli kwamba maandiko yanapiga marufuku aina fulani ya watu kuhukumu; na yanatoa ruhusa ya kufanya hivyo kwa watu maalumu.

Tumeona hapo juu Bwana Yesu akisema kuwa mwenye boriti jichoni hawezi kuona kibanzi kwenye jicho la mwenzake. Ni wazi kwamba hapa anaongelea uwezo wa kuona mambo kiroho. Ukiwa na maisha ya dhambi hautakuwa na uhalali wa kumkemea au kumhukumu mwenye dhambi mwingine. Dhambi hupofusha ufahamu wa mtu.

Kwa kawaida, mwenye dhambi anapomhukumu mwenye dhambi mwingine, huwa anataka tu sifa na kujikosha mbele za wanadamu ili uovu wake usimulikwe na kuonekana. Ndiyo maana Bwana anamwita kuwa ni mnafiki. 

Tunapokuwa wenye dhambi halafu tunawahukumu wengine, tunakuwa wanafiki kwa sababu mioyoni mwetu tunajua kuwa sisi wenyewe hatuna uwezo wa kuziacha zile dhambi za kwetu.

Hebu tuchukue mfano halisi. Unakuwa uko kwenye daladala. Kisha unamwona msichana au mvulana amevaa mavazi yasiyo ya heshima hata kidogo. Halafu unasema, “Watu wengine bwana, hawana heshima kabisa. Hebu ona alivyo. Ovyo kweli kweli.”

Swali atakalokuuliza Bwana ni kwamba: Ni kweli wewe huwa huvai mavazi ya heshima. Lakini, vipi kuhusu uongo? Vipi kuhusu usengenyaji? Vipi kuhusu wivu? 

Ndiyo maana Paulo akasema kwamba: Lakini wewe, ukiwa unaitwa Myahudi na kuitegemea torati, na kujisifu katika Mungu, na kuyajua mapenzi yake, na kuyakubali mambo yaliyo bora, nawe umeelimishwa katika torati , na kujua hakika ya kuwa wewe mwenyewe u kiongozi wa vipofu, mwanga wao walio gizani, mkufunzi wa wajinga, mwalimu wa watoto wachanga, mwenye namna ya maarifa na ya kweli katika torati; basi wewe umfundishaye mwingine, je! Hujifundishi mwenyewe? (Rum. 2:17-21).

Kwa kifupi anachosema hapo ni kuwa, wewe ambaye unamwambia mwenzio kuwa ni hovyo kwa vile kavaa vibaya unasema hivyo kwa kuwa moyoni mwako unayo namna fulani ya elimu njema inayokufanya utambue jema na baya. Lakini, mbona unaitumia tu katika kushambua wengine lakini huelekezi mishale hiyo kwako mwenyewe? Anza kwanza na dhambi zako ndipo utakuwa na haki ya kuwahakimu juu ya wenye dhambi wengine.

Ni kweli kwamba sisi kama binadamu hatuwezi kujua hali ya moyoni ya mwanadamu mwingine. Lakini Mungu wa mbinguni anaona kila kitu. Ndiyo maana anasema kuwa, siku hiyo atamwambia huyo mnafiki, “Wewe ulisema kuwa Hamisi ni mwongo/ni tapeli hadi watu wakamchukia. Lakini mbona wewe ulikuwa mwizi wa mali ya umma japo wanadamu wenzio hawakujua? Mbona wewe ulikuwa msengnenyaji? Kwa kuwa ulisababisha Hamisi akachukiwa, na wewe ni lazima upate hukumu.” 

Hicho ndicho kitakachotokea. Lakini si Mungu wa mbinguni tu anayeona na kuyajua hayo; hata mhusika mwenyewe anajijua alivyo japo anaweza kuwaficha wengine.

Ni kwamba, sote tu wenye dhambi. Lakini yule mwenye dhambi ambazo hazikutubiwa, hana ruhusa ya kumhukumu mwenye dhambi mwenzake. Msengenyaji hana ruhusa ya kumsema mlevi au mwizi au mvaa ovyo kana kwamba yeye ni salama na bora kuliko wao; mwongo hana ruhusa ya kumsema mchawi kwa kuwa wote wawili sehemu yao ni moja baada ya maisha haya.

