Friday, March 30, 2012

Kumkabili Goliati Maishani



MUNGU wa mbinguni huzungumza sana kwa mifano kuliko kwa lugha ya kawaida; ya moja kwa moja. Na mfano mkubwa kabisa ni maisha ya Waisraeli. Maisha yao kwa ujumla wake yalikusudiwa kuwa mfano kwa ajili yetu sisi watu wa leo.


Maandiko yanasema: Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani. (1 Wakorintho 10:11).

Yale waliyopitia ndiyo tunayopitia sisi leo. Kilichowaagusha ndicho kitakachotuangusha na sisi kama hatutatenda kinachotakiwa. Kilichowapa ushindi ndicho kitakachotupa nasi ushindi tukitenda sawasawa.

Wengi wetu tunafahamu kuhusu habari ya Daudi na Goliati.

Ilitokea kwamba kulikuwa na vita kati ya Wafilisti na Waisraeli. Kabla ya makabiliano, Wafilisti walikuwa upande mmoja kwenye mlima, na Waisraeli nao kwenye mlima upande mwingine.

Katika nyakati hizo hakukuwa na bunduki wala mabomu kama leo. Vita vilikuwa vikipiganwa kwa makabiliano ya uso kwa uso; mtu kwa mtu. Askari walitumia mikuki, mapanga, mashoka, mawe na silaha zingine ambazo zilihitaji nguvu za kimwili za binadamu.

Goliati alikuwa ni askari shujaa wa Wafilisti. Alikuwa akitoka kila siku asubuhi na jioni na kusimama juu ya mlima. Kisha, kwa sauti ya juu, akawatukana Israeli na kutamba kwa majigambo na dharau nyingi akisema: Je! Mimi si Mfilisti, na ninyi si watumishi wa Sauli? Jichagulieni mtu, akanishukie mimi. Kama mkiweza kupigana nami na kuniua, sisi tutakuwa watumwa wenu; nami nikimshinda yeye na kumwua, ninyi mtakuwa watumwa wetu, na kututumikia. (1 Samweli 17:8-9).

Ndivyo anavyofanya ibilisi kwako leo. Unapita katika majaribu mazito ambayo umepambana nayo lakini inaonekana kama umefika mwisho. Kila wakati shetani anasema moyoni mwako, “Hii shida mpaka ikuue! Huna cha kufanya! Hutapona kamwe ugonjwa huu! Hata ufanyeje hutoki humu!” n.k.

Lakini je, huyu Goliati alikuwa ni mtu wa namna gani?

Kulingana na maandiko, zamani kulikuwako na uzao wa wanadamu waliokuwa wakijulikana kama majitu. Biblia inasema: Nchi hiyo nayo yadhaniwa kuwa ni nchi ya Warefai; hapo kale Warefai walikaa humo; lakini Waamoni wakawaita Wazamzumi, nao ni watu wengi, wakubwa, warefu, kama Waanaki. (Kumbukumbu la Torati 2:20-21).

Katika Biblia ya Kiingereza, neno Warefai ni giants. Hili ni neno lenye maana ya majitu, mapandikizi, au makubwa sana. Goliati alikuwa ni uzao wa hao Warefai. 

Sasa katika vita hivi kati ya Wafilisti na Waisraeli, maandiko yanasema: Ndipo akatoka Goliathi, wa Gathi, ambaye urefu wake ulikuwa mikono sita na shubiri moja. Alikuwa na chapeo ya shaba kichwani, tena amevaa darii ya shaba; na uzani wake ile darii ya shaba ulikuwa shekeli elfu tano za shaba. Tena amevaa mabamba ya shaba miguuni mwake, naye alikuwa na mkuki wa shaba kati ya mabega yake; na mti wa fumo lake ulikuwa kama mti wa mfumaji; na kichwa cha mkuki wake kilikuwa shekeli mia sita za chuma uzito wake; na mtu aliyemchukulia ngao yake akamtangulia. (1 Samweli 17:4-7). Huyu hakika alikuwa ni pandikizi la mtu kweli kweli!

UREFU WA GOLIATI

Mikono sita na shubiri moja.
Mkono 1 = inchi 18
Mikono sita = 18 X 6 = inchi 108.
Shubiri moja = inchi 9

Ichi 108 + inchi 9 = inchi 117
Hizi ni sawa na sm 274.32 

Watu wengi tunaowaona kuwa ni warefu, wana urefu wa futi kama 6 hivi. Hizi ni sawa na meta 1.8. Lakini Goliati alikuwa na urefu wa futi 9. Hizi ni meta 2.7. Yaani ni meta 3 kasoro sentimeta chache tu!

DARII YA GOLIATI

Darii au dirii ni koti la chuma. Lile la Goliati lilitengenezwa kwa shaba. Hili lilikuwa na uzito wa shekeli elfu tano.
Shekeli 1 = kilo 0.011
Shekeli elfu tano = 5000 X 0.011 = kg 55

Huu ni uzito sawa na mfuko mmoja wa simenti, kisha uongeze kilo tano zaidi. Ina maana kuwa kama angekutupia tu hilo koti lake, unakufa palepale; achilia mbali mkuki na silaha zingine alizokuwa nazo; au yeye mwenyewe akukamate! 

KICHWA CHA MKUKI WA GOLIATI

Kilikuwa na uzito wa shekeli 600
Shekeli 600 X 0.011 = kg 6.6.

Hapa hatuhesabii mpini wake ambao tunaambiwa ulikuwa ni kama mti wa mfumaji. Kimsingi huu si mpini bali ni mlingoti!

