Tuesday, March 25, 2014

Niliokolewa Toka Kwenye Nguvu za Giza – Sehemu ya 1

Emmanuel Eni alizaliwa nchini Naijeria. Alipitia mateso na dhiki nyingi chini ya vifungo vizito vya ibilisi. Katika ushuhuda huu, anatusimulia kile kilichotokea maishani mwake, mateso aliyopata na hatiamaye jinsi Bwana alivyompa ushindi. 

…………………………………………………….. 

Sura ya 1: Kutorokea kwangu kwenye "Maisha Mapya"

 “Mlee mtoto katika njia impasayo, naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” (Mithali 22:6) 

Hii ni hadithi inayohusu kazi za Mungu – kubwa, za ajabu na za kushangaza – kufuatia kutii kwangu agizo la YESU KRISTO kwangu kwamba: “Nenda ukashuhudie kile nilichokutendea.”

Mara nyingi watu huchukulia matatizo kama ni mambo yaliyo nje ya uwezo wetu na kwamba hatuna tunaloweza kufanya kubadili matukio maishani mwetu. Kwa kiasi fulani hili ni kweli. Kuhusiana na mwana wa Mungu, maisha yake yako katika mpango (Mith 16:9). Kama mpango huo utatimia au la, inategemea mambo kadhaa, yakiwamo ukaribu wa mhusika na Mungu, mtazamo wake juu ya makusudi hasa ya maisha, pamoja na aina ya mazingira ya kijamii na kiroho anakojikuta. 

Mtiririko wa maisha yako unatiwa changamoto na mambo yaliyo nje yako. Mgogoro mkuu unafikiwa pale unapotupilia mbali UTASHI wako, kwa uzuri au kwa ubaya. Unaweza kupenda au kuchukia. Unaweza kutaka kuelewa au kutoelewa. Utashi wa kutii ndio nguvu kubwa kabisa ya Mkristo aliyezaliwa upya; huku utashi wa kutokutii ndio nguvu kubwa kabisa inayomharibu mwenye dhambi.

Mtoto akiachwa peke yake duniani, anatawaliwa na mojawapo kati ya nguvu mbili – uzuri au ubaya; kuwa sawa au kuwa mkosaji; Mungu au ibilisi. Kila mtu anatiwa changamoto na nguvu hizi mbili katika maisha; na kila mmoja wetu ni lazima achague ni maisha gani atakayoishi. Na naamini hicho ndicho ambacho Biblia inachomaanisha pale inaposema: “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.” Utakubaliana na mimi kuwa mtu aliye karibu kabisa na moyo wa mtoto yeyote ni mama yake. Yatima ana bahati mbaya hivyo anaweza kushambuliwa na ibilisi kirahisi zaidi kuliko mtoto mwenye wazazi. Mama ni mlinzi wa mwili na roho lakini inakuwa ni matatizo makubwa wazazi wanapokuwa wamepotea, tena katika mazingira ya kutatanisha.   

Hadithi yangu ilianza miaka 22 iliyopita katika kijiji kidogo kiitwacho Amerie Iriegbu Ozu Item katika Mamlaka ya Serikali ya Mtaa ya Bende, kwenye Jimbo la Imo. Wazazi wangu hawakuwa kati ya watu matajiri lakini baba yangu alibahatika kumiliki hekta 42 za ardhi kutoka kwa babu yangu, baraka ambayo leo imegeuka laana kubwa katika historia ya familia yetu. Baba yangu alikuwa akionewa sana wivu na ndugu zake wa karibu na wa mbali kwa sababu ambazo sizielewi. Labda ni kwa sababu ya hicho kipande kikubwa cha ardhi alichorithi.

Tulikuwa ni familia yenye furaha; tukiwa tumezaliwa ndugu wane: Love, Margaret, Emmanuel na Chinyere. Baada ya kupata mabinti wawili, wazazi wetu walisubiri kwa miaka 14 ndipo nilipozaliwa mimi (mvulana pekee) na baadaye ndipo akazaliwa mdogo wangu wa kike, Chinyere. Hii ilileta furaha kubwa sana kwenye familia japo haikuwa ya muda mrefu kwani muda mfupi baadaye ndipo janga la kwanza lilipotokea. Mama yangu mpendwa alifariki. Ilidaiwa kuwa alikufa kwa kulogwa; na miaka minne baadaye, baba yangu naye alifariki. Naye ilidaiwa kuwa alilogwa.