Sasa, inakuwaje tena Paulo anasema katika 1 Wakor. 6:2 kwamba tunatakiwa kuhukumu mambo ya maisha haya?

Kimsingi, hata Bwana Yesu anasema jambo lilelile. Wala hawa wawili hawapingani hata kidogo. Ukiendelea kusoma katika Mathayo, Bwana anasema hivi: ... itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako. (Mt. 7:4-5).

Unaona sasa! Kumbe twaweza kuhukumu. Lakini kwanza ondoa boriti jichoni. Kuondoa boriti maana yake kutubu dhambi kwa maana ya kuziacha. Yaani, unatubu kwa nia na makusudi ya kutorudia tena. Hata ikitokea umerudia, inakuwa ni kwa bahati mbaya kabisa, si kwa makusudi huku ukiwaza kwamba, “Si nitatubu.”

Imeandikwa: Afichaye dhambi zake hatafanikiwa; bali yeye aziungamaye na kuziacha atapata rehema. (Mith. 28:13).

Tunapotubu dhambi zetu na kuishi maisha ya utakatifu na ukamilifu, hakika Bwana anatupa ruhusa na wajibu wa kuhukumu na kuwa kinywa chake hapa duniani. Katika hali hiyo, hatuwi mahakimu wadhalimu bali ni mahakimu tunaosukumwa na upendo wa Kristo ndani yetu; ambao nia yetu ni watu wamjue Bwana na wafanikiwe maishani mwao. 

Kwani ukimwambia mlevi aache ulevi, wewe unapata faida gani kutoka kwake? Maana hata hizo fedha huwa hakuletei wewe. Badala yake unamwambia hivyo ili iwe faida kwake na kwa familia yake binafsi.

Mtakatifu anapomwona msichana au mvulana amevaa mavazi yasiyo ya heshima hataanza kuongea kichinichini juu ya namna alivyo ovyo. Huo ni usengenyaji ambao ni dhambi (isipokuwa kama ni mhubiri anayehubiri waziwazi) bila kumlenga mtu mahususi. Badala yake mtakatifu atahukumu kuwa jambo hili si sawa na ama atamwambia hivyo mhusika au atamwombea. 

Lakini kama wewe ni mwizi, Bwana hakupi ruhusa ya kumhukumu huyo mlevi. Badala yake anakutaka utoe kwanza boriti la wizi wako ndipo utaweza kuona kibanzi cha ulevi wa mwenzako.

Hukumu ya mwenye haki si lawama, masimambo na usengenyaji. Hukumu ya mwenye haki huekea kwenye uponyaji wa roho na mwili wa yule anayehukumiwa.

Kwa hiyo, si kweli hata kidogo kwamba hatutakiwi kuhukumu!

Watakatifu tunatakiwa kuhukumu!

8 comments:

  1. ahsante sana kwani nimejua nini maana ya hukum. Mungu wa Mbinguni akubariki!

    ReplyDelete
  2. Mungu azidi kukubariki emback kwa kuendelea kujifunza na kuwa na shauku ya kumjua zaidi. ni jambo zuri kuendelea kujifunza zaidi na zaidi maana hekima yake kwa kweli haina mwisho, kwa hiyo tukikunja mikono na kubweteka, tunajikosesha mengi mno. Lakini tunapokuwa na shauku na kiu ya haki, Yeye yuko tayari siku zote kutufundisha. ubarikiwe sana.