Kumbuka kuwa, hapa hatuelezwi chochote kuhusu uzito wa mabamba ya miguuni, mpini wa mkuki, chapeo (yaani kofia) ya shaba aliyovaa, pamoja na upanga wake. Ina maana kuwa vitu alivyokuwa amebeba na kuvaa, vilikuwa na uzito wa karibu kilo mia moja; sawa na gunia moja la mahindi!

Kutokana na jinsi alivyokuwa anatisha, katika kule kutoka kwake kila asubuhi na jioni mbele ya Waisraeli, maandiko yanasema: Yule Mfilisti akasema, Nayatukana leo majeshi ya Israeli; nipeni mtu tupigane. Basi Sauli na Israeli wote waliposikia maneno hayo ya Mfilisti, wakafadhaika na kuogopa sana. (1 Samweli 17:10-11). Goliati aliendeleza tambo hizi kwa siku arobaini!

Je, Goliati wako anayekutisha maishani ni nani? Je, ni ukosefu wa kazi? Ni ugonjwa usiopona? Ni masimango? Ni uchumi mbaya? Ni dawa za kulevya zinakutesa? Ni hofu au mashaka juu ya kesho? Ni uchungu au chuki dhidi ya mtu au watu fulani waliokusaliti?

Hayo yote ndio akina Goliati wa maisha yetu. Huo ndio uhalisia wa maisha. Dunia si mbingu. Shida zikiondoka, dunia itakuwa ni mbingu si dunia tena. Maisha ya dunia ni pamoja na shida na majaribu. 

Ni kweli uko baharini na dhoruba ni kali. Lakini akina Goliati wakikukabili wewe unafanya nini? Unalalamika au kuogopa kama Waisraeli walivyonywea mbele ya Goliati? Au unawaza hata kujiua? Ni kweli kuna nyakati maisha yanatisha mno.

Sasa sikia jibu la Mungu wako aliyekuumba ili uwe mshindi; si uwe wa kushindwa. 

Katikati ya fedheha na matukano ya Goliati, alitokea Daudi; kijana mdogo tu.  Daudi japo alikuwa hata hajafikia umri wa watu waendao vitani, aliamua kumkabili yule pandikizi. Alisema: Wewe unanijia mimi kwa mkuki, bali mimi ninakujia wewe kwa jina la BWANA wa majeshi ya Israeli uliowatukana. Siku hii ya leo atakuua mkononi mwangu, .... Nao jamii ya watu wote pia wajue ya kwamba BWANA haokoi kwa upanga wala kwa mkuki; maana vita ni vya BWANA, naye atawatia ninyi mikononi mwetu. (1 Samweli 17:45-47). 

Daudi alizungusha kombeo lililokuwa na kijiwe kidogo kisha akakiachia. Kijiwe kidogo kilimpata jitu wa kutisha na silaha zake hazikumwokoa. Alianguka chini na kufa palepale!

Elimu, fedha, umaarufu, cheo, ujanja au uwezo wowote wa kibinadamu ni sawa na upanga na mkuki. Kuna shida na majaribu mengi ambayo hayatatuliki kwa upanga au mkuki. Kila mwanadamu ana mahali pake pa kukwamia; lazima! Hapo ni mahali ambapo Goliati anakunanga kila siku na wewe unabakia umeinamisha kichwa tu. 

Labda umefika mahali hapo na ukasema, “Hapa sasa basi. Sina tena cha kufanya.” Ni kweli huna cha kufanya lakini, kama alivyofanya Daudi, liko JINA lipitalo majina yote. Hilo ni jina la YESU! Mkabili Goliati wako kwa jina hilo.  

Goliati ni uzao wa majitu. Atakuja na kwako pia kwa sura mbalimbali! Anatisha! Ana nguvu! Sijui unakabiliana na Goliati gani hivi sasa. LAKINI tunaweza kumkabili, si kwa upanga wala mkuki, bali kwa JINA LA BWANA! 

Bwana anaagiza kwamba, Uwe hodari na moyo wa ushujaa; usiogope wala usifadhaike; kwa kuwa BWANA, Mungu wako, yu pamoja nawe kila uendako. (Yoshua 1:9).

Tena anasema kwamba, Utokapo kwenda vitani kupigana na adui zako, na kuona farasi, na magari, na watu wengi kuliko wewe, usiwaogope; kwa kuwa BWANA, Mungu wako yu pamoja nawe, aliyekukweza kutoka nchi ya Misri. (Kumb. 20:1).

Simama na ahadi ya Bwana. Usiangalie ukubwa wa tatizo au adui yako. Mtazame Yeye aliye Mkuu na Mwaminifu, Yesu Kristo. Ni lazima utashinda!

6 comments:

  1. somo zur sana be blessed

    ReplyDelete
  2. Asante kwa kutembelea blog hii. Mungu akubariki rafiki.

    ReplyDelete
  3. Kaka james John hii ni kazi njema na kubwa sana unayoifanya mbele za Mungu, hakika Bwana atakulipa usipozimia roho.

    Sambamba na hilo nilitamani pia mafundisho haya kuwafikia wengi zaidi ili kama mimi ninavyobarikiwa basi wengine pia wabarikiwe vilevile.Kwa sababu hio nilikuwa naomba kibali kuwa nashare kwa wengine kwa njia mbalimbali kwa lengo hilo, nimeona si vyema kufanya hivo bila kibali chako.

    ReplyDelete
    Replies
    1. Shalom. Asante kwa maoni yako na ni kweli Mungu atusaidie tusizimie moyo hadi mwisho wa safari. Ndugu, unaweza kushare kadiri uwezavyo.

      Delete