Wednesday, December 11, 2013

Saa 8 mbinguni - Sehemu ya 1





Mchungaji Ricardo Cid



Mchungaji Ricardo alipata mafunuo mbalimbali kutoka kwa Bwana Yesu kuhusiana na hali ya kanisa, haja ya kuwa waombaji wenye bidii, haja ya kujiandaa kwa ujio wa Bwana, unyakuo na kadhalika. Karibu kwenye Sehemu ya 1 ya ushuhuda huu wenye nguvu ambao, kupitia humu, Bwana atasema na moyo wako na kukupatia msukumo mwingine wa kusonga mbele zaidi katika safari hii ya kiroho katika maisha haya ya kimwili.

...........................

Bwana anasema, “Natuma ujumbe huu kwa watu wangu walioko duniani, maana Mimi nakaa kwenye ulimwengu wa roho.”
Ufunuo 4:1
Baada ya hayo naliona, na tazama, mlango ukafunguka mbinguni, na sauti ile ya kwanza niliyoisikia kama sauti ya baragumu ikinena nami, ikisema, Panda hata huku, nami nitakuonyesha mambo ambayo hayana budi kuwako baada ya hayo.
Ufunuo 5:11-12
Nikaona nikasikia sauti ya malaika wengi pande zote za kile kiti cha enzi, na za wale wenye uhai, na za wale wazee, na hesabu yao ilikuwa elfu kumi mara elfu kumi na elfu mara elfu, wakisema kwa sauti kuu, Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka.


Tafadhali Kanisa sikilizeni kile ambacho kilitokea maishani mwangu. Bwana alianza kushughulika nami kupitia kwenye ndoto.  Nakumbuka katika ndoto ile, nilitoka kwenye nyumba yangu. Nilitembea kwenye mitaa yangu ya jirani na nilihisi kama kuna mtu alininyanyua kwa mikono yangu hadi juu mawinguni na nilikuwa nakimbia kwenye mawingu huku nikimtukuza Mungu. Nuru kali sana ilinijia na sauti kutokea humo ilisema, “Ricardo, Ricardo. Acha kazi yako maana kuna jambo nataka kufanya na maisha yako pamoja na Kanisa langu lililoko duniani.” Baada ya kusikia maneno haya, nilitetemeka sana na kuamka kutoka usingizini. Niliinuka na kuanza kumlilia Mungu na kumwuliza, “Hii ni nini, Bwana?”

Sauti ile ilinijia kwa nguvu sana. Ilinijia kwa siku nyingi. Kisha nililala tena na kuota ndoto ileile na Bwana alirudia ujumbe uleule kwangu. Kila ilipokuja nikawa naamka napiga kelele kwa sababu sauti ya Mungu inakuwa inakuja kwa nguvu zaidi. Na ninapoamka ninatetemeka, ninapiga kelele na wazazi wangu wananiuliza, “Kuna nini?” Nikawa nawasimulia ile ndoto na mama yangu aliniombea na kuniambia, “Kama ni Bwana anasema na wewe, basi atakupatia ufahamu wa kuelewa.”

Tuliendelea kuomba usiku kucha hadi ilipofika wakati wangu wa kwenda kazini asubuhi iliyofuata. Mama yangu aliniambia nijiweke tayari kwenda kazini. Tulimwomba Bwana ishara ili tujue iwapo alikuwa ni Yeye aliyezungumza nami au la. Nilioga, nikajiandaa, kisha nikaenda kazini. Nilikuwa nikifanya kazi “Chile Laboratories.”

Kwa kweli niliipenda kazi yangu. Nilikuwa nikichukuliwa na gari kutoka kituoni na kwenda kazini. Niliposhuka tu kwenye gari, mtu mmoja alinimbia, “Unafanya nini hapa? Hautakiwi kuendelea kuwapo mahali hapa.”

Kwa mara kadhaa, watu wengine nao waliniambia jambo hilohilo. Cha ajabu ni kuwa hata hawakuwa wameokoka. Hii ndiyo ishara ambayo Bwana alinipa. Baada ya ishara ile, niliamua kwenda kwa bosi wangu kuacha kazi. Nilimwambia, “Ni lazima niondoke kwenye kampuni hii kwa sababu Mungu ameniambia nifanye hivyo.” Bwana akitoa amri ni LAZIMA tutii. Bosi wangu akawa na wasiwasi na mimi, akaniuliza, “Utaenda kufanya nini sasa? Utapata wapi kazi nyingine nzuri kama hii?” Nikamwambia kuwa ni lazima nimtii Mungu. Kwa hiyo, waliandaa sherehe ya watu elfu mbili kwa ajili ya kuniaga mimi. Baada ya hapo, nilikusanya kila kitu changu na kuelekea nyumbani.