    ReplyDelete
  3. James kwa kuchangia tu mimi nadhani wakati mwingine unakuta unamuelewesha mtu kwa upendo tu yale anayoyafanya kuwa ni kinyume ni misingi ya ukrristo, unakuta mtu anaanza kuchachamaa usinihukumu hata wewe una dhambi, ni kweli mtu anaweza akawa na mapungufu yake pia lakini kukumbushana wajibu sio mbaya japo wakati mwingine watu hulichukulia hili neno vibaya matokeo yake wanaogopa kukemea dhambi wakihisi wataonekana wanahukumu
    Dhambi zisipokemewa kweli tutafika pabaya, na tunaona siku hizi hata makanisani dhambi zinachekewa, watu hawahubiri Kristo wanahubiri mafanikio, kuoa na kuolewa
    Wasiwasi wangu ni kuwa na kundi kubwa lenye watu wenye mafanikio wanaolekea motoni
    Sipo kumuhukumu mtu,ila huo ni mtazamo wangu wapendwa

    ReplyDelete
  4. Unachosema Star ni kweli. Mungu mwenyewe anataka yule anayeona kuwa mwenzake anakosea, amwonye. Lakini jambo msingi ni kuwa, siwezi kumwonya mtu katika jambo hata mimi ni mkosefu. Kama mimi ni mlevi halafu nikaanza kuwaambia wanangu, kwa mfano, acheni ulevi; hicho ndicho anachosema Bwana kuwa ni unafiki. Ni kushughulikia kibanzi cha mwingine wakati mimi nina boriti. Mungu akubariki.

    ReplyDelete
  5. Asante Bwana Yesu kwamba ukutuacha pasipo mwelekeo. Na mwelekeo huo ni Roho Mtakatifu ambaye kwa uhakika haachi kutuambia yaliyo katika Moyo wa Mungu. Naomba tuwe tayari kufundishwa kwani Yesu bado anayo mengi na wala hatutayamaliza.
    Kubwa ni kwamba tufuatilie majira haya tuliyomo ili tupate neema ya kuyapata yote ya majira haya na kuyaweka kwenye matendo kwa ajili ya utukufu wa Jina la Yesu.
    Kuna hesabu katika yote aliyotuandalia:
    -kwamba iko juu kwa kuwa tumekaa kwenye nafasi ya kuyaweka kwenye matendo na Bwana Yesu kuwa upande wetu.
    -tumeshindwa kukaa kwenye nafasi na hivyo kushindwa kuyapata yale Roho Mtakatifu anayafunua kwetu. NI HATARI SANA KWANI HAKUNA MASHAKA YESU ATATUKATAA KWA KUWA FUNGU LETU NI PAMOJA NA ROHO WA UASI, roho wa shetani.
    Kuwa na Yesu ni gharama ndugu zangu,watumishi mliopewa madhabahu waambieni ukweli watu wa Mungu ili Yesu upande wao na sio kuongelea ya dunia hii tu.
    Mwenye sikio na asikie.

    ReplyDelete
  6. naomba ieleweke kuwa aliyeokoka/ambaye Bwana Yesu ni Bwana kwake KWAMBA NI MADHABAHU YA BWANA YESU.
    Neno la Mungu linasema miili imenunuliwa kwa Damu ya thamani na kwahiyo Roho Mtakatifu anakaa, ni kwake, ni madhabahu ya Bwana.
    Na ni Yeye Roho Mtakatifu anayetufundisha KWELI NA HIYO ITATUWEKA HURU. kwa nini nimesema hayo ili nionyeshe kuwa unapokuwa ndani ya wokovu kuna kuwajibika, ndiyo maana inakuwa gharama kwa kila mwana wa Mungu kuijua kweli naye aiseme kweli kwa wengine. Kwa machache haya nimalizie kusema kuwa ukweli hakutatoka kwenye makanisa tu ila kwa kila mwana wa Mungu NA HATIMAYE TUTAONYANA KWA NAMNA MUNGU ATAVUNA KWA INJILI YA KWELI KUSONGA MBELE. AMINA.

    ReplyDelete
  7. Shalom brother Revocatus. Asante sana kwa kututia moyo kwa mashauri yako ya kweli.

    Ni neno la kweli kabisa kwamba wokovu una gharama na kwamba sisi ni lazima tuitafute kweli ya Mungu wetu kwa bidii. Roho Mtakatifu aliye Mwalimu wetu mkuu yuko tayri kutufundisha kama sisi wenyewe tutataka kuyajua yale aliyotuandalia.

    Mungu akubariki sana.

    ReplyDelete
  8. Thank u soo much may God bless u

    ReplyDelete