Miaka miwili baada ya hapo, dada yangu mkubwa, Love, alipotea kusikojulikana na Margaret, anayemfuata, alipata ukichaa. Ulikuwa ni mlolongo wa majanga kwenye familia ambayo ilikuwa haina makuu lakini yenye furaha.

Mimi na dada yangu wa mwisho tulipelekwa kwa babu na bibi yetu. Huko nilimaliza shule ya msingi na kujiunga baadaye na Item High School. Nilisoma hadi Darasa la III na kuacha shule kwa kukosa ada, n.k. Muda mfupi baada ya hapo, babu na bibi nao walikufa. Baada ya taratibu zote za mazishi kwisha, ndugu tusiyemjua alikuja kumchukua mdogo wangu, Chinyere na hadi leo sijui yuko wapi. Kutokana na mateso mengi, nililazimika kurudi kwenye nyumba ya baba yangu, na nikawa naishi peke yangu toka nikiwa na miaka 13. Mtoto wa miaka 13 anawezaje kujitunza peke yake katikati ya maadui wa baba yake ambao pia ni maadui zake? Nilikuwa ni mtu aliyejawa na hofu sana! Matukio hayo yote yalikuwa ni kama yamenifikisha mahali ambako hata kuishi kukawa hakuna maana. Je, kulikuwa na yeyote anayejali? Je, kulikuwa na mtu aliyewaza juu ya majaliwa ya huyu mtoto mdogo?

Siku moja nilikutana na rafiki niliyemjua shuleni, aliyeitwa Chinedum Onwukwe. Chinedum alinipenda sana na baada ya kusikia yote yaliyonikuta, alinichukua hadi kwa wazazi wake ambao nao walikuwa tayari kunipokea kama mtoto wao mwingine. Maisha yalirudi kwenye hali ya kawaida tena. Nilikuwa mwenye furaha tena. Ndipo nilipojua kuwa Mungu ambaye mama yangu alimwomba pale alipokuwa hai alikuwa ni Mungu aliye hai mahali fulani na ndiye aliyenipatia wazazi wengine wapya. Hivyo ndivyo nilivyowaza moyoni mwangu. Nilifurahia hali hii kwa miaka ipatayo miwili, kisha ibilisi alivamia tena!

Chinedum na wazazi wake walikuwa wanasafiri hadi Umuahia na gari yao iligongana na lori lililobeba mchanga. Chinedum na wazazi wake walikufa papo hapo! Niliposikia habari hizi, nilipoteza fahamu. Majonzi yangu yalikuwa makubwa sana. Niliweza kustahimili hadi msiba ulipoisha, ambapo nilikuwa nikiwaletea kuni na vitu vingine wale waliokuwa wakipika. Mwisho wake nilirudi tena kwenye nyumba ya baba yangu na kuanza tena kufanya kazi za mikono ili niweze kuishi.  

Niliendelea kufanya kazi mbalimbali kwenye mashamba, bustani, kuvua samaki, n.k. hadi siku moja, mtu mmoja alinichukua ili nikamlimie shamba lake kwa pesa kidogo (50k). Kule shambani alinihoji maswali mengi sana. Kwanza, aliniambia nimwonyeshe ardhi ya baba yangu. Pili, nimkabidhi hiyo ardhi. Nilimkatalia katakata matakwa yake, naye akawa amechukia. Akaapa kuwa angeniulia hukohuko porini. Niliogopa na nikaanza kukimbia huku nikipiga yowe kuomba msaada.

Kwa bahati mbaya, kwa kuwa sehemu yenyewe ilikuwa ni mbali porini, hakuna aliyekuja kunisaidia, bali Mungu mwenyewe. Mtu huyo alinifukuza huku ameshika kisu. Lakini kwa sababu nilikuwa mdogo, niliweza kukimbia kwa wepesi kuliko yeye. Hatimaye nililitumbukia kwenye shimo la kina cha meta kama 1.82 hivi na nikafunikwa na majani ndani yake. Alinitafuta lakini baada ya muda alikata tamaa. Baadaye nilitoka shimoni na kwa kutumia njia nyingine, nilirudi kijijini. Nilitoa taarifa kwa wazee lakini hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa – hali ambayo huwakuta yatima wote. Jambo hili lilijenga chuki kubwa sana kwenye moyo wangu wa kitoto – hakuna aliyenipenda; hakuna aliyenijali! Niliwaza moyoni mwangu, kwa nini mtu atake kuniua huku akijua kuwa sina wazazi? Maisha yalikuwa yamejaa mateso.  