Nilipofika nyumbani huku ningali nalia, mama yangu alikuwa tayari ananisubiri kwenye kibaraza cha mbele ya nyumba. Nilimwambia kuwa nimeacha kazi kwa sababu Bwana amethibitisha ndoto yangu kupitia watu wale. Akajibu, “Kama Bwana amesema nawe, basi na ayatumie maisha yako kama apendavyo.” Tuliingia ndani ya nyumba na kuongea hadi usiku ukaingia. Kisha nikamwambia kuwa nahitaji kwenda kulala kwa sababu Mungu atasema nami ndotoni usiku ule.

Nilidhani Bwana angezungumza nami ndotoni lakini hakufanya hivyo kama nilivyowaza. Lakini alikuwa anaenda kushughulika nami kwa njia tofauti. Nilipoenda chumbani kwangu na kuvua nguo zangu, chumba kilianza kutikisika. Nikaanza kupiga kelele, “Kuna tetemeko linalopiga hapa Santiago, Chile.” Nilijaribu kutoka kwenye chumba changu; lakini mtu nisiyemwona alikuwa akinizuia kutoka mlangoni. Niliweza kuwaona mama na ndugu zangu nje ya chumba; na nikapiga kelele za kuomba msaada lakini hakuna aliyekuwa akinisikia. Sasa najua kuwa yule aliyekuwa haonekani alikuwa ni malaika wa Bwana. Nilirudi nyuma na kulala kitandani na kumlilia Mungu, huku nikimwomba anieleze kile kilichokuwa kikiendelea pale.

Ndipo nikasikia sauti ya waziwazi ikisema nami. Roho Mtakatifu alianza kusema na mimi kwa sauti nzuri sana. Aliniambia, “Ricardo, kwa kuwa sasa umeshaacha kazi yako, nataka uende Kanisani na ukaombe kwa saa saba kwa siku kila siku kwa ajili ya maisha yako, na kwa ajili ya Kanisa langu duniani.”

Bwana alipomaliza kuzungumza, chumba kiliacha kutikisika. Ndipo nikanyosha mkono wangu kupitia mlangoni nikagundua kuwa kumbe sasa naweza tena kutoka. Nikakimbia hadi kwa mama yangu na kusema, “Nimesikia sauti ya Roho Mtakatifu!” Nikatoka nje ya nyumba na kuanza kusema hivyo kwa sauti ya juu kule nje.

Baadhi ya watu hawaamini kuwa Mungu bado anazungumza na wanadamu leo; lakini nakuambia anafanya hivyo kabisa! Kama Bwana alizungumza na Ibrahimu, bado anaweza kuzungumza nasi, Kanisa lake, leo! Nilienda Kanisani na kuzugumza na askofu na tukakubaliana kufungua kanisa kila siku saa mbili asubuhi ili niweze kuomba na kutii agizo la Mungu. Kila asubuhi nikawa nakwenda kuomba kwa saa moja, mbili na inapofika ya tatu, nakuwa sina tena kitu cha kuomba. Nikawa namwuliza Mungu, “Bwana, niombee nini tena sasa? Bado nina saa nne mbele!”

Kisha, nikasikia ngurumo chini ya ardhi ikianzia mlango wa nyuma wa kanisa. Nilihisi kanisa likiyumba toka kushoto hadi kulia kama mtu aliyelewa. Wakati huu, Bwana aliongea nami kwa sauti ya wazi kabisa lakini si kwa sauti aliyotumia kwenye ndoto hapo kabla. Sauti aliyosema nami kabla ilikuwa ya mamlaka. Safari hii aliongea kwa sauti ya huzuni na masikitiko. Alisema, “Ricardo, Ricardo, ombea Kanisa langu! Kanisa langu haliko tena kama lilivyokuwa!! Kanisa langu limepoteza imani yake. Kanisa langu haliniamini Mimi wala kuamini juu ya uwepo wangu! Liambie Kanisa langu kwamba Mimi nipo!! Liombee Kanisa langu, maana Kanisa langu haliombi wala kufunga tena!” Hatimaye ule mtikisiko ukakoma baada ya kuwa amemaliza kuongea nami.

Ndipo na mimi nikaanza kuombea Kanisa huku nikitembea humo kanisani kwa saa zile nne zilizobakia; nikiomba watu wa Mungu waamke.