Sasa naelewa kuwa Mungu katika upendo wake alimzuia ibilisi kuniingizia mawazo ya kujiua. Niligeukia Kanisa na kuwa mshirika kamili wa Kanisa la Wokovu (Assemblies of God) pale kijijini kwangu – na hadi sasa bado ni mshirika – lakini kwa bahati mbaya, hata hapo hakuna aliyenijali japo baadhi ya washirika walifahamu hali yangu. Ni muhimu kukumbuka kwamba, nilifanyika mshirika kamili wa Kanisa hata kabla ya kumjua Yesu Kristo. Sikujua maana ya KUZALIWA UPYA. Kama uko kwenye Kanisa la Yesu Kristo na ukajikuta kwenye hali niliyopitia, mpe Bwana Yesu maisha yako. Maandiko yanasema: “…huku mkimtwika yeye fadhaa zenu zote, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.” (1 Petro 5:7).

Katikati ya magumu na mateso haya yote ALICE alitokea! Alice alikuwa ni msichana niliyemfahamu tokea shuleni. Alikuwa mkubwa kwangu kwa miaka mitano zaidi na tulitokea kijiji kimoja. Tulikuwa darasa moja; tulikaa dawati moja; na tulikuwa marafiki wakubwa. Tukiwa katika ‘mapenzi’ haya ya kitoto, tuliahidiana kuwa tutakuja kuoana tukiwa wakubwa. Mzaha mkubwa! Mtoto wa miaka 11 wakati huo, asiye na wazazi, asiye na elimu, asiye na chakula, anaahidi kumuoa msichana aliyemzidi kwa miaka mitano! Baadaye Alice aliondoka na kwenda Akure kwa ajili ya masomo yake ya sekondari na akawa ananitumia barua nyingi sana za ‘mapenzi’.     

Kwa mara nyingine nilipokutana na Alice, nilikuwa nina miaka 15 na yeye 20. Alishamaliza elimu ya sekondari na alikuwa akifanya kazi Standard Bank Lagos (inayoitwa sasa First Bank), huko ambako waliishi wazazi wake.

Kwa vile Alice alifahamu historia yangu na shida nilizopitia, aliamua kuitumia hali hiyo kwa faida yake. Aliniambia nisafiri hadi Lagos kwenda kuungana naye na akanitumia Naira 50 (Naira ni fedha ya Naijeria)! Hizo zilikuwa ni fedha nyingi sana kwa mtoto wa miaka 15 ambaye hajawahi kupata hata N2 kwa siku! Hii ilikuwa ni mana kutoka mbinguni; nah ii ilinipa picha kuwa Lagos ni lazima kutakuwa ni mahali pazuri sana, penye fedha nyingi na vitu vizurivizuri kwa ajili ya kula raha. Kwa hiyo niliwaza kuwa ni lazima niende Lagos ili na mimi nikatafute fedha zangu na kuwa tajiri kama wengine. Akilini mwangu, kwenda Lagos ilikuwa ndiyo njia pekee ya kutoroka kutoka kwenye mateso yangu; kutoroka mbali na maadui wa baba yangu; mbali na maadui zangu; mbali na njaa na matatizo yangu yote! Kutoroka! Kutoroka! Ndiyo, kutoroka mbali na kila kilicho kilicho kiovu!!!  

………………………………………….

Je, nini kilitokea kwa Emmanuel baada ya hapa? Fuatana nami kwenye Sehemu ya 2 ya ushuhuda huu.

6 comments:

  1. Asante kwa shuhuda hii nasubiri sehemu ya 2 Naitwa Wane Msukwa-Sehemu ya pili unaiweka lini?

    ReplyDelete
    Replies
    1. Asante Wane. Sehemu ya 2 iko tayari kwenye page.

      Delete
  2. Ninawiwa kumshukuru Mungu Kwa Ajili yako kazi yako njema Mtu wa Mungu Ninasubiri sehemu ya pili Asante = Apostle Peter Minja JPP-MINISTRY

    ReplyDelete
    Replies
    1. Barikiwa Mtumishi wa Mungu aliye hai, Apostle Peter. Naendelea kuweka sehemu moja baada ya nyingine.

      Delete
  3. mungu akubariki mtumishi wa mungu James, nimejifunza jambo kubwa sana kuwa mpango wa kuokolewa kwa mtu unnaanza mbali sana. Anyango

    ReplyDelete
  4. Shalom Anyango

    ubarikiwe na Bwana. Tuendelee kujifunza.

    ReplyDelete