Alhamisi ya wiki ya pili ya maombezi, niliamka nilikuwa na maumivu makali sana ya mifupa na maungio hivyo sikutaka kuamka. Mama yangu alikuwa ananiamsha ili niende kanisani kuomba; lakini nililalamika kuwa mwili wangu na mifupa yangu ilikuwa na maumivu. Kwa hiyo badala yake alipendekeza niombee nyumbani. Lakini nikamkumbusha kwamba Mungu alisema kuwa natakiwa kuombea kanisani. Kwa hiyo, aliniandalia nguo na akanipeleka kanisani. Asubuhi ile walikuwapo watu wengi wakiomba kanisani na nikaomba waniombee kwa sababu ya yale maumivu ya mwili. Niliwaambia kuwa nilikuwa najisikia mdhaifu sana kuomba. Kwa hiyo, walinipaka mafuta na kuniombea, nami nikapokea nguvu isiyo ya kawaida kutoka kwa Mungu!! Haleluya! Nilianza kuomba nikitembea, huku nikimwomba Mungu rehema kwa ajili ya taifa la Chile na familia na watu wanaotumia dawa za kulevya na Kanisa.

Nilimaliza maombezi, kisha nilirudi baadaye jioni kwa ajili ya ibada. Baada ya baraka za askofu, niliinua mikono yangu na nikahisi kuna mtu amepita na kunigusa mgongoni. Hapo nilipotewa na nguvu zote na kuanguka sakafuni. Askofu aliuliza kuna tatizo gani kwangu nami nikamwambia kuwa sijui, sina tu nguvu na hata kuongea naongea kwa shida. Kisha Kanisa lilinizunguka na kuanza kunena kwa lugha na kupaza sauti. Matokeo yake, baadhi ya waumini waliweza kumwona malaika aliyekuja na kunitaka nitoke kwenye mwili wangu. Askofu akasema, “Hautatoka kwenye mwili wako!” Aliposema hivi, yule malaika akaacha kuniashiria nitoke kwenye mwili wangu. Unajua, mtu yeyote mwenye mamlaka katika Yesu ataheshimiwa na malaika wa Bwana.

Ndipo askofu aliniuliza mimi, “Malaika anataka kukutoa kwenye mwili wako kwa muda gani?” Nilimwuliza yule malaika, “Unataka kunichukua kwa saa moja? Mbili? Saa tatu?” Malaika akajibu, “Hapana. Hautakuwapo kwa saa 8 ili ukamwone Yesu kwenye mbingu ya tatu, maana anataka kuzungumza na wewe.” Halafu malaika akaniambia, “Si mimi nitakayekusindikiza hadi mbinguni, maana mimi ni malaika wako mlinzi ambaye nimekuwa ninakulinda kwa siku zako zote ambazo umeishi hapa duniani. Malaika wawili watakuja kutoka mbinguni ili wakuchukue hadi mbingu ya tatu usiku wa manane.” Nilimweleza haya askofu na akaamua kunipeleka kwa gari ya ndugu  mwingine hadi kwenye nyumba ya mchungaji iliyo kwenye ghorofa ya pili. Nilipolala kwenye chumba, tulisikia mbwa wakibweka na watu wakipiga mayowe.

Baada ya kurudi, nilielezwa kuwa watu wawili wakiwa na mavazi meupe walionekana katikati ya mtaa na kutembea hadi kwenye ghorofa ya kwanza ya jengo lile na kuja hadi kwenye ghorofa ya pili nilikokuwa. Malaika hawa walikuwa wazuri sana. Walikuwa na nywele nyeupe zinazomeremeta; nyeupe kuliko theluji, na macho yao yalikuwa na maumbo ya lulu. Ngozi zao zilikuwa laini kama za watoto wachanga lakini miili yao ilikuwa ina misuli kama ya watu wanaojenga misuli. Malaika hawa wana nguvu sana!!!

Nilimweleza askofu kuwa wale malaika wameshafika na kwamba wametumwa kunipeleka mbinguni. Malaika mmoja alianza kutoa ishara ili niweze kutoka ndani ya mwili. Wakati hili linatendeka, mifupa yangu ilianza kuhisi maumivu tena. Kwa hiyo, ndugu zangu katika Kristo waliokuwa karibu yangu walianza kusugua mwili wangu na kuniambia kuwa ulikuwa unapoa kama barafu. Kisha wakaenda kuchukua vipasha joto ili kuupasha moto mwili wangu tena.

Malaika walipokuwa wakiniita nitoke nje ya mwili wangu, nilianza kujisikia kukata tamaa na nikawa najisogeza kutoka upande mmoja hadi mwingine. Nilianza kuhisi mauti inazidi kufunika mwili wangu. Nikawapazia sauti wapendwa katika Kristo, “Msinizike! Nitarudi!”

Nilitoka kwenye mwili wangu na kuruka kitandani mwangu. Niliwaona ndugu zangu katika Kristo wakigusagusa mwili wangu na kusema, “Ameshaondoka. Ametoka kwenye mwili wake.” Lakini nilikuwa hapo tu pembeni yao huku nikiwaambia, “Niko hapa!” Hata hivyo, hawakuweza kuniona wala kunisikia maana nilikuwa na mwili wa kiroho usioharibika. Walianza kuufunga mwili wangu kwa blangeti.

Mmoja wa wale malaika akaniambia, “Ni wakati wa kuondoka, maana Bwana anakusubiri!” Kila malaika alinishika mkono mmoja na wakaninyanyua kuelekea mbinguni huku tukiwa tunakatisha kwenye anga kwa kasi kubwa mno. Nakwambia hivi, hata kama huamini haya, Yesu Kristo wangu ni halisi na yu hai milele!!

Baadaye Bwana alipokuja kuniambia nirudi kwenye mwili wangu, nilimwambia, “Ni nani duniani ambaye ataniamini? Acha tu nibaki na Wewe hapa!! Hakuna mtu atakayeamini ufunuo huu. Hakuna atakayeamini haya kwa kuwa hawana imani! Ukosefu wa imani duniani ni mkubwa sana. Ni nani atakayeamini mambo haya?” Bwana akaniambia, “Yupo mtu ataamini hadithi yako. Wale tu walio kwenye Kanisa langu la kweli watakuamini.”

Nilipotoka kwenye mwili wangu usiku ule na nikawa napaa kwa kasi ya ajabu kwenda kumtembelea Bwana, niliweza kutazama chini kwenye dunia. Kisha nilipita karibu kabisa na mwezi; mwezi huu unaoangazia dunia wakati wa usiku. Halafu niliweza kuliona jua na ukubwa wake kwa macho yangu. Niliweza kuona ndimi za moto zikilipuka na kupasha joto dunia. Tuliendelea kupaa na nikaona nyota nyingi kadiri tulivyopita. Mungu aliniruhusu nione jua, mwezi na nyota kwa makusudi maalum. Makusudi hayo ni kuwaambia ninyi nyote kuwa Mungu wetu ni Muumba Mkuu wa ulimwengu wote!!! Yeye si mdogo hata kidogo!

Tuliendelea kusafiri kwa kasi sana hadi tukafika mahali ambako hakuna nyota hata moja. Hakuna kitu, ni giza tu. Nilitazama chini na kuziona nyota zote chini yangu. Nikaanza kuogopa na kuwauliza malaika, “Mnanipeleka wapi? Tafadhalini mnirudishe duniani kwenye mwili wangu!” Kisha waliniminya kwa nguvu na kuzungusha miguu yao mmojammoja kwenye miguu yangu na kunishikilia. Nilianza kuinama katika mkao ambao ni kama wa hatari kwa sababu ya hofu. Malaika wakasema, “Kaa kimya! Tunakupeleka kwenye mbingu ya tatu ambako Yesu anakusubiri ili azungumze nawe!” Wale malaika walisimama, na wakati huo nilikuwa naangalia kila upande lakini sikuona kitu chochote kilichoumbwa. Sijui nilikuwa wapi lakini nadhani ilikuwa ni kwenye mbingu ya pili.

Nilikuwa najikakamua katika mkao wa hatari wakati malaika wamenishikilia na nilihisi na kusikia sauti ya kutisha kama vishindo vya watu wakikimbia. Malaika walinishikilia kwa nguvu na kusema, “Ricardo, usiogope. Yesu yuko pamoja nasi!” Wakati wakiongea, pia walisema, “Geuza kichwa chako na utazame juu!”

Nilishangazwa na kile nilichokiona maana kulikuwa kama na viumbe wanajongeajongea juu yetu. Mmoja wa wale malaika akasema, “Tazama, tutakuonyesha kile unachokitazama juu yetu!” Na mmoja wao akafanya ishara kwa mkono kutokea upande mmoja hadi mwingine na anga lote juu yetu likajaa nuru. Baada ya kutokea kwa ile nuru, hakukuwa na kingine zaidi ya mapepo na mashetani wakiwa wamejaa kwenye anga lote. Bwana aliwakemea wote kwa Jina la Yesu!! Biblia ni ya kweli!! Kila kinachoendelea kwenye dunia hii ni kile unachoona kwenye Ufunuo. Yesu anakuja hivi karibuni!! Nawezaje kuwafanya muamini hili? Ni hivi karibuni sana!!

Niliwauliza wale malaika, “Hapa ni wapi?” Mmoja wao akajibu, “Huu ni ulimwengu wa roho wa giza anakoishi shetani na mapepo yake.” Nikaanza kusema, “Kumbe ndiyo maana kuna uovu mwingi sana duniani! Haya mapepo huja duniani kutokea hapa na kusababisha uharibifu wa kila namna na uovu miongoni mwa wanadamu. Dunia imejaa mapepo!!” Kuna mamilioni kwa mamilioni ya mapepo. Idadi yao haihesabiki.


Kisha malaika walianza kuniashiria nitazame kwa makini zaidi na wakanionyesha nyuso za viumbe hawa; na kumbe
wengi wao tayari tunaonyeshwa kwenye televisheni. Viumbe hawa walikuwa ni majitu ya kutisha!! Niliwaona akina Thundercat na Power Rangers na viumbe vingine ambavyo huonekana kwenye sinema za mambo ya kutisha (horror movies). Watengenezaji wote wa sinema na vikatuni hivi wana mikataba na ibilisi ili kutengeneza vitu hivi kwa
ajili ya televisheni na sinema!! Michoro yote hiyo hutoka kwenye ulimwengu wa roho wa giza niliouona. Kwa nini unadhania siku hizi watoto ni wakaidi kiasi hicho?? Ni kwa sababu yale mapepo huwaingia watoto wako pale wanapotazama televisheni zinazoonyesha picha hizo.

Ndiyo maana tunatakiwa kujifunza namna ya kuwafundisha watoto wetu jinsi ya kupambanua kipi cha kutazama na kipi si cha kutazama kwenye televisheni. Malaika aliniambia kuwa yote hayo ni mambo halisi kabisa. Mapepo haya yapo na watu wanafanya mikataba na ibilisi ili kuyaleta duniani.

Mapepo hayo yalianza kunilaani mimi, kanisa, na Baba, na Bwana Yesu na dunia kwa sababu hayamheshimu Mungu wala viumbe wake wowote. Kisha nililiona kabisa pepo linaloitwa Hugo, ambaye ni katuni maarufu kule Chile. Alikuwa anatisha sana kumwangalia. Alikuja karibu yangu na kuniambia, “Tutaenda duniani kote na kuwaua watoto wote!”

Kwa nini unadhani watoto wanaua watoto wenzao? Ni kwa sababu baadhi yao husema kuna kitu kilikuja kutoka kwenye televisheni na kuniambia nifanye hivi au vile. Mapepo haya yanapandikiza chuki duniani. Bwana na aiokoe na kuitakasa Chile!!

Mmoja wa wale malaika akaniambia, “Endelea kutazama!” Na yale mapepo yakasema, “Tumejaribu kuliharibu Kanisa lakini hatuwezi kwa sababu kila tukiua mmoja, basi maelfu wanaibuka kujazia kwenye kifo hicho!” Tangu mwanzo wa Kanisa, shetani amejaribu kuliangamiza, yaani Kanisa linalohubiri Injili ya kweli na kutenda kazi ya Mungu, lakini hawezi kwa sababu Bwana Yesu anatulinda! Utukufu kwa Mungu!

Kisha mapepo yakasema, “Hebu tufanye jambo jipya. Hebu tukaingie ndani ya makanisa, maana wapo wengi ndani humo ambao ni mali yetu! Tutaenda kuwatumia watu hawa kueneza uzushi na migawanyiko miongoni mwa ndugu makanisani. Tutasababisha makanisa kuanguka kupitia uzushi na Roho Mtakatifu atahuzunishwa na kuliacha Kanisa.” Shetani anaenda kila mahali akitafuta kuwaharibu wale wanaopenda haki ya Mungu, kama inavyosema kwenye andiko hili:
Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzunguka-zunguka, akitafuta mtu ammeze.

Sikutaka kuendelea kuangalia mambo yale zaidi. Lakini malaika aliniambia niendelee kutazama matukio yaliyokuwa yanatokea. Niliona mapepo yakiruka kila mahali wakati nyota moja inayong’aa ilipokuwa inakuja.

...........................



Bwana akubariki msomaji wa blog hii. Karibu kwenye sehemu ya 2 na ya mwisho ya ushuhuda huu katika makala yatakayofuata.

No comments:

Post a Comment